Walimu walioajiriwa mara mbili kudaiwa mishahara


Aidan Mhando, Mwanza

SIKU moja baada ya walimu watatu wa Serikali kukamatwa wakifundisha shule binafsi ya Musabe jijini hapa, Serikali ya Mkoa, imesema itawachukulia hatua za kisheria ikiwamo kutudisha mishahara waliyolipwa tangu walipoaga kwenda masomoni.

Walimu hao wanadaiwa kwa nyakati tofauti kumuaga mwajiri kuwa wanakwenda masomoni walikamatwa juzi na Polisi, wakifundisha shule hiyo, huku mmoja akitoroka kwa kuruka ukuta wa shule hiyo.

Jana Mkuu wa Wilaya ya Nyamagana, Mary Tesha akifuatana na polisi walifika shuleni hapo na kuhoji walimu hao, ambapo alisema alipata taarifa kutoka kwa wasamaria wema ya kuwapo walimu walio likizo ya masomo, lakini wanafundisha kwenye shule hiyo.

“Huu ni wizi, kwani walikuwa wanachukua mshahara wa Serikali na hapa wanalipwa pia. Kwa kushirikiana na wakurugenzi tutawahesabia kiasi gani cha fedha mpaka sasa wamechukua ili kuzirudisha,” alisema Tesha.

Aliongeza kuwa ni jambo la kushangaza kuona watumishi wa umma wanashindwa kusoma alama za nyakati, kwani kila mtu alisikia uhakiki wa watumishi hewa, lakini bado watu hawakomi na wanaendelea kukiuka sheria, hivyo lazima sheria ichukue mkondo wake.

Akizungumzia tukio hilo, Mkurugenzi wa Shule hiyo, Daniel Damian alisema ilikuwa vigumu kubaini kwamba walimu hao walikuwa waajiriwa wa Serikali kwani taratibu zote za shule walizifuata ikiwamo kusaini kitabu cha mahudhurio wakati wa kuingia na kutoka.

“Walikuja hapa wakaomba ajira. Sisi tuliwafanyia usaili na kuwaajiri, tuliwauliza kama waliajiriwa serikalini, walikataa. Tunashukuru Serikali mmetusaidia kwa hili, sasa tutakuwa makini,” alisema Damian.

Ofisa Elimu ya Sekondari wa Mkoa wa Mwanza, Gwasa Joseph alisema atafuatilia suala hilo kupata ukweli na hatua za kisheria zitachukuliwa dhidi yao, kwani kitendo hicho ni uvunjaji wa sheria na wamehusika na wizi serikalini.

“Huu ni wizi wa hali ya juu haiwezekani unaomba kwenda masomoni halafu unakwenda kuajiriwa kwingine. Sheria inasema wazi, kwamba mwalimu akiomba kusoma, akiwa   likizo lazima aripoti kwa mwajiri wake,” alisema Daimin.

Walimu waliokamatwa ni Lwiza Ntare (27) ambaye alikuwa akifundisha sekondari ya Kibehe, Chato, Geita; Richard Mgendi (30) akifundisha sekondari ya Misasi, Misungwi mkoani hapa na Gilbert Makwaya (33).

Kati yao mmoja aliyetoroka alikuwa Makamu Mkuu wa Shule hiyo kwa upande wa wanawake.


Share on Google Plus

About Unknown

    Blogger Comment
    Facebook Comment

0 comments:

Post a Comment

Laptop City

Tangazo