Waliotusua waanika siri ya ushindi wao


Waandishi Wetu

Japhet Elia Stephano
KINARA wa matokeo ya darasa la saba, Japhet Stephano wa Shule ya Msingi Kwema wilayani Kahama mkoani Shinyanga ambaye ni mtoto wa mjasiriamali Elia Ntinyako ametaja siri ya mafanikio yake kuwa ni kumwomba Mungu, kusoma kwa bidii na kusikiliza walimu na wazazi.

Stephano alisema hayo jana katika mahojiano maalumu na JAMBO LEO muda mfupi baada ya matokeo ya Mtihani wa Kumaliza Elimu ya Msingi kutangazwa na Baraza la Mitihani la Tanzania (NECTA) Dar es Salaam.

Alisema amelelewa katika maadili na kanuni za imani ya dini yake, pamoja na kutojihusisha na michezo na makundi yasiyo na sababu.

“Nilikuwa napenda masomo yote, ila siri kubwa ya ushindi ni kumwomba Mungu na kufuata maelekezo mema ya wazazi wangu ambao mara kwa mara walinisimamia katika masomo ya kawaida nay a ziada ili kutimiza ndoto zangu. Nitahahikisha hata kidato cha nne naongoza pia,” alisema.

Alisema awali hakutarajia kuwa angeongoza kutokana na ushindani ulivyokuwa mkubwa shuleni kwao ambapo kuanzia darasa la kwanza walikuwa wakigombea nafasi ya kwanza hadi tano.

Stephano alisema malengo yake ya baadaye ni kuwa Mhandisi wa Ujenzi wa Miundombinu na kwamba anajua hilo linahitaji aongeze bidii na juhudi katika masomo.

Hata hivyo, alisema changamoto kubwa aliyokumbana nayo katika kutafuta elimu hiyo kukosa kushiriki michezo na wanafunzi wenzake, kwani muda mwingi aliutumia kujisomea.

Baba wa mwanafunzi huyo, Ntinyako alisema siri ya mafanikio ya kijana wake ni kujisomea na kuwasikiliza kile ambacho wanamwelekeza.

Alisema walichofanya ni kuhakikisha wanafuatilia masomo kwa kuwasiliana na walimu na kukagua madaftari wakati wa likizo na anaposoma masomo ya ziada.

“Kwanza alihakikisha hashiriki starehe za kwenda fukweni, ingawa tunaishi karibu na Ziwa Tanganyika ambako kuna zaidi ya fukwe tatu,” alisema.

Ntinyako alisema pamoja na ugumu wa maisha alihakikisha anasomesha watoto wake kwenye shule nzuri akiamini kuwa elimu ndiyo mkombozi wao na kutaka Watanzania wasiogope kusomesha watoto kwenye shule hizo.

“Sisi ni wajasiriamali lakini tumejikaza kisawasawa ili watoto wetu waweze kupata elimu bora ambayo itawasaidia na matunda yake ndiyo kama leo (jana) mnatupigia simu kutupongeza,” alisema.

Jamal Athumani aliyeshika nafasi ya pili kitaifa alisema siri ya mafanikio yake ni kusoma kwa bidii, kumwomba Mungu, ushirikiano kati yake, walimu, wanafunzi wenzake na wazazi.

Jamal alisema walimu wamekuwa na mchango mkubwa katika mafanikio yake kwa kufundisha vizuri na kuahidi kuwa ataendelea kusoma kwa bidii ili afanye vizuri zaidi ngazi zinazofuata.

Mwanafunzi huyo alisema maisha ya nyumbani kwao ni ya kawaida huku akimpongeza mzazi wake, Dk Asha Maneno kwa kumlea vizuri na kuhakikisha anafaulu.

Mzazi huyo naye alisema amefurahishwa na matokeo ya kijana wake kwani kila mara alikuwa akimsisitiza kusoma kwa bidii, nidhamu na mnyenyekevu kwa Mungu na wanadamu.

Mwanafunzi aliyeshika nafasi ya tatu kitaifa ambaye pia anatoka Shule ya Msingi Kwema, Enock Bundala alisema malezi mazuri kutoka kwa wazazi wake ambao muda mwingi walimsimamia kwa karibu katika masomo yake ndiyo siri ya mafanikio yake.

“Napenda masomo ya Sayansi, Hisabati na Jiografia, natamani niwe mhandisi, nawasihi watoto wenzangu wakiwa darasani wazingatie anachofundisha mwalimu kwani ndiyo siri ya mafanikio, pia kumwabudu na kumpa nafasi zaidi Mungu,” alisema.

