Mahakama ya Mafisadi mbioni kuanza


Sharifa Marira, Dodoma

Jaji Mkuu Othman Chande
MAHAKAMA ya Mafisadi iko mbioni kuanza kazi baada ya Jaji Mkuu, Othman Chande, kukamilisha kanuni za uendeshaji wake pamoja na mafunzo kwa majaji husika.

Aidha, imebainika kuwa mamlaka ya serikali za mitaa inaongoza kwa vitendo vya rushwa kisekta nchini kutokana na kesi nyingi zinazoendelea mahakamani.

Hayo yalisemwa jana mjini hapa na Waziri wa Nchi, Ofisi ya Rais, Menejimenti ya Utumishi wa Umma na Utawala Bora, Angellah Kairuki, mbele ya Kamati ya Bunge ya Utawala na Serikali za Mitaa wakati akiwasilisha taarifa kuhusu hali ya rushwa nchini, utendaji wa Taasisi ya Kuzuia na Kupambana na Rushwa (Takukuru), pamoja na mikakati ya kutokomeza rushwa.

Alisema mashauri yatakayofunguliwa kwenye Mahakama hiyo yatachukua miezi tisa pekee kumalizika.

Alisema kesi za rushwa zilizo mahakamani kuanzia mwaka wa fedha 2014/15 hadi Juni ni 509, kati ya hizo, serikali za mitaa zinaongoza kwa kuwa na kesi 209 sawa na asilimia 41 ikifuatiwa na sekta ya afya yenye kesi 63 sawa na asilimia 12.

Alisema katika mwaka wa fedha 2015/16 sekta hiyo iliongoza kwa kuwa na majalada mengi ya tuhuma za rushwa, kati ya 3,082 yanayoendelea na uchunguzi huku majalada 1,357 sawa na asilimia 44 yakihusu Mamlaka hiyo.

Akizungumzia mafanikio yaliyopatikana katika jitihada za kupambana na rushwa, alisema Takukuru kupitia uchunguzi na mashitaka iliokoa Sh bilioni 43.78 katika kipindi cha Julai, 2015 hadi Septemba 2016.

“Fedha hizo zilitokana na kitengo cha ufuatiliaji wa fedha na mali za watuhumiwa ambazo zilipatikana kwa njia ya rushwa na kutaifishwa,” alisema Kairuki.

Wajumbe wa Kamati hiyo walieleza kuwa chanzo cha rushwa ni adhabu ndogo zinazotolewa kwa wahalifu huku wengine wakidai kuwa mifumo iliyopo ndiyo inasababisha rushwa kuendelea kukua.

Mwenyekiti wa Kamati hiyo, Jasson Rweikiza alisema adhabu inayotolewa ni ndogo na kushauri Serikali kufanyia marekebisho sheria ziendane na za nchi zingine akitolea mfano wa China ambako watu wa makosa makubwa hunyongwa.

Alisema adhabu ya mtu kuiba mamilioni ya fedha na kufungwa miaka miwili au mitatu jela inafanya wananchi wengi kuendelea kufanya ubadhirifu na wanapokamatwa hukubali kifungo ili wakitoka waendelee kula raha na fedha walizoiba.

Mbunge wa Welezo, Saada Mkuya (CCM) alizungumzia rushwa ya ngono kuwa ni tatizo kubwa na kwamba utendaji wa Takukuru katika kushughulikia jambo hilo unawapa wasiwasi wananchi.
Share on Google Plus

About Unknown

    Blogger Comment
    Facebook Comment

0 comments:

Post a Comment

Laptop City

Tangazo