Hatima ya Mengi kujulikana leo


Grace Gurisha

MAHAKAMA Kuu Kitengo cha Biashara, leo inatarajia kutoa uamuzi kama itamwita Mwenyekiti wa Kampuni za IPP, Dk Reginald Mengi kwenda kuulizwa maswali kutokana na kiapo alichojieleza kwa nini asifungwe jela kwa kushindwa kutekeleza hukumu ya kulipa dola 598,750 za Marekani sawa na Sh bilioni 1.2 au la.

Malipo hayo ni ya wafanyabiashara watatu; Muganyizi Lutagwaba, Eric Mshauri na Charles Mgweo, kutokana na mgogoro unaohusu malipo ya uuzaji hisa kwenye kampuni ya Douglas Lake Minerals Ltd, ambayo kwa sasa inaitwa Handeni Gold Inc.

Mahakama hiyo ilifikia hatua hiyo jana, baada ya Wakili wa wafanyabiashara hao, Mafuru Mafuru kuomba Dk Mengi afike mahakamani ili aulizwe maswali yanayotokana na kiapo chake, lakini Wakili wa Mwenyekiti huyo, Deogratias Ringia alipinga mteja wake kuitwa mahakamani hapo.

Kutokana na mabishano hayo, Jaji Amir Mruma alisema uamuzi huo atautoa leo saa 3:30 asubuhi. Katika kiapo kinzani cha Mwenyekiti huyo kuna maombi aliyawasilisha mahakamani hapo akiomba kuongezwa muda wa kukata rufaa kupinga hukumu iliyotolewa.

Hata hivyo, Ringia aliwasilisha pingamizi la awali la kisheria dhidi ya hukumu iliyotolewa na Mahakama ikimwamuru Dk Mengi alipe fedha hizo kutokana na alichodai kuwa hukumu ilikuwa na kasoro za kisheria, kwa sababu haikusainiwa na pia hakuna maombi sahihi ya kisheria waliyoomba ya kutiwa hatiani.

Baada ya Ringia kuwasilisha pingamizi hilo, Jaji Mruma alisema litaamuriwa kwa maandishi, hapo hapo akatoa maelezo kuwa majumuisho ya kwa nini Dk Mengi asifungwe yataendeshwa kwa pamoja kwa njia ya maandishi.

Wakili Mafuru alipinga na kudai kuwa ni jambo ambalo haliwezekani, kwa sababu pingamizi linatakiwa kwanza litolewe ufumbuzi ndipo masuala mengine yaendelee,  kwa hiyo akataka mambo hayo mawili yatenganishwe, na hilo nalo Mahakama italitolea uamuzi.

Kesi hiyo inatarajiwa kusikilizwa na Jaji Amir Mruma, ambapo awali katika uamuzi wake, alikubali Dk Mengi atoe maelezo yake kwa kiapo huku akitoa siku saba kwa Mwenyekiti huyo kukamilisha hilo.

Awali, katika uamuzi wa Jaji Mruma alisema kama kiapo kinzani  kitaacha maswali mengi, basi nafasi ya Dk Mengi kuitwa mahakamani itakuwapo.

Hatua hiyo ya Mahakama inatokana na wafanyabiashara hao kuwasilisha maombi kuitaka Mahakama ikazie hukumu hiyo ya Januari 28.

Kesi hiyo iliyofunguliwa na wafanyabiashara hao ilisikilizwa na Jaji Agathon Nchimbi huku Dk Mengi na kampuni ya K.M. Prospecting Limited wakiwa walalamikiwa.

Hati ya kiapo cha pamoja cha wafanyabiashara hao, ilieleza  kuwa walifungua shauri kwenye Mahakama hiyo wakidai malipo, ambapo juhudi kama hizo zilifanyika  pia na Kampuni ya K.M. Prospecting zikashindikana kwa kuwa mali na akaunti zake za benki hazijulikani ziliko.
Share on Google Plus

About Unknown

    Blogger Comment
    Facebook Comment

0 comments:

Post a Comment

Laptop City

Tangazo