Mtatiro ahimiza viongozi kukumbuka waliowachagua


Mwandishi Wetu

MWENYEKITI wa Kamati ya Uongozi wa Chama cha Wananchi (CUF), Julius Mtatiro, ameomba viongozi walio madarakani kutambua thamani ya kuchaguliwa kwao na kuilipa thamani kwa kuwaletea maendeleo wapiga kura wao.

Mtatiro alisema hayo mbele ya wajumbe waliohudhuria mkutano ulioshirikisha viongozi wa vyama vyenye mlengo wa kimapinduzi Afrika uliofanyika Afrika Kusini hivi karibuni.

Katika hotuba yake iliyopatikana Dar es Salaam, huku akitoa mifano, Mtatiro alisema viongozi wengi wa Afrika wanatumia nguvu kubwa kutafuta madaraka na wakishayapata husahau wananchi kwa kutowapelekea maendeleo.

“Wakati tunapambana kutengeneza demokrasia ya kweli Afrika, ndugu zetu wa vyama tawala wamekuwa wakitumia nguvu kubwa kutafuta madaraka na kukandamiza vyama vya upinzani na wanapoyapata hawawakumbuki tena hata wapiga kura,” alisema.

Mtatiro alisema wakati Waafrika wanapambana kukuza demokrasia na kutafuta maendeleo kwa wananchi, hali imekuwa tofauti kwa vyama tawala ambavyo vimekuwa vikijali sana madaraka bila kukumbuka wapiga kura.

Katika hotuba hiyo, Mtatiro alimnukuu Baba wa Taifa Mwalimu Julius Nyerere ambaye katika hotuba yake mwaka 1960 aliwaambia viongozi kuwa wanapopewa dhamana na kuaminiwa na watu wanatakiwa kulipa uaminifu huo kwa kuwaletea maendeleo.

Aliwataka wajumbe wa vyama vya upinzani waliohudhuria mkutano huo kuunganisha nguvu na kushirikiana kuhakikisha demokrasia ya kweli inapatikana Afrika pamoja na kuwaelekezea maendeleo wananchi ambao ndio wapiga kura.

“Kwa pomaja tukishirikiana na kushikana mikono, tunaweza tukapambana na madhila ambayo sisi vyama vya upinzani tumekuwa tukifanyiwa na vyama tawala na pengine kwa miaka ijayo tutaweza kuonja matunda ya demokrasia ya Afrika,” alisema.

Mkutano huo wa siku mbili uliofanyika Johannesburg, ulihudhuriwa na viongozi wa vyama vya upinzani wa ukanda wa nchi za Jumuiya ya Maendeleo Kusini mwa Afrika (SADC).
Share on Google Plus

About Unknown

    Blogger Comment
    Facebook Comment

0 comments:

Post a Comment

Laptop City

Tangazo