Baba wa mwanafunzi huyo, Daud Bundala alisema matokeo hayo aliyatarajia kutokana na mtoto wake kujisomea kwa bidii na kumwabudu Mungu hivyo anajipanga zaidi kumwendeleza.

Mama wa Enock, Anastazia Shija alisema: “Jina la Mungu lihidimiwe. Siri ni malezi bora kwa mtoto, hasa kuepuka makundi rika maovu na kusimamia kwa umakini matendo yake kuanzia nyumbani hadi matembezini kwa kubaini aina ya marafiki.”

Katika hatua nyingine, mama wa mwanafunzi bora wa kike,Justina Gerald kutoka Shule ya Msingi Tusiime ya jijini Dar es Salaam, Dk Edna Majaliwa alisema amefurahi binti yake kuongoza wasichana wote wa Tanzania kwani alikuwa anajitahidi shuleni.

“Mwanangu alikuwa msikivu, alijituma na alikuwa anafanya uamuzi mkubwa kama mtu mzima ila shangazi yake alimtabiria kuwa atakuja kuwa wa kwanza siku moja,” alisema.

Dk Majaliwa ambaye ni bingwa wa magonjwa ya watoto katika Hospitali ya Taifa Muhimbili (MNH), alisema Justina anapenda kusoma vitabu, kuangalia filamu na kusaidia watoto wa mitaani.

Akizungumzia shule yake kuwa ya kwanza kitaifa, Mkurungezi wa Shule ya Msingi Kwema, Pauline Mathayo alisema siri kubwa ya mafanikio yake ni kumtanguliza Mungu katika shughuli zake pia jitihada za walimu wanaofundisha kwa weledi.

Alitoa mwito kwa walezi na wazazi wasichanganywe na ukali wa maisha ya sasa na yajayo kwa kuwa jukumu lao ni kuongoza watoto katika malezi bora na si bora malezi.

“Kwanza wawafundishe Neno la Mungu na kudhibiti michezo isiyo na tija,” alisema.

Alitaja sababu nyingine ya watoto kufanya vizuri kuwa ni ushirikiano wa wazazi, walimu na wanafunzi, akisema wazazi wamekuwa wakiwafuatilia watoto wao kwa karibu.

Mathayo alisema shule hiyo ina walimu 31 ambao ni Watanzania wote na darasa hilo lilikuwa na wanafunzi 50.

Meneja wa Shule, Emanuel Ang’ulo alisema ushindi huo umetokana na ukaribu wa Mkurugenzi wao kwa walimu wake kuwajali kimaslahi hali inayowapa moyo wa kuwa na bidii ya kufundisha na kuwajenga kisaikolojia.

Mkuu wa Shule, Michael Luhaga ambaye ni mwalimu wa Sayansi, alisema alitarajia matokeo hayo kutokana na juhudi zilizokuwa zikioneshwa na wanafunzi hao.

Mwalimu wa darasa la saba, Adili Majogolo alisema Japhet alikuwa na uwezo mkubwa kitaaluma na alipenda zaidi masomo ya Sayansi akiwa na ndoto za kuwa mwanasayansi siku zijazo.

“Amekuwa akishika nafasi ya kwanza na wakati mwingine ya pili au ya tatu, hakuwahi kushuka zaidi ya hapo,” alisema.

Alisema Jamal na Enock wanapenda kusoma na ni watulivu hali ambayo ilisababisha wasaidiane kwenye masomo.

Mwalimu Mkuu wa Shule ya Msingi Tusiime, Philibert Simon alisema mwanafunzi huyo alikuwa akiongoza katika mitihani ya ushindani iliyokuwa ikifanyika ambapo kati ya mitihani 32 alikuwa anaongoza 19.

Alisema mwanafunzi huyo amekuwa wa kipekee kwenye usomaji na kuna wakati ukifika muda wa kupumzika na wanafunzi kuungana kucheza alikuwa haendi na badala yake alijificha na kujisomea.

Mkurugenzi Mkuu wa Tusiime, Albert Katagira aliishukuru Serikali kwa kubadili mfumo wa alama katika upangaji matokeo na kwamba wangekuwa nafasi ya juu zaidi.

Habari hii imeandikwa na Suleiman Msuya, Celina Mathew, Magreth Magoso na Neema Sawaka
Share on Google Plus

About Unknown

    Blogger Comment
    Facebook Comment

0 comments:

Post a Comment

Laptop City

Tangazo