Greencity ilivyojipanga kung’ara kielimu nchini


Warioba Igombe

KUPATA elimu iliyo bora ni moja ya haki za msingi za mtoto, ndio maana malengo ya Serikali yamejikita katika kuendeleza elimu nchini kwa namna yoyote iliyo bora.

Kuwapatia wanafunzi elimu bora ndiyo shabaha ya msingi ya Sera ya Elimu na Mafunzo ya Mwaka 2014. Pia ni shabaha ya Sera zilizokuwepo kabla ya hii tangu uhuru mpaka sasa.

Kusaidiana na Serikali, wadau wa elimu mkoani Morogoro walianzisha Shule ya Sekondari ya Greencity kwa lengo la kuwapatia wanafunzi elimu bora.

Sekondari ya Greencity ipo Mkundi Manispaa ya Morogoro. Uongozi wa shule hii unasema umejipanga kuleta mapinduzi kwenye sekta ya elimu nchini.

Shule hii ilianza rasmi mwaka 2013, ikiwa na wanafunzi 51 wa kidato cha kwanza, ambao kuanzia Novemba mosi wanatarajia kuanza mtihani wa taifa wa kumaliza elimu ya kidato cha nne.

Katika matokeo ya mtihani wa moko shule hiyo imeshika nafasi ya 16 kati ya 47 kwa sekondari zilizopo Manispaa ya Morogoro.

Mkuu wa Shule ya Sekondari ya Greencity, Jonathan Mwachipa, anabainisha kuwa lengo ya shule yake ni kuhakikisha wanafunzi wake wanapata matokeo mazuri katika mitihani ya taifa.

Kutokana na lengo hilo, uongozi wa shule hii umetenga muda wa jioni kila siku wanafunzi kujisomea kwa kupitia masomo yote waliyofundishwa ili kupata uelewa zaidi.

Mwalimu Mwachipa anaeleza kuwa kitendo cha wanafunzi kutumia muda wa jioni kujikumbusha masoma waliyofundishwa, kimekuwa chachu ya matokeo mazuri katika mtihani wa moko ukilinganisha na shule nyingine ambazo ni kongwe mkoani Morogoro.

“Pamoja na uchanga wa shule yetu, wanafunzi wamefanya vizuri katika mtihani wa moko. Hii ni dalili nzuri kwa vijana wetu kuelekea mtihani wao wa mwisho wa taifa kidato cha nne,” anasema.

Anasema kuwa wanafunzi 75 walifanya mtihani wa moko, na kati yao wasichana ni 31 na wavulana 44, ambapo waliopata daraja la kwanza walikuwa ni 13 wasichana wakiwa 11 na wavulana wawili.

Mkuu huyo anasema waliopata daraja la pili ni wanafunzi 21, daraja la tatu 35 na daraja la nne wanafunzi sita, hakuna aliyepata sifuri. Katika matokeo hayo wanafunzi wengi wamefanya vizuri masomo ya sayansi hususani somo la baolojia na kemia.

Pamoja na elimu bora inayotolewa darasani, mkuu huyo anasema mandhari nzuri ya shule na hewa safi inachangia wanafunzi wao kufanya vizuri katika masomo yao.

“Kwa ujumla kwa sasa shule yetu ina wanafunzi 340 kati yao wasichana ni 239 na wavulana 10,” anasema.

Pia anasema mbali na kutumia njia mbalimbali zinazofanywa na walimu ili kuhakikisha wanafunzi wanafaulu, wana wastani ambao ni lazima mwanafunzi aufikie ili aendelee na darasa linalofuata.

“Mwanafunzi kuingia darasa linalofuata lazima afikishe wastani wa alama 50. Utaratibu huu umewasaidia wanafunzi wengi kufanya vizuri darasani. Hakuna mwanafunzi anayeingia darasa lingine kwa ‘huruma’ ni alama tu tulizoziweka ndizo zinamvusha mwanafunzi,” anasema mkuu huyo.

Wastani huo humfanya mwanafunzi atumie muda mwingi kusoma bila kusukumwa na mtu ili aweze kuvuka hicho kikwazo na hivyo kufanya vizuri darasani.

Anasema wanafunzi wake wamepania kuhakikisha wanafanya maajabu kwa kuwa na ufaulu mzuri utakaowawezesha wote kwenda kidato cha tano.

Mwachipa anasema ili kuhakikisha inafanya mapinduzi ya elimu nchini, shule tayari imeanzisha kidato cha tano na cha sita.

Mbali na hayo, anasema ni ukweli ulio wazi kuwa wamepata mafanikio ya kutia moyo ingawa bado wana kazi kubwa ya kuendeleza mbele safari.

Wanafunzi wajivunia wastani

Mmoja wa wanafunzi wa shule hiyo, Happiness Jumanne, anayesoma kidato cha tatu anasema utaratibu wa shule kuweka wastani ili kila mwanafunzi aufikishe ni mzuri kwani unasaidia kumfanya mwanafunzi anapojiandaa na mitihani akumbuke kwamba anapaswa kuvuka alama 50 ambazo ni wastani wa masomo yote.

“Wastani unamfanya mwanafunzi kusoma kwa bidii kila wakati ili asishindwe kufikisha wastani uliowekwa na shule na hivyo kwenda darasa linalofuata,” anasema Happiness.

Kwa upande wake, William Jonathan, anayesoma kitado cha pili anasema wastani wa alama 50 huongeza ushawishi kwa wanafunzi kusoma kwa bidii.

“Kwa mwanafunzi anayefikisha wastani uliowekwa na shule humrahisishia mwanafunzi husika kufanya vizuri katika mitihani ya taifa.

Huu utaratibu humjengea mwanafunzi kujiamini na kujituma katika masomo yake hivyo kujibu mtihani wowote ule kwa urahisi,” anasema.   

Jina la Greencity lilivyopatikana

Mkuu huyo anasema kuwa shule hiyo iliamua kutumia jina la Greencity baada ya mmiliki wake, Ramadhan Mrema, kuona kuwa maeneo ya shule hiyo yana mimea iliyosheheni rangi za kijani.

Anasema mwaka 2013, wakati shule hiyo ikijengwa kulikuwa na mimea iliyosheheni rangi ya kijani hali iliyomshawishi kutumia jina la Greencity akiamini kuwa mazingira yao yatakuwa chachu ya maendeleo shuleni hapo.

Changamoto

Kuhusu changamoto, Mwachipa anasema shule yake inakabiliwa na kutokuwa na uzio na kwamba mikakati yao kwa sasa ni kutafuta ufumbuzi wa tatizo hilo.





Share on Google Plus

About Unknown

    Blogger Comment
    Facebook Comment

0 comments:

Post a Comment

Laptop City

Tangazo