Kampeni chafu zatikisa CCM

* Matajiri wamwaga fedha kuwania uongozi
·         * Mangula aonya wamebainika, watakiona

Sharifa Marira na Leonce Zimbandu

MAKAMU Mwenyekiti wa CCM, Philipo Mangula, ameanza kupokea majalada ya wanaCCM walioanza kujipitisha kutoa rushwa kwa ajili ya uchaguzi wa ndani wa chama hicho, unaotarajiwa kufanyika mwakani.

Amesema ana taarifa kwamba baadhi ya wana CCM wameanza kutumia mbinu chafu za fedha kutaka nafasi mbalimbali, lakini ‘imekula kwao’ kwa kuwa hawatapenya kwani atawashughulikia.

Mangula alitoa kauli hiyo jana Dar es Salaam, wakati akitoa mada ya maadili ya viongozi kwenye kongamano la maadhimisho ya kumbukizi ya Mwalimu Julius Nyerere na kueleza kukerwa na tabia ya wafanyabishara wenye fedha kutaka kuteka kila mahali.

Alisema ndani ya CCM yeye ni maarufu kwa jina la ‘Mzee wa Mafaili’, hivyo ataendelea kupitia majalada hayo ili kuhakikisha maadili yanazingatiwa na kuenzi misingi ya Azimio la Arusha, kwani hakuna atakayepenya kwa rushwa.

“Zipo taarifa kuwa wapo baadhi wameanza kujipitisha na kutoa rushwa kwa ajili ya uchaguzi wa mwakani, nawahakikishia kwangu watu hao hawawezi kupita, nitamfuatilia kila mmoja atakayejihusisha na rushwa ili asipate nafasi hiyo,” alisema.

Kutenganisha
Alisema ili kudhibiti mianya hiyo, atahakikisha sheria inatungwa ya kutenganisha kati ya wafanyabiashara na uongozi, kwa vile wafanyabiashara wanatafuta nafasi ya uongozi, ili kuendeleza biashara zao.

Mangula alisema ni aibu kwa mpigakura kuhongwa kiasi kidogo cha fedha na kupoteza haki ya msingi ya kuchagua kiongozi mwenye sifa kwa ajili ya maendeleo. Alisema iwapo tabia ya kununua uongozi itaendelea, baadaye vijana wanaohitimu masomo watakosa nafasi za kugombea kutokana na kukosa fedha za kuhonga.

Watanzania wanapaswa kufahamu hatua zinazochukuliwa na Rais John Magufuli, kuwatumbua watumishi wazembe, imetokana na kauli ya vikao halali vya CCM ili atekeleze hayo.

“Huo ni mpango mkakati wa chama, kwa lengo la kuondokana na rushwa, vinginevyo misingi na maadili ya uongozi vitapotea,” alisema.

Spika mstaafu na Mwenyekiti wa Kongamano hilo, Anne Makinda aliwataka vongozi wa vyama vya siasa kupeleka vijana wao kwenye Chuo cha Kumbukumbu ya Mwalimu Julius Nyerere (MNMA) kujifunza maadili ya uongozi ili kuepuka rushwa.

Alisema kongamano hilo lilizingatia mada kuu tatu; Azimio la Arusha, Miiko ya Uongozi na Maadili ya Viongozi, ambayo yanapaswa kutumiwa na kila kiongozi kujitathmini.

Mmoja wa watoa mada, Katibu Mkuu wa CCM mstaafu, Wilson Mukama alisema viongozi wengi wa siasa wapo kwa ajili ya maslahi binafsi ya kupata utajiri, zikiwamo nyumba, magari na fedha. Alisema hali hiyo inawafanya watumie gharama yoyote kupata nafasi ya uongozi huku akijua fedha hizo zitarudi na kutengeneza maisha mapya.

“Wapo viongozi kwa ajili ya maslahi yao na si maslahi ya jamii, huko ni kutoka nje ya maadili,” alisema.

“Viongozi wengi wanashughulika na matatizo yao binafsi ndio maana hata wabunge walilalamika walipopewa Sh milioni 95 za kununulia magari walipoingia madarakani wakadai ni ndogo, ushabiki wao ni magari, nyumba na fedha lakini si waliowachagua,’’ alisema Mukama.

Butiku
Mwenyekiti wa Taasisi ya Mwalimu Nyerere, Joseph Butiku alisema kiongozi wa nchi hapaswi kuongoza kama tembo badala yake anapaswa kuheshimu wananchi akitambua kuwa binadamu wote ni sawa jambo ambalo Mwalimu Nyerere alilisisitiza.

‘’Ukitaka kuwa kiongozi wa nchi hii unapaswa utambue na uwe na imani kwamba watu wote ni sawa, usiwe Rais tembo unapaswa kujua kuwa watu unaoongoza unatokana nao na uwaongoze kwa heshima,’’ alisema na kuongeza:

’’Ukitaka kuwa Spika unapaswa ujue unaongoza wabunge wanaotuwakilisha sisi, hivyo uongoze ukijua kwamba wabunge wanawakilisha watu wengi, chagua unataka kuwa kiongozi wa watu unaotumwa na watu au unataka kuwa kiongozi wa kutafuta utajiri na kuongoza matajiri,’’ alisema.

Alisema wanasiasa wengi hawasikilizi wanaowachagua, ndiyo maana wanakuwa maadui wa wananchi kutokana na kwenda kinyume na matakwa yao.

“Viongozi wengi nchi hii ni wababaishaji, mnakuwa maadui wa wananchi kutokana na kwenda kinyume na wanavyotaka, mko nje ya mstari wao, acheni kubabaisha, Nyerere alikuwa binadamuna aliamini kwa binadamu, Imani yake ilikuwa kwa watu wote na ndicho kiini cha mambo yote, Imani katika watu, watu wote ni watu hakuna mtu mbuzi, kuku wala paka,’’ alisema Butiku.

Butiku alisema hata mwaka 1985 wakati Mwalimu Nyerere anaaga bungeni, alisema kazi muhimu kuliko zote kwake na kwa wananchi wote ni kujenga Taifa lenye umoja kwa msingi wa heshima na usawa kwa binadamu.

Kondo
Kanali mstaafu,Dk Harun Kondo alisema Azimio la Arusha ndilo linalotambulisha Taifa hivyo ni vigumu kuliua na atakayejaribu atakufa yeye, kutokana na kuwa na misingi ya kisayansi, likizungumzia matatizo halisi ya wananchi.

“Suala la rushwa nchini limekuwa kama dini, imani za watu ni rushwa pekee, tumekuwa kama kiwiliwili kinachotembea, tumeondoka katika misingi ya Azimio na siasa za Ujamaa na Kujitegemea tumekwenda kupotelea tunakokujua wenyewe,’’ alisema Dk Kondo.
Share on Google Plus

About Unknown

    Blogger Comment
    Facebook Comment

0 comments:

Post a Comment

Laptop City

Tangazo