Lipumba amsubiri Seif kortini


Suleiman Msuya

MWENYEKITI wa Chama cha Wananchi (CUF), Profesa Ibrahim Lipumba na wafuasi wanaomuunga mkono, wanasubiri hatua ya Katibu Mkuu wa chama hicho, Maalim Seif Sharif Hamad na wafuasi wake kwenda mahakamani kuzuia utekelezaji wa maelekezo ya msajili wa vyama mahakamani.

Uamuzi huo umekuja wakati upande wa Maalim Seif ukieleza kuwa katika maandalizi ya mwisho ya kuwasilisha mahakamani maombi ya kutoa zuio la barua ya Msajili wa Vyama vya Siasa ambayo ilimtambua Profesa Ibrahim Lipumba kuwa mwenyekiti wa halali wa chama hicho.

Mkurugenzi wa Habari na Uenezi CUF, anayetajwa kuwa upande wa Lipumba, Abdul Kambaya alisema wanachosubiri ni maelekezo ya mahakama kama kweli Seif ataenda kortini.

“Sisi hatuna cha kufanya, tunasubiri Seif na wenzake waende mahakamani. Nadhani uamuzi wa mahakama ndiyo utatoa mwongozo wa sisi kuchukua hatua au kukaa kimya,” alisema Kambaya.

Awali, Mwenyekiti wa Kamati ya Uongozi ya CUF upande wa Maalim Seif, Julius Mtatiro aliliambia JAMBO LEO kwamba baada ya Mahakama Kuu kukubali na kuwaruhusu kuwasilisha ombi lao, mawakili wao wapo katika hatua za mwisho kuwasilisha shauri hilo mahakamani.

“Kwa sasa tupo katika maandalizi ya kuwasilisha Mahakamani kuhusu ombi letu la kutoa zuio la msajili kwani hakutendea haki chama,” alisema.

Aidha, alisema CUF wanapeleka ombi lingine mahakamani ambalo litatoa onyo kwa Msajili kuingilia uamuzi wa vyama vya siasa kwani anavunja sheria na Katiba.

Mtatiro alisema Msajili ameonesha dhahiri kwamba anatumikia kundi mojawapo katika mgogoro wa chama hicho, jambo alilosema halikubaliki katika mfumo wa vyama vingi.

Katika hatua nyingine, Kambaya alisema Lipumba anatarajiwa kuanza ziara nyingine mikoani mwishoni mwa mwezi huu hiyo ikiwa ni baada ya kurejesha kutoka mikoa ya Kanda ya Kusini.
Share on Google Plus

About Unknown

    Blogger Comment
    Facebook Comment

0 comments:

Post a Comment

Laptop City

Tangazo