Sayansi haijatatua fumbo la kuzeeka


William Shao

Sayansi imechangia sana kuboresha afya na teknolojia ya tiba.

“Ni watu wachache sana katika nchi zinazoendelea wanaokufa kutokana na magonjwa ya kuambukiza au matatizo yanayotokea wakati wa kujifungua,” linasema gazeti la ‘Scientific American’.

Kwa mujibu wa jarida hilo ni kwamba, vifo vya watoto wachanga vimepungua kwa asilimia 75 tangu mwaka 1960. Na kwamba pamoja na maendeleo yote hayo, sayansi haijafanikiwa kurefusha maisha ya mwanadamu.

“Hata baada ya utafiti wa miaka mingi, bado uzee ni fumbo kubwa. Hata hivyo, uthibitisho uliopo unaonesha kwamba mwili huanza kuzeeka wakati ambapo maagizo katika chembe za urithi ambazo hudhibiti ukuzi huacha kufanya kazi vizuri,” linasema toleo jingine la jarida la Scientific American.

Makala hiyo inaendelea kusema hivi: “Ikiwa kuzeeka kunasababishwa na utendaji wa chembe za urithi, inawezekana kwamba siku moja tatizo hilo likatatuliwa.”

Katika jitihada zao za kutafuta sababu za kuzeeka, ikiwa ni pamoja na magonjwa yanayohusiana na uzee, wanasayansi fulani wanachunguza maendeleo ya hivi karibuni katika elimu ya chembe za urithi inayoitwa ‘epigenetics’.

Ni nini kinachohusika katika elimu ya epigenetics? Kila chembe hai ina habari ambazo zinahitajika ili chembe mpya zifanyizwe. Nyingi ya habari hizo zinapatikana katika ‘genome’, yaani, mkusanyiko wa habari zote zilizo katika chembe za urithi.

Hata hivyo, katika miaka ya hivi karibuni, wanasayansi wameanza kuchunguza kwa undani zaidi utendaji mbalimbali ndani wa chembe, yaani, kuchunguza ’epigenome’, neno linalomaanisha kihalisi, “juu ya genome” yaani, jinsi habari iliyo ndani ya chembe za urithi itakavyotumika.

Taaluma hiyo ya kuchunguza utendaji huo pamoja na utendaji wa kemikali zilizomo ndani ya chembe inaitwa epigenetics.

Molekuli zinazofanyiza epigenome hazifanani hata kidogo na chembe za urithi. Chembe za urithi zinafanana na ngazi iliyojipinda, lakini epigenome ni alama au vibandiko vyenye kemikali ambavyo hujibandika juu ya chembe za urithi.

Epigenome’ hufanya kazi gani? Kama kiongozi anavyoongoza kwaya, ‘epiginome’ huelekeza jinsi habari zilizo kwenye chembe za urithi zitakavyotumiwa.

Vibandiko hivyo vya molekuli hutendesha au kuzima chembe fulani za urithi kulingana na mahitaji ya chembe na mambo mengine yanayohusiana na mazingira ya mtu, kama vile aina ya vyakula anavyokula, mkazo anaokabili, na sumu anayopumua.

Ugunduzi wa hivi karibuni kuhusu jinsi chembe za urithi zinavyoelekezwa umebadili sana maoni ya watu kuhusu sayansi ya biolojia ambayo inahusianisha utendaji wa chembe za urithi na magonjwa na hata kuzeeka.

“Utendaji wa chembe za urithi umehusianishwa na magonjwa kama vile ‘schizophrenia’, baridi-yabisi (rheumatism), kansa, na maumivu ya kudumu,” anasema mtafiti wa utendaji wa chembe za urithi, Nessa Carey. 

Kwa hiyo, uchunguzi wa utendaji wa chembe za urithi unaweza kuleta matibabu yanayoweza kuboresha afya, kutibu magonjwa, ikiwa ni pamoja na kansa, na hivyo kurefusha maisha.

Hata hivyo, kwa sasa, bado wanasayansi hawajafaulu. “Bado tunatumia mbinu za zamani za kukabiliana na uzee, unatakiwa kula mboga nyingi na kufanya mazoezi,” anasema Carey.

Hata hivyo, kwa nini wanadamu wanajihangaisha sana kurefusha maisha yao? Kwa nini tunataka kuishi milele? Gazeti ‘The Times’ la Uingereza liliuliza hivi:

“Kwa nini wanadamu duniani kote wanahangaika sana kubuni njia za kuendelea kuishi, iwe ni kupata uhai usioweza kufa, ufufuo, kuendelea kuishi baada ya kifo, au kuzaliwa upya katika mwili mwingine?” Kama tulivyoona, jibu la swali hilo litatusaidia kujua sababu hasa kwa nini tunazeeka. Lakini hadi kufikia hatua hii, hata baada ya utafiti wa miaka mingi, bado uzee ni fumbo kubwa.

Share on Google Plus

About Unknown

    Blogger Comment
    Facebook Comment

0 comments:

Post a Comment

Laptop City

Tangazo