Rwanda yapitisha 70% ya mizigo Dar


Celina Mathew

Francois Kanimba
WAZIRI wa Biashara na Viwanda wa Rwanda, Francois Kanimba amesema uhusiano wa kibiashara kati ya nchi yake na Tanzania umeimarika na sasa inapitisha asilimia 70 ya mizigo kwenye bandari ya Dar es Salaam.

Kanimba alitoa kauli hiyo jana alipotembelea Bandari hiyo kuona namna inavyofanya kazi na maboresho yaliyofanywa na Rais John Magufuli kudhibiti upotevu wa mizigo uliokuwapo awali.

Katika maelezo yake, Waziri huyo alisema kipindi cha nyuma kulikuwa na upotevu mkubwa wa madini na kukiri kuwa kwa sasa umetoweka.

Alisema baada ya changamoto hiyo, walifanya mazungumzo na watu wa Bandari hiyo kuhakikisha  mizigo ya Rwanda inakuwa salama.

“Nimetembelea Bandari hii kuangalia namna inavyofanya kazi, kwa kiasi kikubwa changamoto hiyo imepungua, japo ilikuwa na matarajio tofauti na ilikuwa ikitugharimu sana, lakini kwa sasa ulinzi umeimarika hivyo mizigo inapita salama,”alisema na kuongeza:

“Kuna mabadiliko makubwa na wafanyabiashara wa Rwanda wanasema Bandari imebadilika kwa kiasi kikubwa na mizigo yetu  inapita kwa asilimia 70.”

Aliongeza kuwa Rwanda na Tanzania zina mpango wa kuanzisha mfumo wa kuagiza mizigo pamoja ambao kwa kiasi kikubwa utawezesha mizigo inayotoka nchi hiyo kuwa salama na kufika kwa wakati.

Alisema pia watahakikisha wanaweka watendaji wazuri na mamlaka zitakazokuwa zinakagua mizigo yakiwamo mashirika ya viwango ya nchi hizo mbili kwa lengo la kuwezesha soko kuwa kubwa na la uhakika.

Kwa upande wake, Waziri wa Viwanda, Biashara na Uwekezaji nchini, Charles Mwijage alisema Tanzania inashika nafasi ya 108 kati ya nchi 189 kwenye masuala ya kuhakikisha biashara zinakwenda vizuri na kwamba hali hiyo, inatokana na ucheleweshwaji wa mizigo kwenye mipaka, mizani na bandarini.

Alisema awali tulikuwa nafasi ya 139 lakini kwa sasa 132, jambo ambalo bado hakijapungua kitu na kwamba hiyo inatokana na changamoto hizo, hivyo wataangalia namna ya kufanya maboresho makubwa kwenye suala hilo ili kuendeleza biashara zilizopo sasa.
Share on Google Plus

About Unknown

    Blogger Comment
    Facebook Comment

0 comments:

Post a Comment

Laptop City

Tangazo