Ma-RC watano wanaong'ara


Waandishi Wetu

WAKATI Serikali ya Awamu ya Tano ikianza mwaka wake wa pili madarakani tangu ilipoingia Novemba 5 mwaka jana, wakuu watano wa mikoa wametajwa kung’ara kati ya 26 wa mikoa ya Tanzania Bara.

Wakizungumza na JAMBO LEO kwa nyakati tofauti kuhusu utendaji wa viongozi hao wanaomwakilisha Rais John Magufuli katika ngazi ya mikoa, watu wa kada mbalimbali walitoa maoni yao na kuwataja majina na mikoa wanapofanya kazi.

Wakuu wa mikoa waliotajwa kufanya vizuri katika kipindi hicho ni Mkuu wa Mkoa wa Dar es Salaam, Paul Makonda, Amos Makalla (Mbeya), Antony Mtaka wa Simiyu.

Wengine ni Mrisho Gambo wa Arusha na John Mongella wa Mwanza, wote wakiwa katika umri wa ujana.

Wakuu hao wa mikoa wa Serikali ya Awamu ya Tano wametimiza miezi tisa tangu walipoteuliwa, huku kukiwa na kumbukumbu ya amri tano walizopewa na Rais John Magufuli, wakati wakila kiapo Ikulu, Dar es Salaam.

Kiongozi mkuu huyo wa nchi aliteua wakuu wa mikoa 26 Machi mwaka huu akisema: “Mnakwenda kufanya kazi kwa ajili ya kutatua kero za wananchi. Hamuendi mikoani kutangaza siasa, mnakwenda kutimiza wajibu wenu kwa ajili ya wananchi.”

Aliwataka wawakilishi wake hao wakuu kupambana na ujambazi, kusimamia ilani ya uchaguzi ya CCM, kutatua kero za wananchi, kuzuia vijana kucheza pool table na kusimamia utekelezaji wa elimu bure.

Haikushangaza alipofanya mabadiliko ya wakuu watatu wa mikoa, Juni 26 mwaka huu, ikiwa ni pamoja na kujaza nafasi ya aliyekuwa mkuu wa mkoa wa Shinyanga, Anna Kilango ambaye uteuzi wake ulitenguliwa kutokana na kushindwa kusimamia ipasavyo zoezi la kubaini watumishi hewa.

JAMBO LEO imetafuta maoni ya watu wa kada mbalimbali kuhusu utendaji kazi wa wakuu wa mikoa katika kipindi cha miezi tisa.

Kabla ya kuteuliwa kwao, Rais alitaja vigezo ambavyo angetumia kuwapima wakuu wa mikoa na wilaya, akiwataka kuzingatia suala la upungufu wa madawati, upungufu wa chakula na migogoro ya ardhi.

Wakuu hao wa wilaya walikula kiapo cha kwanza mbele ya Rais na cha pili waliapa kwa pamoja kwa kutumia dakika nane, baadaye walisaini hati ya ahadi ya uadilifu kwa viongozi wa umma, inayotolewa na Ofisi ya Rais, Sekretarieti ya Maadili ya Viongozi wa Umma.

Wakuu hao wa mikoa waliotajwa kufanya vizuri katika kipindi hicho ni Mkuu wa Mkoa wa Dar es Salaam, Paul Makonda, Amos Makalla (Mbeya), Antony Mataka (Simiyu), Mrisho Gambo (Arusha) na John Mongella (Mwanza).

Ofisa Mtendaji wa Chama cha Wafanyabiashara wenye viwanda na Wakulima (TCCIA) mkoani Mbeya, Emile Malinza alisema: “Makalla ni mfano wa kuigwa ikilinganishwa na watangulzi wake. Amefanya mabadiliko makubwa, hasa kwenye bei za bishaa na migogoro kati ya Serikali na wafanyabiashara kuhusu kodi katika soko jipya.”

Alisema mkuu huyo wa mkoa pia amefanikiwa kwa kiasi kikubwa kutatua migogoro ya wakulima na wafugaji. Katika miundombinu hasa wilayani Rungwe waliokuwa wakipata shinda kuvuka mito kutokana na kukosekana kwa madaraja pamoja na kuhakikisha waliopewa viwanda wanaviendeleza.

Mhadhiri wa Chuo Kikuu Dar es Salaam (UDSM), Richard Mbunda alimtaja Mtaka kuwa kiongozi anayefanya kazi bila kuingiza siasa.

Alisema chini ya utendaji wake amebuni mradi wa ‘Mkoa mmoja, bidhaa moja’ lengo likiwa ni kuhamasisha wananchi kujiingiza katika miradi inayoweza kuwaingizia kipato, ikiwemo kuzalisha bidhaa zinazotoka mkoani humo, jambo alilodai kuwa litasaidia kuwaongezea kipato wanancho hao.

 “Mradi huu umekuwa ukitumika katika nchi mbalimbali duniani ikiwemo Japan, akiendelea na utaratibu huu ni wazi kuwa atafika mbali zaidi,” alisema Mbunda.

Gambo naye ametajwa katika orodha hiyo licha ya kuitumikia nafasi hiyo kwa muda mfupi, huku kiongozi wa Nane Nane, Kanda ya Kaskazini, Arthur Shayo alisema licha ya mkuu huyo wa mkoa ‘kupambana’ na mbunge wa Arusha Mjini, Godbless Lema, bado ameweza kufanya mazuri.

“Kwa kweli ameweza kupambana na unyanyasaji wa wafanyabiashara wadogo kwa kiasi kikubwa na kuondoa usumbufu kwa wafanyabiashara kwa kupunguza mlundikano wa kodi,” alisema.

Mhadhiri mwingine wa Udsm, Dk Benson Bana alisema: “Licha ya kulalamikiwa katika baadhi ya mambo, lakini Makonda amefanya mengi mazuri. Hasa kuwafikia wananchi na kusikiliza kero zao.”
Alifafanua: “Amekuwa mbunifu zaidi, hasa ule mpango wake wa upandaji miti ambao unaweza kuifanya Dar es Salaam kuwa jiji zuri zaidi.”

Huku akieleza jinsi Makonda alivyowatuhumu makamanda wa polisi kwa rushwa amekuwa akishiriki katika ujenzi wa wodi za hospitali mbalimbali mkoani humo.

Meneja wa Chama Kikuu cha Ushirika (NCU) jijini Mwanza, Juma Mukilu alisema Mongela ni kiongozi aliyefanya mazuri mkoani humo licha ya juzi agizo lake kuwaondoa wamachinga kupingwa na Rais Magufuli.

“Anashirikiana na wananchi katika ujenzi wa barabara tena hata kwa kubeba mawe kwake ni sawa tu…, pia amekuwa bega kwa bega na wakulima kwa kupanga bei za mazao ambazo wafanyabiashara watazimudu,” alisema.
Share on Google Plus

About Unknown

    Blogger Comment
    Facebook Comment

0 comments:

Post a Comment

Laptop City

Tangazo