Mbowe agonga mwamba kurudi Billicanas


Grace Gurisha

MAHAKAMA Kuu ya Tanzania, Kitengo cha Ardhi imetupilia mbali maombi ya Mwenyekiti wa Chadema, Freeman Mbowe ya kutaka kurudishwa kwenye jengo la Shirika la Nyumba la Taifa (NHC) 'Billicanas', kutokana na kudaiwa kodi ya Sh bilioni 1.3 na shirika hilo.

Uamuzi huo wa kutupwa kwa maombi ya Mbowe uliosomwa kwa saa moja ulitolewa jana na Jaji Sivangilwa Mwangesi, baada ya kupitia hoja mbalimbali na mawakili wa Mbunge huyo na wa NHC.

Jaji Mwangesi alisema baada ya kupitia hoja zao za awali alijiridhisha kwamba mchakato wa kumhamisha Mbowe kutoka jengo hilo ulifanyika kihalali.

Alisema mchakato huo ulioendeshwa na kampuni ya udalali ya Foster Auctioneers and General Traders, ulikuwa halali na ulifuata taratibu zote za kisheria.

“Kampuni hii ilifuata taratibu zote za kisheria tofauti na ilivyodaiwa na upande wa mlalamikaji, pia kuhusu suala la mkataba baina ya Mbowe na NHC, hilo si sehemu ya Mahakama.

“Kutokana na kujiridhisha huku, Mahakama inatupilia mbali maombi ya Mbowe ya kutaka kurudishwa kwenye jengo la Billicanas," alisema Jaji Mwangesi. 

Jaji huyo alisema alitupilia mbali maombi hayo bila gharama, kwa hiyo Mbowe hatatakiwa kulipa gharama za maombi hayo.

Mbowe kupitia kampuni yake ya Mbowe Hotels Limited, alifungua shauri namba 722 la mwaka 2016 dhidi ya NHC, akiiomba Mahakama itoe amri ya kurejeshwa katika jengo hilo, kwa madai kwamba kuondolewa kwake kulifanywa kinyume cha sheria.

Kupitia mawakili wake, alidai hakupewa ilani na NHC kumtaarifu kwamba anapaswa kuondoka kwenye jengo hilo na kwamba aliondolewa bila amri ya Mahakama.

Pia aliomba arudishiwe mali zake zilizochukuliwa na NHC kupitia kampuni ya udalali ya Foster, kwa maelezo kwamba zilichukuliwa kiholela huku wakidai kuwa kampuni hiyo ya udalali haikusajiliwa na Mahakama na pia aliiomba itolewe amri ya kuzuia asibughudhiwe baada ya kurudishwa.

Katika madai ya msingi ya Mbowe, Wakili Kibatala alidai kuwa mteja wake si mpangaji kwenye jengo hilo, bali ni mbia ambaye anamiliki asilimia 75 katika uendeshaji wake huku NHC wakimiliki asilimia 25.

Msingi wa pili, Kibatala aidai kuwa hata kama Mbowe angekuwa anadaiwa kodi na NHC, kuondolewa kwake kulifanywa bila kuzingatia sheria, kwa kuwa hakukuwa na amri ya Mahakama iliyowapa wadai nguvu ya kisheria ya kumwondoa.

Kwa upande mwingine, Mbowe kupitia hati ya kiapo, alidai kuwa hadaiwi hata senti tano na NHC kama pango la jengo la Billicanas na kwamba amekuwa akilipa tozo zote zinazotakiwa kwa mujibu wa mkataba baina yake na shirika hilo.

Nje ya Mahakama
Baada ya uamuzi huo, hali ilikuwa tete kwa mawakili wa Mbowe, Peter Kibatala, John Mallya na Omary Msema kwa kuona kuwa Mahakama hiyo haikutenda haki kwa mteja wao kwa hiyo watakata rufaa.

Wakili Mallya alisema walipokea uamuzi na waliiomba Mahakama iwape nakala ya uamuzi na kwamba jambo hilo halitaishia hapo litakwenda mahakama za juu.

“Tutakata rufaa na tutakwenda mahakama za juu, hivyo tutaupitia vizuri uamuzi huu kisha tuchukue hatua, hivyo mkataba wa Mbowe na NHC haukupata kutekelezwa na haupo,” alisema Mallya.

Kibatala alisema wamepeleka maombi ya nakala ya uamuzi huo ili waende kwenye marejeo katika Mahakama ya Rufaa na pia wamepeleka maombi ya kuzuia chochote kufanyika katika eneo husika.

Akizungumzia mali za Mbowe, alisema hadi watakapopata uamuzi wa Mahakama ya Rufaa, baada ya kupitia uamuzi wa Mahakama Kuu ya Tanzania, Kitengo cha Ardhi.

NHC

Akizungumza nje ya Mahakama, Wakili wa NHC, Aliko Mwamanenge alisema wanaishukuru Mahakama kwa kutenda haki kutokana na uamuzi huo.

Alisema kutokana na uamuzi huo Mahakama ilikubali kwamba kila kitu kilichofanyika siku ya kutolewa kwa mali za Mbowe kilifanyika kihalali, hivyo mali zake haziwezi kurudishwa.

"Mali zake haziwezi kurudishwa kwa sababu bado hajalipa deni analodaiwa na shirika, kwa hiyo atapewa mali zake atakapolipa deni hili,” alisema Mwamanenge.
Share on Google Plus

About Unknown

    Blogger Comment
    Facebook Comment

0 comments:

Post a Comment

Laptop City

Tangazo