Elimu ya Juu wasotea mikopo


Hussein Ndubikile

NI balaa. Ndivyo unavyoweza kusema baada ya maelfu ya wanafunzi wa vyuo vikuu nchini kushindwa kujisajili kutokana na Bodi ya Mikopo ya Elimu ya Juu (HESLB) kuchelewesha mikopo hadi jana, siku tatu tangu vyuo hivyo vifunguliwe.

Uchunguzi uliofanywa na gazeti hili katika vyuo kadhaa Dar es Salaam, umebaini kuwa baadhi ya wanafunzi hao wanaranda mitaani wakisubiri mkopo huo ambao kuchelewa kwake kumefanya hata vyuo vishindwe kuwahudumia.

JAMBO LEO ilishuhudia wanafunzi hao katika Chuo Kikuu cha Dar es Salaam (UDSM), Tumaini, DUCE, Ardhi na Muhimbili wakisotea usajili chuoni hapo, huku wengi wakieleza kukwama kwa siku ya nne jana.

UDSM na Tumaini vilifunguliwa Oktoba 10, lakini baadhi ya wanafunzi wanaotoka mikoani walilazimika kufika Dar es Salaam tangu Oktoba 8 kuwahi usajili.

Hata hivyo, walipofika chuoni, wengi walishindwa kujisajili baada ya kuelezwa kuwa Bodi ya Mikopo haijawaingizia fedha, hivyo kulazimika kuzunguka mitaani wakisubiri fedha hiyo.

Mwanafunzi wa Shahada ya Kwanza ya Elimu kutoka Iringa, Primus Kola alisema  aliwasili Dar es Salaam Oktoba 8 kuwahi usajili UDSM. Alisema tangu afike hajaambiwa ni lini majina ya kugawiwa mikopo yanafika.

Mwanafunzi huyo aliyeeleza kuwa yuko katika hali ngumu kifedha, alisema: "Nilifika tangu Oktoba 8 hadi sasa sijajua hatima yangu ya mikopo na hapa sina ndugu wa kwenda kuishi kwao."

Mwanafunzi mwingine wa Shahada ya Sheria, Said Ally alisema haelewi kwa nini Bodi haijaleta majina ya wanafunzi wanaotakiwa kupewa mikopo na hana fedha za kumwezesha kufanya usaili.

"Huwezi kupata sehemu ya kulala bila kulipia fedha hata usajili wa kozi yako inakuwa vigumu," alisema.

Mwanafunzi mwingine wa mwaka wa kwanza Shahada hiyo kutoka Mwanza, Halima Sudi alisema bado hajajua siku ambayo majina yatawasilishwa chuoni na hilo linaendelea kumpa wakati mgumu.

Waziri wa Mikopo wa Serikali ya Wanafunzi wa UDSM (DARUSO), Eliud Kasunzu alisema aliambiwa kilichochelewesha majina hayo ni kutokana na Tume ya Vyuo Vikuu (TCU) kuchelewesha mchakato wa ushughulikiaji wanafunzi wanaotakiwa kujiunga na vyuo.

Alisema baada ya kufuatilia Bodi ya Mikopo waliambiwa ndani ya wiki hii au wiki ijayo majina hayo yatawasilishwa chuoni hapo. Alifafanua kuwa endapo Bodi hiyo haitapeleka majina hayo watakwenda wizarani kujua hatima ya wanafunzi hao.

Mkurugenzi Msaidizi wa Habari Elimu na Mawasiliano wa Bodi ya Mikopo, Cosmas Mwaisobwa alisema anafahamu vyuo vimeanza udahili bila orodha ya majina ya wanaostahili kupata mikopo.

"Ninachoweza kusema ni kwamba tunafahamu tatizo hilo na Bodi inaendelea na mchakato wa kukamilisha majina na kuyawasilisha vyuoni," alisema.

Alipoulizwa anadhani lini majina hayo yatakuwa tayari, alijibu: “Siwezi kusema lini kazi hii itakwisha ila muhimu ni kujua kuwa tatizo linajulikana na Bodi iko katika hatua za mwisho kukamilisha orodha ya majina."
Share on Google Plus

About Unknown

    Blogger Comment
    Facebook Comment

0 comments:

Post a Comment

Laptop City

Tangazo