Makonda, Mjema wawekwa mtegoni


Celina Mathew

George Simbachawene
WAZIRI wa Nchi Ofisi ya Rais Tawala za Mikoa na Serikali za Mitaa (Tamisemi) George Simbachawene ametoa siku tatu kwa Mkuu wa Mkoa na Wilaya ya Ilala, kuhakikisha wanawaondoa wamachinga wanaofanya biashara eneo la Mradi wa Mabasi Yaendayo Kasi (UDART), na wasipotekeleza hilo kibarua chao kitaota nyasi.

Kauli hiyo inakuja siku moja baada ya Rais John Magufuli kutangaza kuwa hataki kuona mmachinga yeyote anafanya biashara kwenye miundombinu ya mradi huo na atakayekiuka atachukuliwa hatua za kisheria.

Simbachawene aliitoa kauli hiyo Dar es Salaam jana wakati akizungumza na waandishi wa habari akisema hana nia mbaya na kauli ya Rais kuwa wamachinga wasibugudhiwe na wasiofuata sheria lazima wachukuliwe hatua kutokana na kusababisha changamoto kwa wapita njia na mabasi hayo.

“Rais aliposema wamachinga wasibughudhiwe si hao wanaovunja sharia, kwa kuwa wamachinga ni wastaarabu, hawezi kuwa mtu anayekaa kwenye barabara bali hao ni waleta fujo, aliomaanisha Rais ni wanaotii sheria na wakiambiwa eneo hili haliruhisiwi wanaondoka angalau hata kama halijapangwa rasmi, hupati changamoto,” alisema.

Alisema barabara hizo ni nyembamba lakini cha kushangaza wamachinga wanafanya biashara bila woga na alisisitiza kutumia nguvu kuwaondoa wasipotii amri hiyo na kuondoka kama wanavyotakiwa.’

“Natoa siku tatu, Mkuu wa Mkoa na wa Wilaya kuhakikisha wamachinga walio kwenye maeneo hayo wanaondoka kuanzia Fire, Msimbazi hadi Gerezani,” alisema.

Mkuu wa Mkoa wa Dar es Salaam ni Paul Makonda wakati Mkuu wa Wilaya ya Ilala akiwa ni Sophia Mjema.

Alisema endapo wamachinga watarudi eneo hilo, Mkuu wa Mkoa na wa Wilaya ya Ilala watambue kuwa kazi imewashinda, hivyo watakosa kibarua kwa kuwa Rais aliwataka kufuata sheria na si kufanya biashara kinyemela.

“Nikiona wamerudi, basi Mkuu wa Mkoa na Mkuu wa Wilaya kazi imewashinda maana mimi ninayetoa maagizo haya nipo chini ya Rais na ndiye anayeniagiza kila siku nifanye nini, kwa hiyo hakusema wafanye wanavyotaka na kwamba hawana haki bali alisema tusiwatoe bila kuwatafutia maeneo, hivyo watoe nafasi ili tutekeleze majukumu,” alisema.

Aliwataka kutambua kuwa wakati wao wanatimiza majukumu yao kuna haki za watu wengine hazitakiwi kuchezewa na kuwaomba wamsikie, wamwelewe na kisha watii amri kwa kuondoka kwenye barabara hiyo ya BRT.

“Nadhani jana mlimsikia Rais, alisema atakayechezea barabara ya BRT kamata peleka au choma tairi, huyo ni Rais amesema, sasa mimi niseme nini?” Alihoji Simbachawene.

Aliwataka wamachinga waondoke kwenye miundombinu ya barabara kuanzia Kimara-Morocco, Kimara - Feri na Kimara-Gerezani hasa Gerezani, kwa kuwa hata eneo la kukata kona ni shida hivyo hawawezi kuacha liendelee.


Share on Google Plus

About Unknown

    Blogger Comment
    Facebook Comment

0 comments:

Post a Comment

Laptop City

Tangazo