Wadau wa habari waomba kujadili Muswada


Joyce Kasiki, Dodoma

Deo Nsokolo
WADAU wa habari nchini, wameiomba Kamati ya Kudumu ya Bunge ya Huduma za Maendeleo ya Jamii kuwaongeza muda hadi Februari mwakani.

Lengo ni ili wajadili kwa kina Muswada wa Huduma za Habari wa Mwaka 2016 kwa manufaa ya waandishi wa habari na Taifa kwa jumla.

Wakizungumza na waandishi wa habari baada ya kukutana na kamati hiyo na kutoa hoja hiyo jana, wadau hao walisema muda waliopewa kuujadili ni mfupi, hivyo kuhitaji muda wa nyongeza ili kuwafikia wadau wengi hasa wanahabari ambao ndio walengwa wa sheria tarajiwa.

Rais wa Muungano wa Klabu za Waandishi wa Habari Tanzania (UTPC), Deogratius Nsokolo alisema wadau wa sekta ya habari ni wengi hivyo si rahisi kuwafikia wote kwa muda uliowekwa na kujadiliwa kwenye Bunge lijalo.

"Muswada huu una wadau wengi, lakini wadau wakubwa ni wanahabari wenyewe ambao wanahitaji muda wa kutosha kuujadili na kutoa maoni yao, bila hivyo utawaathiri wao na jamii kwa jumla.

“Tunamwomba Waziri husika aliangalie wazo hilo, lakini kimsingi hatupingi kutungwa sheria hiyo kwani ina manufaa kwa wanahabari pamoja na kulinda taaluma ya habari nchini," alisema Nsokolo.
Rais wa Chama cha Wanasheria Tanzania (TLS), John Seke alisema chama hicho kimeona bado wadau wa habari  wanahitaji nafasi ya kujadili Muswada huo ili upate maoni ya kutosha.

Meneja Programu kutoka Baraza la Habari Tanzania (MCT), Pili Mtambalike alisema licha ya kuwa sheria hiyo iliombwa na wadau hao kutokana na sheria zilizopo kuwa kandamizi, wanahitaji muda zaidi wa kuujadili.

"Kwa muda mrefu tasnia ya habari tumekuwa kwenye mchakato, sheria hii tuliiomba, tulisema zilizopo ni kandamizi kwa hiyo tukasema tushirikiane  na Serikali tuwe na sheria zitakazosaidia kukuza tasnia ya habari, uhuru na uwezo wa  vyombo vya habari kuchangia mchakato wa kukuza demokrasia nchini,

"Na bahati nzuri tangu mwaka 2006 wadau tulitoa maoni na mwaka 2011 tukaboresha maoni na leo tumepata Muswada, una mambo mengi ambayo yataathiri waandishi wa habari, wanamiliki wa vyombo vya habari na wanaotusaidia kwenye kazi zetu za habari, tunapenda kupata muda ili tufikie maelewano na kupata hiyo sheria," alisema Mtambalike.

Katibu wa Chama cha Wamiliki wa Vyombo vya Habari, Henry Mahanika alisema kuomba muda wa nyongeza si kuuchelewesha wala kuupinga.

"Si mbinu ya kuchelewesha au kupinga sheria hii isiwepo na ndiyo sababu tukaomba tupate muda kidogo tu kwa sheria hii ambayo imeanza mchakato kwa takribani miaka 10.
“Miezi minne tuliyoomba si muda mrefu na hiyo ni kutaka kujiridhisha ili wadau wapitie na kuona kama kuna vipengele ambavyo haviendani na sera wala Katiba na waweze kutoa maoni yao," alisema Mahanika.

Makamu Mwenyekiti wa Jukwaa la Wahariri Tanzania (TEF), Deodatus Balile alisema wadau walianza kukutana Septemba hadi Oktoba na wanaona kila sababu ya kukusanya maoni ya wadau hususan wanahabari wa mikoa yote nchini.

Alisema lengo la ushirikishwaji huo na kuomba muda huo hadi Februari ni kutengeneza sheria ambayo haitapitwa na wakati, haitaonea mtu na wakati mwingine kuipeleka tasnia  mbele zaidi kadri teknolojia inavyokua.

Mwenyekiti wa Kamati hiyo, Peter Serukamba aliendelea na kikao na kusoma maudhui ya sheria hiyo pamoja na mchakato wake katika hatua zote na baada ya kumaliza kusoma akataka wadau waanze kutoa maoni yao.




Share on Google Plus

About Unknown

    Blogger Comment
    Facebook Comment

0 comments:

Post a Comment

Laptop City

Tangazo