Sababu 11 za kichaa kwa Watanzania

Fidelis Butahe na Suleiman Msuya

SIKU moja baada kuibuliwa kwa utafiti unaoonesha kuwa katika kila watu wanne duniani mmoja ana matatizo ya akili, wanasaikolojia nchini wametaja sababu 10 za ukichaa kwa Watanzania, ikiwamo ya ugumu wa maisha.

Wamesema utafiti huo wa Shirika la Afya Duniani (WHO) ulioibuliwa juzi na Waziri wa Afya, Maendeleo ya Jamii, Jinsia, Watoto na Wazee, Ummy Mwalimu unaweza kuwa wa kweli na kusisitiza kuwa ni suala linaloweza kutokea katika jamii na hivyo halipaswi kupuuzwa.

Sababu zingine ni msongo wa mawazo, kushuhudia mauaji ya kutisha, ajali, kuvamiwa, ubakaji, kurithi kwa wazazi, mazingira, malezi mabaya, kukosa imani ya dini na mmomonyoko wa maadili.

Katika maelezo yake, Mwalimu alisema mwaka jana Tanzania ilionesha kuwa na wagonjwa wa afya ya akili 311,789 kulingana na takwimu za waliokwenda hospitali kuchunguzwa.

Mhadhiri wa Chuo Kikuu Dar es Salaam (UDSM), Kitengo cha Saikolojia, Chris Mauki alisema: “Matatizo ya akili yanachangiwa na mambo mengi na huwa ni tatizo zaidi mijini, ndiyo maana takwimu za utafiti zinaonesha Dar es Salaam inaongoza ikifuatiwa na Mwanza.”

Alisema msongo wa mawazo ni moja kati ya sababu na ambayo inatokana na mtu kusongwa na matatizo na hivyo kuwa na maswali yasiyo na majibu juu ya hatima ya maisha yake.

 “Akili inabeba vitu ambavyo haina uwezo wa kuvimudu na kufikia ukomo wa uwezo wake,” alisema.

Alisema watu kuishi kwenye mazingira magumu katika ukuaji wao huku wakishuhudia matukio hatari kama kuvamiwa, mauaji, ubakaji na ajali, huchangia kwa kiasi kikubwa matatizo ya akili.

“Pia ukikuta mtu aliye kwenye umasikini mkubwa tangu akiwa mdogo huku akishuhudia migogoro isiyokwisha ya wazazi au walezi na na hata anapokua anaendelea kuishi kwenye umasikini, humfanya akose matumaini, hivyo kupata tatizo hili,” alisema Mauki.

“Mtu kutokuwa na imani pia ni tatizo kwani mtu akiwa anamtumaini Mungu hujawa na imani, hivyo anaona hata kama anapitia katika mambo magumu kuna siku atafanikiwa,” aliongeza.

Dk Richard Shukia wa UDSM, Idara ya Saikolojia, alisema kisaikolojia hali ya mtu kuwa kichaa inaweza kutokea katika njia mbili kuu ambazo ni kurithi kwa wazazi au familia husika na kutokana na mazingira yanayomzunguka mhusika.

Mhadhiri Mwandamizi huyo alisema wapo watu ambao wamepatwa na kichaa kutokana na kurithi kwa wazazi, hivyo dhana nzima ya kusimamia utafiti inaweza isiakisi hali halisi.

Alisema wapo wengine wanapata kichaa kutokana na mazingira ambayo yamewazunguka, hivyo moja kwa moja yanaakisi utafiti ukiwamo ya WHO.

“Kichaa au hali ya utukutu inaweza kuwa ya kurithi au mazingira yanayozunguka mfano alichofanya ‘Scorpion’ kwa maelezo ambayo yanasemwa ni mazingira,” alisema.

Aidha, alisema hali hiyo ya ukichaa inaweza kuchangiwa na msongo wa mawazo hali ambayo inasababisha mhusika kuamini kuwa hana cha kupoteza.

Mhadhiri Mwandamizi na Mkuu wa Idara ya Elimu Chuo Kikuu cha Kumbukumbu ya Mwalimu Nyerere (MNMA), Dk Berther Losioki alisema malezi ni sababu ya jamii kuingia katika hali ya ukichaa.

Alisema pamoja na utafiti huo wa WHO bado Tanzania   inapaswa kufanya utafiti ili kuwa na taarifa sahihi ya hali ilivyo jambo alilodai kuwa litasaidia kukabiliana na tatizo.
Alisema familia ambayo imelelewa katika maadili na malezi bora ni ngumu kupatwa na hali ya ukichaa hivyo kuzitaka familia kuishi maisha yenye misingi sahihi ya kifamilia.

Mkuu wa Chuo cha Ustawi wa Jamii (ISW), Dk Abuu Mvungi alisema hajaona utafiti huo wa WHO ila kwa upande wa mmomonyoko wa maadili, anaamini asilimia kubwa unachangiwa na vyombo husika kushindwa kusimamia majukumu yake.

Alisema jamii inaishi itakavyo na wakati mwingine ikichukua hatua za kutaarifu vyombo husika hakuna uamuzi ambao yanachukuliwa yenye tija kwao.

“Mfano ukiangalia historia ya tukio la ‘Scorpion’ unagundua kuwa Jeshi la Polisi halikufanya kazi yake ipasavyo na kama lingetekeleza tukio kubwa lilotokea awali, lile lisingetokea. Wapo ambao watafikiria kuwa utafiti wa WHO ni sahihi kumbe sisi ndio sababu,” alisema.
Share on Google Plus

About Unknown

    Blogger Comment
    Facebook Comment

0 comments:

Post a Comment

Laptop City

Tangazo