Lowassa aendelea kulia na Tume ya Uchaguzi


Suleiman Msuya

MWAKA mmoja tangu Uchaguzi Mkuu ufanyike nchini, aliyekuwa mgombea urais kwa tiketi ya Chadema, Edward Lowassa amesema alishindwa kutokana na Tume ya Uchaguzi isiyo huru.

Aidha, Waziri Mkuu huyo wa zamani amesema pamoja na mafanikio machache katika baadhi ya maeneo kwenye utawala wa sasa, maisha ya Watanzania yamezidi kuwa magumu.

Lowassa alisema hayo kwenye taarifa yake aliyoitoa kwenye vyombo vya habari jana, mwaka mmoja baada ya Watanzania kupiga kura Oktoba 25 mwaka jana, ambapo alisema anasononeshwa na hali ya sasa ya Watanzania na ingawa bado ana ari, nguvu na hamasa katika mapambano ya kisiasa.

“Hatutaki kuendelea kulilia maziwa yaliyokwishamwagika ambayo hayazoleki, lakini kile ambacho tulikisema wakati ule kwa nini tunataka mabadiliko, hivi sasa kila mtu anakiona,” alisema Lowassa na kuongeza:

“Ajira imeendelea kuwa bomu linalosubiri kulipuka, elimu bure iliyoahidiwa sivyo inayotekelezwa, utumishi wa umma umekuwa kaa la moto.”

Alisema anakumbuka Oktoba 25 mwaka jana, akisema ilikuwa siku muhimu kwa Watanzania na yeye binafsi, ambapo aliongoza wananchi kupiga kura akiwa mgombea wa upinzani.

“Naamini nilileta sura na msisimko mpya katika siasa za Tanzania,” alisema Lowassa.

Aliongeza:“Nilishirikiana na wenzangu kuionesha nchi demokrasia maana yake ni nini na kuwa kukosekana kwa Tume ya Uchaguzi iliyo huru ni sababu ya sisi kushindwa.

“Ninapogeuka nyuma kuingalia siku ile, nasikia faraja kubwa sana hasa kwa jinsi Watanzania walivyotuunga mkono na kuonesha matumaini makubwa kwetu.”

Alisema katika kipindi hicho, mkewe Regina naye alionesha ujasiri na ushupavu wa hali ya juu ambao ulimpa nguvu kubwa.

Hata hivyo, alisema kwa hali ilivyo sasa, anasononeka kuona viongozi wanavyoshindana kuweka ndani madiwani na viongozi wengine wa kuchaguliwa hasa wa vyama vinavyounda Umoja wa Katiba ya Wananchi (Ukawa).

Mbunge huyo mstaafu wa Monduli alishukuru wananchi kwa imani waliyoonesha kwake na Ukawa na kwamba kumalizika kwa uchaguzi mmoja ndio mwanzo wa uchaguzi mwingine.

“Mapambano ndiyo kwanza yameanza. Kwa kasi, nguvu, ari na hamasa niliyonayo ni kubwa zaidi kuliko wakati mwingine wowote,” alisema Lowassa.

Mjumbe huyo wa Kamati Kuu ya Chadema alisema chini ya Mwenyekiti Freeman Mbowe, waliendesha kampeni za kiungwana kama walivyoahidi.

“Upepo ule ulivuma kwa kasi mpaka visiwani ambako Maalim Seif Sharif Hamad aliporwa dhahiri ushindi,” alisema.

Uchaguzi uliofanyika mwaka jana matokeo ambayo yalitangazwa na Tume ya Taifa ya Uchaguzi (NEC), Lowassa  alipata kura zaidi ya milioni 6.7 huku Rais John Magufuli akipata kura zaidi ya milioni 8.9.
Share on Google Plus

About Unknown

    Blogger Comment
    Facebook Comment

0 comments:

Post a Comment

Laptop City

Tangazo