Morocco kujenga Msikiti, uwanja wa soka


Celine Mathew

SERIKALI za Tanzania na Morocco zimetiliana saini mikataba 21 ya kiuchumi na biashara, huku Mfalme wa Nchi hiyo, Mohammed VI akikubali maombi ya Rais John Magufuli kujenga Msikiti mkubwa Dar es Salaam na uwanja mkubwa wa mpira Dodoma, vitakavyoanza kujengwa mara moja.

Utiaji saini mikataba hiyo ulitangazwa jana Ikulu, Dar es Salaam katika siku ya pili ya ziara ya siku sita ya Mfalme huyo, kati ya mikataba hiyo ukiwamo wa usafiri wa anga kutoka Rabat hadi Dar es Salaam na askari 150 kwenda nchini humo wiki ijayo kwa ajili ya mafunzo.

Akizungumza Ikulu, Rais Magufuli alisema historia kati ya Tanzania na Morocco ilianza kujengwa miaka ya 1631 na kwamba mikataba hiyo itaisaidia Tanzania kuwa nchi ya viwanda ifikapo mwaka 2025.

“Namshukuru Mfalme kwa kuja na wafanyabiashara, lakini katika maongezi yake ameniambia kuwa mwaka jana, nchi hiyo ilipokea watalii zaidi ya milioni 10.5 na kwamba mwaka huu wanatarajia kupokea milioni 14,” alisema.

Alisema Mfalme huyo alimhakikishia kuwa Shirika la Ndege Tanzania (ATCL), litashirikiana na la Morocco kuhakikisha usafiri unakuwa mzuri na ndege zinasafiri kutoka nchini humo hadi Dar es Salaam.

Rais Magufuli alisema Mfalme huyo alimhakikishia kuwa nchi hiyo itashirikiana na Tanzania, lengo likiwa ni kukuza uchumi unaotarajiwa kufikia asilimia 7.9 ifikapo mwishoni mwa mwaka huu.

Aliongeza kuwa Tanzania ipo kwa ajili ya kujenga uchumi wa kisasa kutokana na uwepo wa madini tofauti hivyo kumhakikishia Mfalme huyo kuwa ni eneo zuri la kuweka wawekezaji.

Hata hivyo, Rais Magufuli alisema Mfalme huyo alimwomba aongeze siku moja nchini ambapo alimruhusu na kumsisitiza kuwa hata kama anataka tatu akae tu.

Mikataba

Mikataba hiyo ni pamoja na makubaliano ya jumla katika ushirikiano wa kiuchumi, Sayansi, kiufundi na kitamaduni baina ya Serikali ya Morocco na Tanzania ambao ulisainiwa na Waziri wa Mambo ya Nje na Ushirikiano wa Afrika Mashariki, Dk Augustine Mahiga na Waziri wa Mambo ya Nje wa Morocco, Alahddine Mezouar.

Mkataba mwingine ni wa kuanzishwa kwa Jukwaa la Ushauriano wa Kisiasa baina ya Wizara ya Mambo ya Nje ya Tanzania na Morocco kati ya Dk Mahiga na Mezouar wa Morocco.

Mwingine ni wa sekta ya gesi, nishati, madini, sayansi ya miamba kati ya Tanzania na Morocco ambao ulisainiwa na Waziri wa Nishati na Madini, Profesa Sospeter Muhongo na Mezouar.

Aidha, mkataba wa usafiri wa anga baina ya Tanzania na Morocco ambao ulisainiwa na Waziri wa Ujenzi, Uchukuzi na Mawasiliano, Profesa Makame Mbarawa na Mezouar.

Mkataba wa Mradi wa Mtangamano wa kuwasaidia wakulima wadogo nchini ambao ulisainiwa na Waziri wa Kilimo, Mifugo na Uvuvi, Dk Charles Tizeba na Aziz Akhannouch wa Morocco.

Pia mkataba wa sekta ya uvuvi ambao ulisainiwa na Dk Tizeba na Akhannouch, Mkataba wa Maendeleo ya Nishati mbadala baina ya MASEN na Wizara ya Nishati na Madini ambao ulisainiwa na Katibu Mkuu wa Wizara ya Nishati na Madini, Profesa Justin Ntalikwa na Mwenyekiti wa MASEN, Moustapha Bakkoury.

Mkataba kati ya Bodi ya Utalii nchini pamoja na Kamisheni ya Utalii Zanzibar na Ofisi ya Utalii ya Taifa la Morocco ambao ulisainiwa na Mkurugenzi Mtendaji, Devota Mdachi na Mtendaji Mkuu wa Ofisi ya Taifa ya Utalii Morocco, Abderrafie Zouiten.

Mingine ni kundi la utoaji mikopo la Morocco na Benki ya Maendeleo ya Kilimo Tanzania, Shirika la Bima la Taifa Tanzania (NIC), Shirika la Bima la Morocco (MAMDA) kwa ajili ya maendeleo ya bima ya mazao nchini.

Aidha mkataba baina ya kundi la SNTL la Morocco na Mamlaka ya Maeneo Maalumu ya Uwekezaji (EPZA), ya Tanzania katika ubia wa uendelezaji na utangazaji wa nguzo za viwanda.

Pia mkataba baina ya Mamlaka ya Usafirishaji ya Taifa ya Morocco na kampuni Hodhi ya Rasilimali za Reli Tanzania (RAHCO), kwa ajili ya ubia ili kuendeleza reli ya Mtwara-Mchuchuma/ Liganga.

Mwingine ni kati ya Baraza la Bishara baina ya Shirikisho la Wafanyabiashara wa Morocco (CGEM) na taasisi ya Sekta Binafsi Tanzania (TPSF), baina ya Benki ya BOA na Hospitali ya CCBRT ili kuiwezesha kujiendesha. 
Share on Google Plus

About Unknown

    Blogger Comment
    Facebook Comment

0 comments:

Post a Comment

Laptop City

Tangazo