Serikali kutathmini hali ya chakula


*Yasisitiza hakuna njaa, yakoromea wafanyabiashara
*Yakiri kukabiliwa ukame, yaonya wanaoficha chakula  

Sharifa Marira

Dk. Charles Tizeba
WAKATI Serikali ikisema nchi haina njaa, imeazimia kufanya tathmini ikihusisha halmashauri 55 zenye uhaba wa chakula na kubaini kaya zenye tatizo hilo.

Hayo yamesemwa na Waziri wa Kilimo, Mifugo na Uvuvi, Dk Charles Tizeba, akiwa Dar es Salaam huku Waziri MKuu akiwa Dodoma naye akiwataka wananchi kupuuza upotoshaji unaofanywa na wafanyabiashara kuhusu hali ya chakula nchini.

Akizungumza na waandishi wa habari, Dk Tizeba alisisitiza kuwa nchi haina njaa bali  ukame katika baadhi ya maeneo na kuwataka wafanyabiashara walioficha chakula wakitoe mara moja kabla Serikali haijatumia njia zake kukitoa.

Dk Tizeba alisema baadhi ya watu wanatumia ukame kupelekea ujumbe kwa jamii kuwa nchi inakabiliwa na njaa, huku akisisitiza kuwa akiba ya chakula ipo ya kutosha.

Katika maelezo yake, Dk Tizeba alisema wizara yake kwa kushirikiana na Ofisi ya Waziri Mkuu (Tamisemi), Shirika la Chakula na Kilimo Duniani (FAO) na Taasisi ya Chakula na Lishe nchini (TFNC), wanafanya tathmini ya chakula nchini.

“Tathimini hiyo inayosimamiwa na kuratibiwa na Ofisi ya Waziri Mkuu, itaiwezesha Serikali kupata taarifa za uhakika zaidi kuhusu hali ya chakula na lishe, hasa katika maeneo yaliyoonekana kuwa na upungufu kwenye tathmini ya awali na yaliyojitokeza baada ya tathmini,” alisema Dk Tizeba.

Waziri Mkuu akiwa Dodoma naye aliwataka wananchi kuepuka upotoshaji unaofanywa na wafanyabiashara kuhusu hali ya chakula nchini, kwa lengo la kupandisha bei ya chakula.

Akizungumza wakati wa uzinduzi wa safari za ndege za Shirika la Ndege Tanzania (ATCL)  mjini humo, Waziri Mkuu Majaliwa alisema mwenye jukumu la kutoa taarifa za njaa ni Serikali pekee, si vyombo vya habari wala mtu yeyote.

Ufafanuzi huo wa Serikali umekuja huku wanasiasa na wasomi wakisema nchi inakabiliwa na njaa na Baraza la Maaskofu Tanzania (TEC) na Baraza Kuu la Waislamu Tanzania (Bakwata), yakiwataka waumini wao kufanya maombi, hija, mfungo kwa lengo la kukabiliana na ukame unaolikabili Taifa.

Katika ushauri wa kada hizo mbalimbali, juzi Mkuu wa Kanisa la Kiinjili na Kilutheri Tanzania (KKKT), Dk Frederick Shoo aliitaka Serikali kufanya tathmini ya kubaini upungufu wa chakula nchini.

“Nawashangaa sana watu, kwani ukame huu nimeuleta mimi au Kijazi (Dk Agnes- Mkurugenzi Mkuu wa Mamlaka ya Hali ya Hewa)? Wanakimbilia kulalama na kututupia maneno jambo ambalo si sawa,” alisema Dk Tizeba.

“Ukame umekuja wenyewe, msitengeneze jambo katika jamii na kwa bahati mbaya kauli zenu mkitoa zinaandikwa kila mahali na zinaleta shida,” alionya Waziri.

Huku akilia na wafanyabiashara, Waziri huyo alisema Serikali ina taarifa za wanaoficha chakula kwenye maghala wakisubiri bei ipande na kuwataka wakitoe   mara moja.

“Waliofungia chakula wapo wengi na tunawajua,tunaomba wakitoe na wakiuze kwa wananchi. Wasiisukume Serikali ifike hatua ambazo si za kawaida. Hatuwezi kuwavumilia watu hao, waache chakula kiingie sokoni, ’’ alisema Tizeba.

