Serikali yataka wahasibu wabadhirifu waanikwe


Dotto Mwaibale

Dk Philip Mpango
SERIKALI imeitaka Bodi ya Taifa ya Wahasibu na Wakaguzi wa Hesabu (NBAA) kuweka hadharani majina ya wahasibu wabadhirifu ili jamii iwajue.

Hayo yalisemwa juzi na Waziri wa Fedha na Uchumi, Dk Philip Mpango, kwa niaba ya Waziri Mkuu, Kassim Majaliwa wakati akizindua Kituo cha Taaluma ya Uhasibu cha Bunju na Kongamano la Uhasibu la mwaka 2016 la siku tatu Dar es Salaam.

"Ni vizuri mkaanza kuweka hadharani majina ya wahasibu wasio waadilifu ili jamii iweze kuwajua," alisema Mpango.

Mpango alisema kukamilika kwa ujenzi wa kituo hicho, kutaisaidia Serikali kuelekeza fedha zilizokuwa zikitumiwa na Bodi hiyo kukodi kumbi kwa kazi zake na sasa kupelekwa kufanya kazi zingine za maendeleo.

"Nawaombeni mkitunze kituo hiki ili kitimize malengo yake ya kuleta manufaa kwa wananchi na Taifa kwa ujumla," alisema Mpango.

Aliwataka wahasibu nchini kutumia taaluma yao kuisaidia Serikali hasa katika kipindi hiki cha nchi kuelekea kwenye uchumi wa viwanda, badala ya kushirikiana na wafanyabishara wasio waaminifu kuiibia Serikali.

Mkurugenzi Mkuu wa NBAA, Pius Maneno alisema katika kipindi cha miaka 12 iliyopita, walikuwa wakitumia Sh bilioni 1.5 kwa gharama za kumbi hivyo ujenzi wa kituo hicho utaondoa changamoto hiyo na kitakuwa pia chanzo cha mapato.

Mpango alisema Serikali itaendelea ‘kutumbua’ watumishi wasio waaminifu bila kumwonea huruma mhusika na kuwa atakayebainika atapelekwa Mahakama ya Ufisadi.

Mwenyekiti wa Bodi ya NBAA, Profesa Isaya Jairo alisema kituo hicho kimejengwa kwa mkopo wa Sh bilioni 15 kutoka Shirika la Hifadhi ya Taifa (NSSF), Mfuko wa GEPF bilioni 10/- huku wahasibu na wakaguzi wakichangia bilioni 8/-.

Alisema awali walikadiria ujenzi huo ungekamilika kwa Sh bilioni 14 lakini kutokana na sababu mbalimbali, kukamilika kwake kulifikia Sh bilioni 33.

Mwenyekiti wa Bodi wa GEPF, Joyce Shaidi aliishukuru Serikali kwa ushirikiano na mifuko ya jamii na NBAA , hasa katika suala la kusukuma mbele maendeleo ya nchi na kuzitaka taasisi zake kwenda kukodi ukumbi wa kituo hicho cha kimataifa, ili kusaidia kurejesha fedha zilizokopwa kukijenga.

Share on Google Plus

About Unknown

    Blogger Comment
    Facebook Comment

0 comments:

Post a Comment

Laptop City

Tangazo