JK ana kwa ana na Lowassa msibani


Sharifa Marira na Hussein Ndubikile

MILIMA haikutani binadamu hukutana. Ndivyo unavyoweza kusema baada ya Rais mstaafu Jakaya Kikwete na Waziri Mkuu wa zamani, Edward Lowassa kukutana jana na kupeana mikono katika tukio lililoonekana kukumbusha mengi kuhusu ‘maswahiba’ hao wa siku nyingi.

Walikutana baada ya miezi 15 tangu Lowassa alipohamia Chadema baada ya kukatwa CCM katika kinyang’anyiro cha urais na CCM kumpa Rais John Magufuli dhamana ya kupeperusha bendera yake kwenye mbio za urais.  

Lowassa ambaye alijitosa katika mbio hizo, jina lake lilikatwa na Kamati Kuu ya CCM chini ya uenyekiti wa Kikwete wakati wa mchakato wa kura ya maoni kumpata mgombea urais.

Baada ya kutua Chadema na kuuponda mchakato wa CCM kupata mgombea wake wa urais, Lowassa alipitishwa kwa tiketi ya Chadema na kuungwa mkono na  Ukawa na kwa mara ya kwanza alizungumzia sakata la zabuni ya kufua umeme ya Richmond, kubainisha kuwa  ilitekelezwa kwa agizo kutoka ngazi za juu.

Lowassa alikuwa Waziri Mkuu kuanzia mwaka 2005 hadi 2008 alipojiuzulu kutokana na sakata hilo la Richmond.

Wawili hao ambao kwa nyakati tofauti wamekuwa wakirushiana vijembe, walikutana jana katika viwanja vya Karimjee wakati wa kuaga mwili wa aliyekuwa Meya wa Jiji la Dar es Salaam, Didas Masaburi.

Tukio hilo lilitokea siku 57 tangu waliposhiriki Misa ya shukrani ya maadhimisho ya miaka 50 ya ndoa ya Rais wa Serikali ya Awamu ya Tatu, Benjamin Mkapa,  lakini hakukuwa na tukio bayana la kukutana na kupeana mikono kama ilivyotokea jana.

Kikwete ndiye alikuwa wa kwanza kufika kwenye viwanja hivyo saa 3 asubuhi akifuatana na mkewe Mama Salma, na kukaa viti vya mbele kwenye eneo maalumu lililotengwa kwa ajili ya viongozi.

Wakati Lowassa akiingia kwenye viwanja hivyo sambamba na mkewe Regina,  alisalimu  viongozi mbalimbali huku Kikwete akionekana kuwa makini kumtazama.

Kadri alivyokuwa akisalimia mmoja baada ya mwingine ndivyo alivyokuwa akikaribia alipoketi Kikwete alisimama na kumpa mkono.  

Tukio hilo lilivuta hisia za mamia ya watu waliojitokeza katika viwanja hivyo pamoja na waandishi wa habari ambao walipigana vikumbo kupata picha ya wanasiasa hao.

Lowassa ambaye sasa ni mjumbe wa Kamati Kuu ya Chadema alipoulizwa na JAMBO LEO nini kauli yake baada ya kupeana mkono na Kikwete alihoji: “Sasa niseme nini?”

Kuzorota kwa uhusiano wa wanasiasa hao wanaoelezwa kuwa marafiki wa miaka mingi waliopanga mengi pamoja ikiwa ni pamoja na kuwania urais mwaka 1995, kulitajwa kuibuka kabla ya Uchaguzi Mkuu mwaka jana.

Licha ya wao au wapambe wao kuzikanusha taarifa hizo, huku wakati fulani Lowassa akibainisha kuwa hakukutana na Kikwete barabarani, hali ilikuwa tofauti katika kipindi cha kuelekea uchaguzi huo hasa baada ya jina la Lowassa kukatwa.

Kitendo cha Waziri Mkuu huyo wa zamani kujiunga upinzani kilifungua ukurasa mpya wa kurushiana maneno, yakianzia kwa Mwanasheria Mkuu wa Chadema, Tundu Lissu ambaye kwa nyakati tofauti alinukuliwa na vyombo vya habari akimtaka Kikwete aseme Richmond ni ya nani.

Kauli hiyo ilijibiwa na Kikwete katika kampeni za uchaguzi huo, akimtaka Lissu kumtaja mwenye Richmond kwa madai kwamba anatembea naye kwenye kampeni kila siku. Hatua hiyo ilisababisha mwanasiasa huyo naye kumjibu Kikwete kuwa Richmond ilikuwa yake.

Katika mkutano wa mwisho wa kufunga kampeni, Kikwete alisema Richmond ilikuwa ya Lowassa na yeye kwa kuwa alikuwa Mkuu wa Nchi aliruhusu mitambo hiyo kuagizwa lakini akataka sheria ya ununuzi ifuatwe, jambo ambalo Lowassa na kamati ya makatibu wakuu iliyoteuliwa na Waziri Mkuu, hawakulizingatia.

Hali hiyo ilionekana kuwa mwanzo wa mwisho wa urafiki wao wa miaka mingi walioanza pamoja mbio za kuingia Ikulu mwaka 1995 na pia walipoanza utumishi wa TANU na baadaye CCM, baada ya kuhitimu shahada zao Chuo Kikuu Dar es Salaam (UDSM) miaka ya 1970.
Share on Google Plus

About Unknown

    Blogger Comment
    Facebook Comment

0 comments:

Post a Comment

Laptop City

Tangazo