Vyeti vya bandia kuumbua wabunge


* Wengi wadai kuwa na Shahada, bila kutaja fani
* Baadhi nao wabania viwango vyao vya kitaaluma

Mwandishi Wetu

UHAKIKI wa vyeti kwa watumishi wa umma, huenda ukaibua ‘madudu’ kuhusu aina ya viongozi waliochaguliwa na wananchi, ukifika kwa wabunge, baada ya watafiti wa wasifu wa wabunge hao, kubaini kuwa wengi hawapendi kueleza taaluma walizosomea.

Mbali na idadi kubwa ya wabunge hao kukataa kutaja taaluma na fani walizosomea zaidi ya kudai kuwa wana Shahada ya chuo kikuu, utafiti huo umebaini pia baadhi yao kukosa wasifu kabisa wa kitaaluma zaidi ya jina, chama na aina ya ubunge.

Utafiti uliopewa jina la ‘Watawala Wetu’, uliofanyika mwaka huu wakati Serikali ikifanya uhakiki wa vyeti vya watumishi wa umma, umebaini taswira hiyo ya kukataa kutaja taaluma kwa wabunge 66, wakati watafiti hao wakitafuta taarifa za mambo matatu; ikiwamo kama wabunge wanaakisi taswira ya jamii ya Watanzania.

Mambo mengine ambayo watafiti hao kutoka Taasisi ya Sayansi ya Jamii; Bituro Kazeri na Emmanuel Ndomondo walilenga kupata taarifa zake; ni kama wabunge hao wanakidhi matarajio ya Watanzania katika zama hizi na mwisho ni kama wana uwezo wa kutekeleza majukumu yao kwa mujibu wa Katiba ya Jamhuri ya Muungano wa Tanzania.

Madudu yaliyoibuka

“Ukusanyaji wa taarifa ulikutana na changamoto ya kukosekana taarifa za kutosha. Kwa mfano wabunge wengi walionesha kuwa wana elimu ya kiwango cha Shahada bila kutaja ni shahada ya taaluma ipi. Hii ilileta changamoto ya kupanga ni ujuzi au stadi zipi walizonazo.

“Changamoto nyingine ni kutokuwepo kwa taarifa kabisa kwenye wasifu wa wabunge zaidi ya jina, chama na aina ya ubunge,” imeelezwa katika utafiti huo ambao pia umeonesha namna Bunge la 11 la Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, linavyokabiliwa na nakisi ya wanataaluma mbalimbali.

Watafiti hao wameeleza kwamba, hapana shaka katika mabadiliko hayo jamii imepanua vigezo vya wasifu wa wenzao wanaowachagua kuwa wabunge.

“Kwa mfano inawezekana kwa zama zilizopo kusoma na kuandika katika Kiswahili na Kiingereza si sifa inayotosha kumpa mtu ubunge pale anapokuwa anashindana na mwingine mwenye sifa zaidi ya hizo,” walieleza wakijaribu kuoanisha sifa ambazo jamii itahitaji kutumia kama kigezo na zilizopo katika Katiba.

Wenye shahada/diploma

Kati ya wabunge 389 waliofanyiwa utafiti kuhusu wasifu wao, taarifa zinaonesha kuwa 105 wamedai kuwa na Shahada ya kwanza ya chuo kikuu.

Kati yao, CCM ina wabunge 61 waliodai kuwa na Shahada kati ya wabunge wake 275;  Chadema wabunge 32 kati ya wabunge wake 69 na CUF ina 11 tu waliodai kuwa na elimu hiyo kati ya wabunge wake 42.

Wenye diploma ilidaiwa ni wabunge 51 na kati yao 34 ni wa CCM; tisa Chadema na CUF wanane.

Uzamili/uzamivu

Wabunge 136 kati ya 389 walidai kuwa na elimu ya Shahada ya Uzamili au Uzamivu ambapo kati yao, CCM ina 110; Chadema 17; CUF saba; NCCR-Mageuzi na ACT-Wazalendo kila kimoja mbunge mmoja.

Msingi, sekondari, siri

Aidha, wabunge 18 walikiri kuwa wao elimu yao ni ya msingi na kati yao CCM ni 16, Chadema mmoja na CUF mmoja.

Waliodai kuwa na elimu ya sekondari ni wabunge 73, kati yao 49 wanatoka CCM; Chadema ni 10 na CUF wako 14.

Wabunge sita; watano kutoka CCM na mmoja CUF hawakutaka kabisa kutaja elimu yao wakisema ni siri yao.

Nakisi ya taaluma

Kati ya wabunge 66 waliokataa kueleza taaluma au uzoefu wao, utafiti huo umeonesha kuwa 33 ni waliosema awali kuwa na Shahada ya Kwanza. Wako pia wabunge wanane waliodai kuwa na Shahada ya Uzamili au Uzamivu, na walipotakiwa kuanisha taaluma walikataa.

Mbali na waliokataa kusema taaluma japokuwa wanadai kuwa na Shahada ya Kwanza, Uzamili na Uzamivu, utafiti huo pia ulibaini Bunge kukabiliwa na nakisi ya wanataaluma wengi.

Taaluma zilizosomewa na mbunge mmoja mmoja ndani ya Bunge zima ni Jiolojia, urubani, usanifu majengo, uanadiplomasia, usanifu, mipango wa uchumi, polisi, usafirishaji, utafiti na utalii.

Fani 10 zenye wabunge wengi ni ualimu (48); uhasibu na fedha (35); ujasiriamali (33); sheria (26); utawala na biashara (17); uhandisi (14); utawala (13); uhadhiri (12); habari na mawasiliano (11) na siasa na uchumi kila moja wabunge tisa.

Share on Google Plus

About Unknown

    Blogger Comment
    Facebook Comment

0 comments:

Post a Comment

Laptop City

Tangazo