Ridhiwani aiomba jamii isaidie kuokoa maisha ya watoto


Sharifa Marira

MBUNGE wa Jimbo la Chalinze, Ridhiwani Kikwete (CCM) ameiomba jamii hasa vijana, kujenga tabia ya kujitolea  damu ili kuokoa maisha ya watu wenye uhitaji katika vituo vya vya afya na hospitali mbalimbali nchini.

Aidha amewahamasisha wananchi kupima afya zao mara kwa mara kwa lengo la kujua maradhi yanayowakabili na kupatiwa matibabu mapema kabla ya magonjwa kukua na kuleta madhara.

Ridhiwani aliyasema hayo juzi Chalinze katika kampeni ya kuchangia damu salama iliyotambuliwa kama " Changia Damu Salama kwa mama na mtoto", ambapo alikuwa ni mgeni rasmi katika kampeni hiyo.

Alisema tatizo la damu ni kubwa na kuna umuhimu wa kuchangia pamoja na kupima afya kila wakati ili kuweza kujikinga ama kutibu magonjwa mapema kabla ugonjwa haujakua.

“Tujitolee damu ndugu zangu kuwa wenye mahitaji ni ndugu zetu,'mama zetu, watoto wetu na watanzania wenginw wenye mahitaji,” alisema.

Aliongeza: “Licha ya kuwa mgeni rasmi, siwezi kuja kuangalia watu wakichangia damu wakati mimi mwenyewe ninayo damu ya kutosha kuchangia.”

Alieleza kuwa takwimu zinaonesha kwamba watoto chini ya umri wa miaka mitano mkoani Pwani wako kwenye hatari ya kupoteza maisha kutokana na upungufu wa damu na kwamba kwa hali hiyo kuna kila sababu ya kuokoa maisha ya watoto hao.

Alisema watoto wenye umri huo wamekuwa wakiongoza kwa kukosa damu kutokana kuugua ugonjwa wa malaria, lakini pia kutofikishwa hospitali mapema.

Ridhiwani alitaja kundi jingine lililo hatarini kuwa ni kinamama wajawazito na majeruhi wa ajali aliosema wamekuwa wakipata tatizo la ukosefu wa damu hasa wanapohitaji kufanyiwa upasuaji.

Share on Google Plus

About Unknown

    Blogger Comment
    Facebook Comment

0 comments:

Post a Comment

Laptop City

Tangazo