Msomi amkosoa Msajili wa Vyama


Suleiman Msuya

MHADHIRI Mwandamizi wa Chuo Kikuu cha Dar es Salaam (UDSM), Kitivo cha Sheria, Dk Onsmo Kyauke amekosoa kitendo cha Msajili wa Vyama vya Siasa, Jaji Francis Mutungi kuegemea upande katika mgogoro wa kisiasa ndani ya CUF, akidai ni udhalilishaji wa taaluma ya sheria nchini.

Dk Kyauke alisema hayo jana alipozungumza na JAMBO LEO Dar es Salaam, siku chache baada ya Ofisi ya Msajili kutoa barua kwa CUF kuruhusu kufungua akaunti kupitia kwa Mwenyekiti wake, Profesa Ibrahim Lipumba jambo alilosema ni kinyume na sheria na Katiba ya chama hicho.

Alisema kulingana na hali ya chama hicho, Msajili  alipaswa kuwa mtu wa kati, kwani kufanya hivyo ni kuongeza mpasuko na kudhalilisha taaluma ya sheria nchini.

“Nadhani Msajili anapaswa kujiuzulu kwani kimsingi ameonesha udhaifu, ushahidi upo kwenye mgogoro wa CUF kwa kuandika barua ya ufunguzi wa akaunti kinyume na taratibu,” alisema.

Alisema kwa mujibu wa Katiba ya CUF, chombo chenye mamlaka ya kufungua akaunti ni Bodi ya Wadhamini ambapo benki husika inapaswa kupokea cheti cha usajili na si barua ya Msajili kama ilivyofanyika katika mchakato wa kufungua akaunti kupitia Lipumba.

Alisema katika mchakato huo baada ya benki kupokea maombi inapaswa kupeleka taarifa kwa Wakala wa Usajili, Ufilisi na Udhamini (RITA) ambao ndio unatoa taarifa kwa benki husika kuhusu wadhamini na nia ya kufungua akaunti.

Dk Kyauke pia alisema inasikitisha kuona Lipumba anafanya mikutano ya hadhara mikoani huku kukiwa na katazo la Jeshi la Polisi bila kuchukuliwa hatua.
Share on Google Plus

About Unknown

    Blogger Comment
    Facebook Comment

0 comments:

Post a Comment

Laptop City

Tangazo