Polisi wadaiwa kusimamia uchomaji moto nyumba za wafugaji


Warioba Igombe, Morogoro

WAFUGAJI wa Jamii ya Wasukuma wamesema watoto wao wameshindwa kuhudhuria massomo kutokana na nyumba wanazoishi kuchomwa moto uliosababisha vifaa vyao ya shule kuteketea.

Mwenyekiti wa wafugaji hao, Dotto Dofu alisema jana kuwa zaidi ya watoto 50 wameshindwa kuhudhuria masomo yao darasani kutokana na kukosa nguo za shule.

Alifafanua kuwa Januari 13 mwaka huu, Polisi walifika katika kijiji cha Kisaki na kuzichoma nyumba hizo kwa moto kwa madai kuwa wafugaji hao wanaishi kwenye maeneo ya vyanzo vya maji wakati Serikali imezuia kuharibu vyanzo hivyo.

“Askari walifika maeneo haya na kuzichoma nyumba zetu zote kwa madai kuwa tunaharibu vyanzo vya maji kitendo kilichosababisha watoto wetu washindwe kwenda shule baada ya nguo zao za shule kuteketea kwa moto,” alisema Dofu.

Alisema kuwa askari hao walifika na kuamuru watoto waliowakuta kwenye kaya hizo kuchoma nyumba zao wenyewe, huku wao wakiwa wamewasimamia kwa silaha za moto, kitendo kilichofanya vijana hao kutii amri.

Kutokana na kitendo hicho, Dofu amesema hajui ni nini hatima ya watoto hao kuendelea na masomo, kwani baada ya kuchoma nyumba hizo vitu mbalimbali zikiwepo fedha na chakula viliteketea.

Alisema kuwa mbali na watoto wao kushindwa kuhudhuria masomo yao darasani, wamekuwa wakilala nje, ikiwa ni pamoja na kuishi kwa kutegemea misaada kutoka kwa ndugu na jamaa wanaoishi mikoa ya jirani.

Baadhi ya wazazi wa watoto hao wamepanga kuonana na uongozi wa shule ili watoto wao waweze kuruhusiwa kutumia nguo za nyumbani hadi pale watakapopata fedha ya kununua sare za shule.

Mkuu wa wilaya, Regina Chonjo amewataka wafugaji hao kuondoka maeneo ya vyanzo vya maji akibainisha kuwa wakiendelea kuishi katika maeneo hayo, Serikali itawachukulia hatua kali za kisheria.
Share on Google Plus

About Unknown

    Blogger Comment
    Facebook Comment

0 comments:

Post a Comment

Laptop City

Tangazo