Meya Ubungo kujulikana Jumanne ijayo


Fidelis Butahe

Boniface Jacob
SIKU tano baada ya kuahirishwa kwa uchaguzi wa Meya na Naibu Meya wa Manispaa ya Ubungo, Mkurugenzi wa Manispaa hiyo, John Kayombo ameitisha tena uchaguzi huo Jumanne ijayo.

Uchaguzi huo uliahirishwa baada ya kususiwa na vyama vinavyounda Ukawa kwa madai ya kupewa taarifa ndani ya muda mfupi, kuongezwa kinyemela kwa idadi ya madiwani na kupinga ‘uhuni’ uliofanyika katika uchaguzi wa Manispaa ya Kinondoni, baada ya wateule wa Rais nao kuruhusiwa kupiga kura.

Kwa mujibu wa barua ya Kayombo ya Oktoba 24 kwa madiwani wote wa Manispaa ya Ubungo, kutakuwa na mkutano wa Baraza la Madiwani Novemba mosi kwa lengo la kufanya uchaguzi huo.

Akizungumza na JAMBO LEO, Diwani wa Ubungo, Boniface Jacob ambaye pia ni mgombea wa umeya wa Manispaa hiyo, alisema barua hiyo imefuata sheria na taratibu kwa kutolewa wiki moja kabla ya uchaguzi huo.

“Kwenye uchaguzi wa awali barua yao ilieleza kuwa ulikuwa wa dharura jambo ambalo si sahihi. Wametambua makosa yao na pia ule haukusema kuwa kutakuwa na mkutano wa Baraza la Madiwani,” alisema.

Kuhusu idadi ya madiwani, Jacob alisema ni lazima waibuke na ushindi, kwa sababu Chadema na CUF kwa pamoja wana idadi kubwa ya madiwani kuliko CCM.

“CUF ina madiwani wawili, Chadema 10 pamoja na wabunge wawili, CCM wana madiwani wawili. Madiwani wa viti maalumu, CCM wana mmoja na Chadema watatu. Kwa takwimu hizo tayari tumeshashinda,” alisema.

“Katika uchaguzi wa awali pia tulikataa uamuzi wa Mkurugenzi kutaka Mwasa (Salama wa CUF) na Lyimo (Susan wa Chadema) kupiga kura Ubungo wakati wanaishi Kinondoni.

“Katika uchaguzi huu hatutakubali pia wajumbe hawa kupiga kura maana wanastahili kushiriki uchaguzi wa Kinondoni,” alisema.

Alifafanua kwamba kwa kuwa waliokuwa wagombea wa umeya na naibu meya wa Kinondoni walifungua kesi kupinga matokeo ya wagombea wa CCM, wana imani Mahakama itatenda haki ili wahusika washiriki kuchagua meya kihalali.
Share on Google Plus

About Unknown

    Blogger Comment
    Facebook Comment

0 comments:

Post a Comment

Laptop City

Tangazo