Kidato cha nne kilingeni leo


Suleiman Msuya

JUMLA ya watahiniwa 408,442 wamesajiliwa kufanya mtihani wa kidato cha nne mwaka huu unaoanza leo, imeelezwa.

Kati yao, 355,995 ni wa shule na 52,447 ni wa kujitegemea ikilinganishwa na watahiniwa 448,382 wa shule wa mwaka jana.

Katibu Mtendaji wa Baraza la Mitihani Tanzania (NECTA), Dk Charles Msonde alibainisha hayo wakati akizungumza na waandishi wa habari jana Dar es Salaam.

Alisema kati ya watahiniwa wa shule 355,995 wavulana ni 173,423 sawa na asilimia 48.72 na wasichana ni 182,572 sawa na asilimia 51.28, huku wasioona 59 na wenye uoni hafifu wakiwa 283.

Dk Msonde alisema kati ya watahiniwa 52,447 wa kujitegemea, 25,529 sawa na asilimia 48.68 ni wavulana na 26,918 sawa na asilimia 51.32 ni wasichana huku wasioona wakiwa saba; wanawake watatu na wavulana wanne; mwaka jana walikuwa 54,317.

Alisema katika Mtihani wa Maarifa (QT), jumla ya watahiniwa 20,634 walisajiliwa kufanya mtihani huo mwaka huu, wanaume ni 7,819 sawa na asilimia 37.89 na wanawake ni 12,815 sawa na asilimia 62.11; mwaka jana walikuwa 19,547.

“Watahiniwa nchi nzima naamini wameajiandaa vya kutosha, hivyo ni vema wakazingatia misingi ya taratibu za mitihani kwani hatutavumilia mtu atakayejaribu kudanganya,” alisema.

Alisema maandalizi kwa ajili ya mitihani hiyo yamekamilika ikiwa ni pamoja na kuisambaza mitihani pamoja na vijitabu vya kujibia na nyaraka zote muhimu katika mikoa yote Tanzania Bara na Visiwani.

Umuhimu

Akizungumzia umuhimu wa mtihani huo, Dk Msonde alisema ni kupima uwezo na uelewa wa mwanafunzi katika aliyojifunza kwa miaka minne.

Dk Msonde alisema matokeo ya mtihani huo yatatumika kuchagua wanafunzi wa kujiunga na kidato cha tano na fani mbalimbali za utaalamu wa kazi kama vile afya, ualimu, kilimo, ufundi na nyinginezo.

Katibu Mtendaji huyo alisema mikakati yao ni kuhakikisha wanakuwa na taarifa ambazo zitaonesha idadi ya wanafunzi walioanza darasa la kwanza hadi la saba.

Katika mtihani wa mwaka jana, wahitimu ambao walifaulu mtihani wa kidato cha nne walikuwa robo ya wahitimu wote, hali ambayo ilionesha kuwa ufaulu hakuwa mzuri.
Share on Google Plus

About Unknown

    Blogger Comment
    Facebook Comment

0 comments:

Post a Comment

Laptop City

Tangazo