Alisema Serikali haitagawa chakula cha bure kwa wananchi kwa kuwa chakula kipo cha kutosha.

Dk Tizeba ambaye pia ni Mbunge wa Buchosa, alisema upatikanaji wa chakula nchini ni wa kuridhisha hasa vyakula kama mchele na maharage, na kwamba upatikanaji wa mahindi si wa kuridhisha sana.

“Pamoja na hali hii, bei za baadhi ya vyakula zimeanza kupanda kutokana na mazao kidogo kuingia sokoni kwa wakati huu kunakochangiwa na mwenendo usioridhisha wa unyeshaji mvua za vuli na kuchelewa kunyesha mvua za msimu kwenye maeneo mengi nchini,” alisema.

Alisema mvua za wastani zilinyesha Kagera, Mwanza, Geita, Kilimanjaro, Arusha, Mara, Pwani na Simiyu na mazao yaliyopandwa katika baadhi ya maeneo hayo yaliathiriwa na ukame hususan mkoa wa Kagera.

“Hali ya upatikanaji chakula unaridhisha isipokuwa bei ya mahindi imepanda ikilinganishwa na mwaka jana kipindi kama hiki. Hii inatokana na kutoingia sokoni kwa mazao mapya ya msimu wa mvua za vuli,” alisema.

Alisema Serikali kupitia Wakala wa Taifa wa Hifadhi ya Chakula (NFRA) kwa mwaka huu wa fedha, imepanga kununua tani 100,000 za chakula na hadi Januari 8, ilikuwa imenunua tani 62, 087 za mahindi.

Dk Tizeba aliwataka wananchi kutumia vizuri akiba ya chakula walichonacho na kuacha ya tamaa ya
kukiuza.

Huku akielezea kupanda na kushuka kwa bei ya mahindi, mchele na maharage, Dk Tizeba alisema jambo hilo ni la kawaida kutokea kwa kipindi kama hiki, kutokana na mwanzo wa msimu kukosa mazao sokoni, hivyo kusababisha bei kupanda na mwanzo wa mavuno bei kushuka kutokana na mazao mengi kuingia.

“Hali ya kutoridhisha ya unyeshaji mvua za vuli umechangia wafanyabiashara wa nafaka nchini, hasa wa mahindi kuingiza zao hilo kidogo sokoni na kuongeza kasi ya mahitaji kutoka kwa wananchi na kusababisha bei kuzidi kupanda,” alisema huku akitaja mkoa wa Lindi kuuza kwa bei ya juu gunia la maharage, mchele na mahindi.

Majaliwa

“Mwaka jana nchi ilikuwa na akiba ya chakula zaidi ya tani milioni tatu hali iliyofanya baadhi ya wabunge na wafanyabiashara kuomba kibali cha kuuza nafaka nje ya nchi.

“Serikali ilitoa kibali hicho baada ya kujiridhisha na akiba ya kutosha ya chakula. Baada ya kibali kutoka, tani milioni 1.5 ziliuzwa nje ya nchi,” alisema Majaliwa.

Alisema tani milioni 1.5 zilizobaki zilihifadhiwa akiba ambapo tayari wameruhusu ziuzwe nchini ili kupunguza kupanda kwa bei za vyakula.

“Naomba wananchi msiwe na wasiwasi juu ya hali ya chakula nchini. Msisikilize kelele zinazopigwa na watu mbalimbali na baadhi ya vyombo vya habari yakiwamo magazeti, kwani taarifa hizo si za kweli. Chakula kipo cha kutosha licha ya mvua kusuasua katika baadhi ya maeneo nchini,” alisema.

Alisema kwa kuwa mvua zimeanza kunyesha katika maeneo mbalimbali nchini, wananchi wanatapaswa kuzitumia kulima mazao ya muda mfupi yanayostahimili ukame.

Alisema iwapo nchi itakumbwa na uhaba wa chakula itatoa utaratibu wa namna ya upatikanaji wa chakula kwa wananchi wake.

Kuhusu kupanda kwa bei ya vyakula kwenye baadhi ya masoko, alisema inatokana na   uhaba wa chakula nchi jirani.
Share on Google Plus

About Unknown

    Blogger Comment
    Facebook Comment

0 comments:

Post a Comment

Laptop City

Tangazo