Mbunge adai kuingiziwa fedha chafu kwenye akaunti ya U-DC


Fidelis Butahe

MBUNGE wa Makete (CCM), Profesa Norman Sigalla amesema ameijulisha Taasisi ya Kuzuia na Kupambana na Rushwa (Takukuru) kuhusu  sakata la kuingiziwa kiasi cha Sh. milioni 5 katika akaunti yake ya benki, akisema hajui aliyeidhinisha alipwe.

Amesema kuanzia Januari hadi Aprili mwaka huu, aliingiziwa Sh. milioni 1.2 katika akaunti hiyo  na kwamba haziwezi kuwa za mshahara wa ukuu wa Wilaya ya Songea kwa sababu aliacha wadhifa huo tangu Julai mwaka jana, baada ya kuteuliwa na Tume ya Taifa ya Uchaguzi (NEC), kugombea ubunge wa Makete na kushinda.

Sigalla alitoa kauli hiyo jana katika kipindi cha Power breakfast kinachorushwa na Redio Clouds Fm, baada ya kudaiwa kupokea mshahara wa ukuu wa wilaya wa miezi mitano wakati akiwa mbunge.

“…Nikavijulisha vyombo vya usalama kama Takukuru, watizame huyu anayeingiza fedha anaingiza kwa nia gani, kwanini ahuishe akaunti ya mkuu wa wilaya ambayo imefungwa, kwanini haingizi hizo fedha zote, zingine zinakwenda kwa nani?” alihoji.

“Nilipomaliza ukuu wa wilaya akaunti yangu ilisimamishwa na hakuna fedha nilizolipwa. Sasa iweje baada ya miezi sita kupita ndio nianze kuingiziwa fedha.”

Katika ufafanuzi wake Sigalla alisema, Juni mwaka huu aliandikiwa barua na Katibu wa Bunge, akielezwa kuwa amepokea barua kutoka kwa Katibu Tawala mkoa wa Ruvuma, ikieleza kuwa mbunge huyo alikuwa akipokea mishahara miwili, ya ubunge na ukuu wa wilaya.

“Akaunti hii ambayo mshahara wa ukuu wa wilaya ulikuwa ukipitia kwa sasa ndio ninayopitishiwa mshahara wa ubunge…,nilipopewa ile barua nilihamaki na nilichofanya ni kukimbilia benki kuchapisha bank statement (taarifa binafsi za kibenki), kuanzia siku niliyoacha ukuu wa wilaya hadi mwezi Juni nilipopewa barua hiyo,” alisema.

“Nilipoitazama sikuona mshahara wa Sh milioni 4.6 ukiingia…, baadaye tulikwenda mbali zaidi…, tuligundua kuwa kuna Sh milioni 1.2 imeingia kuanzia Januari hadi Aprili na fedha hiyo haionyeshi  inaingizwa na nani zaidi ya kusomeka salary transaction.”

Alipoulizwa sababu za kutobaini kuingizwa kiwango hicho cha fedha, alisema haikuwa rahisi kwake kubaini hilo.

“Agosti mwaka huu nilimwandikia barua  Katibu wa Bunge na kumtajia kiwango cha fedha kilichoingia katika akaunti yangu (Sh milioni 5) na kumwomba kikatwe katika mshahara wangu wa ubunge au malupulupu na kirudishwe Hazina,” alisema.

“Nikasema anayeingiza (fedha hizo) achukuliwe hatua ili aeleze ameingiza kwa nia gani, pili akaunti hii ilikuwa haiingizi fedha zozote za mkuu wa wilaya, sasa iweje imefufuka na kuingiza kiasi hicho cha fedha, ni kitu gani, maana huo si mshahara wa mkuu wa wilaya.”

Alisema ili  mtu aweze kufungua akaunti iliyofungwa anahitaji kuwa na nywira na kusisitiza mtu huyo ni rahisi kumbaini.

“Hii si bahati mbaya. Ingekuwa baada ya kuacha ukuu wa wilaya na fedha kuendelea kuingia tungesema ni bahati mbaya, lakini ilishafungwa kwa miezi sita, sasa unapoifungua si bahati mbaya, je ulitumwa,” alisema.
Share on Google Plus

About Unknown

    Blogger Comment
    Facebook Comment

0 comments:

Post a Comment

Laptop City

Tangazo