Tuyaenzi ya Nyerere na ‘kuyaishi’ tunayoyaenzi



Mashaka Mugeta

Mashaka Mgeta
UMOJA wa Afrika (AU) umeungana na Watanzania katika nadharia na vitendo vinavyoelekezwa katika kumkumbuka na kumuenzi Baba wa Taifa, hayati Mwalimu Julius Nyerere aliyefariki dunia Oktoba 14, 1999 katika Hospitali ya Mtakatifu Thomas jijini London, Uingereza.

Ingawa AU imekuwa ikijikita katika fikra za waasisi wake na waliopigania uhuru katika mataifa ya Afrika akiwamo Mwalimu Nyerere, lakini taasisi hiyo iliyoasisiwa kutoka Umoja wa Nchi Huru za Kiafrika (OAU) imekwenda mbele zaidi.

Imezindua Kituo cha Amani na Usalama cha Makao Makuu yake (AU) kilichoitwa Mwalimu Julius Nyerere, kikiwa jijini Addis Ababa, Ethiopia.

Kupewa jina la Mwalimu Nyerere kwa kituo hicho si jambo jipya, kwa maana yapo majengo, barabara, vyuo, vituo vya maendeleo ya jamii na vinginevyo katika kona tofauti za dunia hususani barani Afrika, vilivyopewa jina la Mwalimu Nyerere.

Hivyo hata AU wanapoamua kulitumia jina hilo kwa Kituo cha Amana na Usalama cha Makao Makuu yake, ni mwendelezo wa hulka na kusudio jema la kumuweka Mwalimu Nyerere.

Kwamba Mwalimu Nyerere anasimama katika watu wanaopaswa kuiendeleza misingi aliyoisimamia, ndoto za maendeleo, umiliki wa rasilimali, ujenzi wa umoja na uwapo wa Amani kwa nchi yake, bara lake na wananchi kwa ujumla.

Kutumika kwa jina la Mwalimu Nyerere ni ishara ya kukumbuka namna Kiongozi huyo alivyosimamia haki, usawa, kukemea uovu na kuguswa umasikini wa watu.

Mwalimu Nyerere anapokumbukwa hata na AU, inakuwa rejea ya kuufikirisha ulimwengu namna ambavyo aliweka kando matendo na fikra zenye kukidhi manufaa binafsi, familia ama marafiki, bali kuifanya jamii pana ya raia walio wengi wake wenye furaha.

Kwa maana hiyo, kupitia maisha bora. Mwalimu Nyerere aliyethamini utu wa mtu, akashiriki kubuni, kutunga na kuzisimamia ahadi 10 za waliokuwa wanachama wa chama Tanganyika African Nation Union (Tanu) ambacho Februari 5, 1977 kiliungana na chama cha Afro Shiraz cha Zanzibar, kikaanzishwa Chama Cha Mapinduzi (CCM).

Ahadi hizo zenye sifa na viashiria vya tunu za uongozi bora ni binadamu wote ni ndugu zangu na Afrika ni moja, nitaitumikia nchi yangu na watu wake wote na nitajitolea nafsi yangu kuondoa umaskini, ujinga, magonjwa na dhuluma.

Nyingine ni rushwa ni adui wa haki sitapokea wala kutoa rushwa, cheo ni dhamana. Sitakitumia cheo change wala cha mtu mwingine kwa faida yangu, nitajielimisha kwa kadiri ya uwezo wangu na kutumia elimu yangu kwa faida ya wote.

Pia zikawapo, nitashirikiana na wenzangu wote kuijenga nchi yetu, nitasema kweli daima, fitina kwangu mwiko, nitakuwa mwanachama mwaminifu wa TANU na raia mwema wa Tanganyika na Afrika na ya mwisho ikaandikwa, nitakuwa mtiifu na mwaminifu kwa Rais wa Serikali ya Tanganyika.

Kwa ufupi, jina la Mwalimu Nyerere linapotajwa na kumbukumbu ya maisha yake kurejea akilini mwa watu, msingi wake unachagizwa na ahadi hizo.

Hivi sasa Mwalimu Nyerere hayupo tena duniani katika umbile lake, isipokuwa fikra zake zipo na zitadumu. Atazidi kuwa rejea ya namna uongozi wa mataifa hasa ya Afrika unavyopaswa kuwa, hata kama waliopo madarakani kwa kila nchi, hawawezi kutekeleza, kufuata na kujifunza kutoka kwake.

AU inapofikia hatua ya kumkumbuka Mwalimu Nyerere kwa kulitumia jina lake, lakini ikukumbukwa kwamba Umoja huo ulishakubali na kuitumia lugha ya Kiswahili iliyotumiwa na mwanasiasa huyo wa karne kuiunganisha Tanzania na Watanzania, raia wa taifa hili wakiwamo viongozi wanasimama wapi?

Bila shaka lipo jukumu moja kubwa kwa Tanzania. Jukumu linapopaswa kuingizwa kwenye mifumo ya kisheria inayotoa adhabu kwa watakaoikiuka, kwamba misingi iliyoasisiwa na Mwalimu Nyerere inapaswa kuenziwa ili watu waiishi misingi hiyo.

Misingi iliyo sehemu kubwa ya tunu za Taifa (kama ilivyowahi kutajwa kwenye rasimu ya Katiba Mpya iliyowasilishwa na Tume ya Jaji Warioba) inapaswa kuendelezwa baada ya kuenziwa. Hivyo kuienzi kusiwe kunakotokana na kauli za kisiasa pasipo utashi na uthubutu unaodhihirika machoni pa watu.

Tanzania na raia wake wakiwamo waliokabidhiwa na watakaokabidhiwa dhamana za uongozi, wanapaswa kujiepusha na kuwa mfano wa eneo la jiografia lenye misitu likakosa wajenzi. Kwamba pamoja na kujaliwa ‘kisima cha hekima’ za Mwalimu Nyerere, watu waishi ndivyo sivyo!

Mwalimu Nyerere alifundisha kila eneo la kijamii kuanzia uhusiano wa mtu na mtu, kikundi ama taasisi moja na nyingine, kisha kwa raia wote. Uhusiano unaojikita katika kuheshimiana, kuvumiliana na kupingana pasipo kupigana.

Mwalimu Nyerere alielekeza na kufundisha namna bora ya kuiendeleza misingi ya haki za binadamu na usawa kwa watu wote. Alipinga unyanyasaji, uonevu na ubaguzi wa kila aina. Kisha akasimamia umoja wa kitaifa unaochagiza kasi ya maendeleo na ustawi wa watu.

Lakini orodha ya mafundisho na maelekezo ya Mwalimu Nyerere hayaishi hapo, kwa maana hata yakiandikwa yote si eneo la safu hii ama gazeti zima litatosha. La hasha, isipokuwa kwa machache yanayotokana na AU ilivyomuenzi Mwalimu Nyerere.

0754691540

***************************************

Share on Google Plus

About Unknown

    Blogger Comment
    Facebook Comment

0 comments:

Post a Comment

Laptop City

Tangazo