Makinda ahimiza huduma bora hospitali za umma


Joyce Anael, Moshi

Anne Makinda
MWENYEKITI wa Bodi ya Mfuko wa Taifa wa Bima ya Afya (NHIF), Anne Makinda, amezitaka hospitali na vituo vya afya vya umma kutoa huduma bora ikiwa ni pamoja na kuhakikisha zina vifaatiba na dawa.

Makinda alitoa rai hiyo jana kwenye ofisi ya Mkuu wa Mkoa wa Kilimanjaro mjini hapa akisema watu binafsi wamekuwa wakinufaika na fedha za huduma ambazo zinatolewa na NHIF kutokana na vituo vya umma kushindwa kutoa huduma nzuri na bora.

Alisema ipo haja sasa Serikali kuhakikisha kuna vifaa vya kutosha kwenye vituo vya afya na hospitali za Serikali, ili kutoa huduma bora na nzuri na kuvutia wananchi wengi zaidi.

"Hospitali za umma ni za muda mrefu, majengo yapo hivyo wanaweza kutoa huduma bora na wananchi wakaenda huko, ni suala tu la kujipanga," alisema.

Alisema watu binafsi wamekuwa wakichangamkia fursa za NHIF kwa kutoa huduma nzuri na bora, na kufanya wananchi kukimbilia huko badala ya vituo vya umma ambavyo  vimeonekana kushindwa kutoa huduma nzuri.

Kaimu Mkurugenzi Mkuu wa NHIF, Bernard Konga alisema fedha nyingi zinazotoka katika mfuko huo, zimekwenda vituo binafsi na maduka ya dawa ya binafsi, licha ya Serikali kuwa na vituo vingi na hospitali nyingi nchini hususan vijijini.

Alisema tatizo kubwa katika vituo na hospitali za Serikali kwa sasa ni upungufu wa dawa, hivyo kuna haja ya kuliangalia suala hilo kwa makini na kuhakikisha fedha zinazotolewa kwa ajili ya dawa zinatumika kwa ajili ya dawa badala ya kupelekwa kwenye maeneo mengine.

Mkuu wa Mkoa wa Kilimanjaro, Saidi Sadick aliiomba NHIF kufuatilia mkopo ulioombwa na Hospitali ya Rufaa ya Mkoa huo, wa Mawenzi kwa  ajili ya kujenga duka la dawa na kuuwezesha kutoka, hatua ambayo itasaidia kupunguza adha ya wagonjwa kwenda kununua dawa kwa gharama kubwa katika maduka ya dawa ya binafsi.

Share on Google Plus

About Unknown

    Blogger Comment
    Facebook Comment

0 comments:

Post a Comment

Laptop City

Tangazo