Tusishangilie mafanikio, tutekeleze sera kwa maendeleo


Mashaka Mgeta

Mashaka Mgeta
MWISHO wa wiki iliyopita, nilikuwa ninaangalia, kupitia runinga, hafla ya ufunguzi wa fainali za mashindano ya soka kwa nchi za Africa (Afcon) yanayoendelea nchini Gabon.

Ufunguzi huo ulitanguliwa na burudani za muziki, miongoni mwa waliotumbuiza akiwa ni kijana Mtanzania, Nasib Abdul maarufu kama Diamond Plantnumz.

Diamond kama anavyofahamika miongoni mwa wengi, aliagwa Januari 10, mwaka huu, akikabidhiwa bendera ya Taifa na Waziri wa Habari, Utamaduni, Wasanii na Michezo, Nape Nnauye.

Tukio la kukabidhiwa bendera halikuwa geni kwangu. Ninaamini halikuwa geni kwa watu wengi kwa maana imeshatokea na kuzoeleka mara ‘chungu nzima’, Watanzania kukabidhiwa bendera kama ilivyokuwa kwa Diamond.               

Lakini kitendo cha kuonekana kwa bendera hiyo kwenye ufunguzi wa mashindano ya AFCON kiliibua hisia na kuuona mwanga mpya.

Kwamba kama nchi itadhamiria na kuchukua hatua za utekelezaji kwa sera mbalimbali zilizopo, mipango na mikakati ya kitaifa ni dhahiri hakuna jambo la kitaifa, kikanda na kimataifa litakaloshindikana.

Pamoja na kutambua michango yawatu wengine waliowahi kuliwakilisha Taifa katika matukio tofauti, inapaswa kwa Taifa hususani wasimamizi na watekelezaji wa sera, mipango na mikakati ya maendeleo katika nyanja tofauti, kupata jawabu la kuivusha nchi kutoka hapa ilipo.

Imekuwa kawaida kwa wenye mamlaka ya kuyawezesha hayo, ili kuchagiza kasi ya mafanikio, wanakuwa nyuma, ushindi unapopatikana, wanajitokeza na ikibidi kwa kujivisha heshima wasiyoistahili.

Mathalani Diamond, akijituma na kuonesha uwezo mkubwa katika Sanaa ya muziki, jina lake linakua, uwezo wake unaongezeka kama ilivyo kwa kazi anazozipata iwe kwa kualikwa ama kwa kuomba.

Na anapojituma pasipo kujali ‘upweke’ anaokutana nao katika safari ngumu zinazompa mfanikio kila uchwao, anabaki kuwa Mtanzania na kuiwakilisha nchi.

Ndio maana akiwa na wenzake kadhaa, akaiweka Tanzania katikati ya ulimwengu ulioshuhudia ufunguzi wa mashindano ya Afcon, ingawa timu ya Taifa (Taifa Stars) haikufuzu mashindano hayo.

Nina hakika, kama Taifa Stars ingefuzu, ni dhahiri kwamba kungekuwapo Watanzania waliokwenda Gabon kuishangilia na hivyo kuungana na Diamond na wenzake ‘kuinogesha’ nchi kwenye mashindano hayo.

Lakini kama ilivyo kwa sekta nyingine, michezo imebaki kudorora licha ya kuwapo sera, mipango na mikakati inayosomeka na kueleweka vizuri. Tunakwenda wapi?

Hali kama hiyo ipo katika nyanja nyingine za kijamii hususani zinazolenga maendeleo ya kiuchumi na ustawi katika maisha ya watu.

Jitihada binafsi za raia zimeibua mafanikio dhidi ya utekelezaji wa mipango, mikakati na sera za pamoja kama taifa. Watanzania wengi hasa wenye dhamana za usimamizi na utekelezaji wa sera, mikakati na mipango wamebaki kuwa hodari wa kushangilia mafanikio binafsi badala ya kuwa sehemu ya kufanikisha mafanikio hayo.

Ndivyo ilivyotokea kwa Diamond mwishoni mwa wiki. Watu wengi walimshangilia, walishangilia mafanikio yake.

Nina hakika hata watungaji, wasimamizi na watekelezaji wa sera, mipango na mikakati inayohusu michezo na sanaa, walimshangilia Diamond, wakashangilia mafanikio yake. Lakini sina hakina kama walipataje ujasiri wa kuzihoji nafsi zao, “nimechangia nini katika hili?

Ama kama ningetimiza wajibu wangu, tungefikia ukomo gani wa kushangilia zaidi ya huu unaoishia kwa ‘mwalikwa’ Diamond?

Tukiuacha mfano huo, hivi sasa Serikali ya awamu ya tano chini ya Rais John Magufuli ipo katika mpango wa kuifanya nchi kuwa yenye uchumi unaotegemea viwanda.

Uchumi wa viwanda ni dhana pana. Hata tafsiri ya viwanda vidogo vinavyodaiwa kuchochea ukuaji wa uchumi kwa raia na kutengeneza ajira nyingi bado ‘inapindishwa’ hususani na wanasiasa.

Je, wenye dhamana kwa kila eneo husika wamejiandaa vipi kuitazama Tanzania, wakilenga ubunifu, ujuzi, taaluma, uzoefu na aina yoyote ya mchango utakaoifanya nchi kuwa ya viwanda?

Ama kama inavyoonekana sasa kwa Diamond, watu wataendelea kubweteka, washindwe kutimiza wajibu wao wakisubiri wachache ‘watakaotoka’ kwa mafanikio, basi tuungane kuwashangilia.

Pamoja na dhamira yake nzuri, Rais Magufuli pekee hawezi kuifanya Tanzania kufanikiwa katika sekta ya viwanda. Kwa maana ili viwanda viwepo, vikiwategemea na kuwanufaisha raia wa Tanzania, yapo mambo mengi yanayopaswa kufanyika.

Miongoni mwa hayo ni kuwasomesha na kuwaandaa wataalamu wa kuendesha ama kukarabati viwanda, wajuzi wa vipuri, wasambazaji wa malighafi za uzalishaji hususani mazao ya kilimo, watunzaji na wengine kedekede.

Sera za uchumi zipo, mipango na mikakati inayolisukuma gurudumu la sekta hiyo ipo, wasimamizi wake wake, je wanafanya nini sasa hivi kwa ajili ya Tanzania na Watanzania?

Rais mstaafu, Jakaya Kikwete, alipenda kutumia msemo mmoja wakati akihimiza jambo jema, kwamba “hili linawezekana ikiwa kila mmoja atatimiza wajibu wake.”

Hata sasa, maana ya usemi wa Rais mstaafu Kikwete maarufu kama JK bado ‘inaishi’ katikati ya maisha ya watu.

Pasipo kutimiza wajibu, watu wengi wataendelea kuwa washangiliaji wa mafanikio yanayofikiwa na wachache. Hapo taifa halitapiga hatua ya maendeleo. Ni muhimu Taifa likajikita katika utekelezaji wa sera, mipango na mipango ya maendeleo kwa vitendo.

0754691540
Share on Google Plus

About Unknown

    Blogger Comment
    Facebook Comment

0 comments:

Post a Comment

Laptop City

Tangazo