Waziri Mkuu ‘agawa’ bodaboda 200 Arusha


Mwandishi Wetu

Kassim Majaliwa
WAZIRI Mkuu, Kassim Majaliwa, ametangaza kukabidhi pikipiki 200 zenye thamani ya sh. milioni 400 kwa vijana 200 wa Jiji la Arusha waliokuwa wakiendesha pikipiki za watu binafsi zisizo na tija, ili kuweza kuwakwamua kiuchumi na kujitegemea kwa mapato.

Majaliwa amegawa pikipiki hizo ambazo zimechangwa na wadau mbalimbali wa maendeleo mkoani Arusha baada ya Mkuu wa Mkoa huo. Mrisho Gambo kubuni mpango huo kwa lengo la kuwawezesha vijana kupata pikipiki bila riba wala dhamana.

Waziri Mkuu alikabidhi pikipiki hizo juzi baada ya kumaliza kuhutubia maelfu ya wananchi waliohudhuria katika mkutano wa hadhara kwenye Uwanja wa Sheikh Amri Abeid.

“Nawataka vijana mhakikishe mnakuwa waaminifu kwa kufanya kazi kwa bidii ili pikipiki ziweze kuwasaidia kuwainua kipato,” alisema Majaliwa.

Katika hafla hiyo, Waziri Mkuu alisema mwananchi yeyote hata kama si mtumishi wa umma ana wajibu wa kuiheshimu Serikali na kuitumikia, akiwataka vijana hao pia kuwa waadilifu.

“Serikali ya awamu ya tano imeanza kazi na moja kati ya majukumu yetu ni kuboresha nidhamu ndani na nje ya Serikali hivyo ni lazima ipate heshima yake.”

“Tumeamua kuwatumikia. Tumeamua kuwahudumia Watanzania wote bila ya kujali itikadi zao za kisiasa na kidini na Mheshimiwa Rais anataka kuona wananchi wake akifurahia Serikali yao,” alisema.

Kwa upande wake Gambo alisema pikipiki hizo zilizokabidhiwa kwa vijana hao zimetolewa zikiwa na bima kubwa huku kila Kata ikitoa vijana wanane.

Katika hatua nyingine, Waziri Mkuu alisema zaidi ya Sh. bilioni 800 zimetengwa kwa ajili ya ujenzi wa miradi mbalimbali ya maendeleo mkoani Arusha.

Majaliwa ambaye yuko mkoani Arusha kwa ziara ya kikazi alisema kati ya fedha hizo sh. bilioni 476 zitatumika katika ujenzi wa miradi wa maji ili kumaliza kero hiyo. “Mkoa wa Arusha unakabiliwa na changamoto kubwa ya upatikanaji wa maji safi na salama, hivyo fedha hizo zinalenga kumaliza tatizo hilo ambalo limechangiwa na uharibifu wa mazingira,” alisema.

Alisema kiasi kingine cha Sh. bilioni 264 kilitolewa ili kuimarisha upatikanaji wa umeme wa uhakika katika mkoa huo.
Share on Google Plus

About Unknown

    Blogger Comment
    Facebook Comment

0 comments:

Post a Comment

Laptop City

Tangazo