Afrika, Korea Kusini wajadili maendeleo ya viwanda

Mwandishi Maalumu, Seoul, Korea Kusini

Dk Philip Mpango
MKUTANO wa Tano wa Ushirikiano kati ya Afrika na Korea Kusini (KOAFEC), ulifunguliwa jana jijini hapa, ajenda kuu ikiwa ni namna nchi za Afrika zinavyoweza kutumia kilimo katika muktadha wa maendeleo ya viwanda ili kujikwamua kiuchumi.

Katika mkutano huo unaohusisha nchi 54 za Afrika na Korea Kusini, Rais John Magufuli anawakilishwa na Waziri wa Fedha na Mipango, Dk Philip Mpango, ambaye aliuelezea kuwa utaleta mapinduzi katika nchi za Afrika ikiwamo Tanzania kwa kuwekeza kwa kiasi kikubwa kwenye kilimo, rasilimaliwatu na Teknolojia ya Habari na Mawasiliano-TEHAMA.

Dk Mpango alisema licha ya Korea Kusini kupata uhuru mwaka mmoja na Ghana, mwaka 1954 miaka michache kabla ya Tanzania Bara, imepiga hatua kubwa kimaendeleo na kuwa moja kati ya nchi za dunia ya kwanza kiuchumi, lakini Ghana na Tanzania bado ni masikini.

“Ni jambo zuri, tuimarishe ushirikiano na Korea Kusini ili njia walizotumia kupiga hatua kubwa kimaendeleo, nasi tuweze kujifunza kwa haraka,” alisema Dk Mpango.

Alisema baadhi ya mawaziri wa fedha aliozungumza nao walisema uongozi thabiti wa nchi na uwekezaji mkubwa katika rasilimaliwatu na kilimo cha kisasa, vinaweza kukwamua nchi za Afrika kuondokana na umasikini.

“Ni muhimu elimu na ujuzi tuvisisitize tunapoanza hatua ya kujenga Tanzania mpya kwa nguvu zaidi, lakini jambo lingine ni kwamba kilimo ndio msingi ambao watu wengi wanaishi wakitegemea hivyo mkutano huu unaendana na mkakati wetu wa Mpango wa Pili wa Maendeleo wa Taifa,” alisema Dk Mpango.

Mkuu wa Idara ya Utafutaji Rasilimali kutoka Serikali ya Mapinduzi Zanzibar, Sabra Issa Machamo alisema uhusiano wa Zanzibar na Korea Kusini ni wa kuigwa na nchi hiyo inafadhili mradi mkubwa wa kilimo cha umwagiliaji unaotarajiwa kujengwa visiwani humo.

Awali akifungua mkutano huo, Naibu Waziri Mkuu wa Korea Kusini, ambaye pia ni Waziri wa Fedha, II Ho YOO, alisema Serikali yake imeamua kuwekeza kiasi kikubwa cha rasilimali zake kuendeleza nchi za Afrika kupitia sekta za kilimo, rasilimali watu na viwanda.

Alisema mkazo mkubwa utakuwa kushirikisha sekta binafsi kusisimua uchumi wa nchi zinazonufaika na mpango huo ili kuharakisha maendeleo yao.
Share on Google Plus

About Unknown

    Blogger Comment
    Facebook Comment

0 comments:

Post a Comment

Laptop City

Tangazo