Hofu ukosefu wa dawa yatanda Ocean Road


Emeresiana Athanas


BAADHI ya wagonjwa katika Hospitali ya Taasisi ya Saratani ya Ocean Road iliyoko jijini Dar es Salaam, wamelalamikia kukosa huduma kwa muda mrefu kutokana na uhaba wa dawa.

Wagonjwa hao walilieleza gazeti hili kwa nyakati tofauti kuwa baadhi yao wamekaa hospitalini hapo kwa zaidi ya miezi sita bila tiba.

Walisema tatizo la kukosa dawa ni la muda mrefu na imekuwa kawaida kwa madaktari kuwaandikia dawa na wagonjwa kutakiwa kwenda kununua kwenye hospitali binafsi nje.

Mmoja wa wagonjwa hao (jina tunalifadhi kwa usalama wake) aliyesema kuwa ametoka mkoani Kigoma, alisema dawa katika hospitali hiyo hazipo.

"Mara nyingi utakuta unaandikiwa dawa lakini unapokwenda katika duka la dawa huzikuti na hivyo kutakiwa kutafuta nje ya
taasisi hiyo," alisema.

Mgonjwa huyo aliyeeleza kuwa yuko hospitalini hapo kwa kipindi cha miezi sita sasa, alifafanua kuwa mara nyingi zile dawa muhimu ndio hukosekana katika duka hilo.

Kuhusu huduma ya upimaji mionzi alisema hizo zimekuwa zikicheleweshwa kutolewa kutokana na sababu wasizo zijua.

"Kama unavyojua mtu unaweza fika hospitalini ukiwa na hali mbaya baada ya kuzunguka katika hospitali mbalimbali lakini cha
ajabu huduma hiyo pamoja na kuwa muhimu bado haitolewi kwa wakati.

Alisema yeye alifika Ocean Road akiwa na maumivu makali lakini akatakiwa kurudi baada ya miezi mitatu akielezwa kuwa dawa hazipo.
"Wakati huo nilikuwa na maumivu makali lakini nikatakiwa nirudi baada ya miezi kadhaa. Kwa sababu nilikuwa nimezidiwa nikalazimika kurudi mapema zaidi na ndipo nilipolazwa,” alisema.

Mgonjwa mwingine alisema Ocean Road hakuna dawa na hilo limekuwa likileta usumbufu mkubwa kwa wagonjwa. "Mfano dawa aina ya 'Akemi' zinauzwa ghali na hivyo kutulazimu kuchukua muda mrefu kuzipata na kwa wakati huo unakuwa hupatiwi huduma hadi utakapo zipata hizo dawa," alisema.

Alisema tatizo lingine aliloona ni upande wa mionzi. “Kama mimi tangu nifike sijapimwa sasa hili linawapa tabu hata wanaotuuguza kwani wengine hatuna ndugu na uwezo wetu ni mdogo.” Alisema.

Alisema suala hilo linaumiza hivyo kuiomba Serikali kuhakikisha inalishughulikia mapema ili kuwaondolea wagonjwa hao usumbufu.

Mgonjwa mwingine aliyejitambulisha kwa jina la mama John alisema kuwa suala la ucheleweshwaji wa huduma ya mionzi linawapa changamoto kubwa.

Mgonjwa mwingine alisema upatikanaji wa dawa ni hafifu hospitalini hapo na hivyo kuitaka Serikali ishughulikia suala hilo mapema.

Alisema tangu afike hospilitani hapo amekuwa akisafishwa vidonda tu na siyo kupewa dawa kwa kuwa dawa hazipo.

Mmoja wa madaktari wa taasisi hiyo ambaye hakutaka kutajwa gazetini kwa kuwa siyo msemaji alikiri tatizo hilo akifafanua kuwa la muda mrefu.

"Ukosefu wa dawa upo mkubwa tu kutokana na Bohari ya Dawa (MSD), kutokutuletea kwa muda sasa, lakini mimi sio msemaji hivyo itakuwa vizuri ukifika kwa Mkurugenzi atakupa ufafanuzi zaidi kuhusu suala hilo," alisema.

Hata hivyo, Mkurugenzi wa Ocean Road, Julius Mwaisalage hakutaka kutoa ushirikiano kwa mwandishi wa habari hii.

Awali, Mkurugenzi huyo alidai kuwa yuko katika vikao Wizara
ya Afya na kumtaka mwandishi amtumie maswali ili ayajibu. Lakini hakusema chochote hata baada ya maswali hayo kumfikia

Hata hivyo, Mkurugenzi wa Bohari ya Dawa (MSD), Laurean Bwanakunu alisema kuwa bohari hiyo haijawahi kusitisha kupeleka dawa Ocean Road.

ALifafanua kuwa “Wiki mbili zilizopita MSD ilipeleka Ocean Road kutoka kwa washirika watatu. Tulipeleka aina kumi za dawa.” Alisema

Aliongeza kuwa bohari hiyo kwa kushirikiana na taasisi hiyo
zimebainishwa dawa kulingana na umuhimu ili uagizaji uendane na uhitaji na kuhakikisha upatikanaji endelevu wa dawa.
Share on Google Plus

About Unknown

    Blogger Comment
    Facebook Comment

0 comments:

Post a Comment

Laptop City

Tangazo