Waziri Mkuu ataka watumishi weledi



Mwandishi Wetu, Dodoma

Waziri Mkuu Kassim Majaliwa
WAZIRI Mkuu Kassim Majaliwa amesema wakati umefika wa kuwa na watumishi wenye weledi wa kutosha kwenye halmashauri zote nchini na pia hazitakiwi kuwa pango la wezi, wazembe au jalala la kutupa wabadhirifu walioshindikana kwingineko.

Aidha, Waziri Mkuu amesema serikali za mitaa na halmashauri zote nchini zinatakiwa kujitathmini na kujipanga vizuri zaidi kuona jinsi zitakavyokuwa chachu ya maendeleo ya viwanda tarajiwa.

Waziri Mkuu alitoa kauli hiyo jana wakati akifungua kikao cha Baraza la Mashauriano (RCC) mkoani hapa. Alisema kikao ni chombo muhimu na endapo kitatumika vizuri kitasaidia kusukuma maendeleo ya mkoa na kupunguza migogoro kwenye halmashauri.

Alisema Serikali itaendelea kuongeza ruzuku kwa halmashauri zote nchini kwa kadri uwezo utakavyoruhusu na kusisitiza, kuwa fedha hizo lazima zisimamiwe vizuri na zielekezwe kwenye miradi ya maendeleo inayogusa wananchi.

“Endapo itabainika kuwapo baadhi ya sheria zinazokwamisha utendaji katika mamlaka za serikali za mitaa, hatutasita kuzifanyia mapitio na hatimaye kuzibadili ili ziendane na azma yetu ya kutoa huduma bora kwa wananchi,” alisema.

Alisema Serikali Kuu ina maslahi makubwa kwa serikali za mitaa, si tu kwa kuwa ni Serikali kamili katika ngazi hiyo, bali pia kutokana na ukweli kwamba kero nyingi za wananchi ziko ngazi hiyo.

Waziri Mkuu alisema vyanzo vingi vya mapato ya Serikali vinapatikana kwenye halmashauri huku changamoto kubwa ikiwa ni kulegalega kwa halmashauri nyingi katika ukusanyaji mapato ya kodi na yasiyo ya kodi, jambo linalozorotesha utoaji huduma kwa wananchi.

Hivyo Waziri Mkuu alitoa rai kwa halmashauri hizo kuendelea kuboresha huduma kwa wananchi na kutatua kero zao kikamilifu na kwa wakati pamoja na kubuni vyanzo vipya vya mapato na kuongeza kasi ya ukusanyaji mapato.

Pia alizitaka zihakikishe malipo yote yanafanyika kielektoniki na zihamasishe vijana na kina mama wajiunge na vikundi vya uzalishajimali na kuwapa stadi za kazi na mikopo yenye masharti nafuu ili kuwa chanzo cha mapato baadaye.

Alisema watendaji wa halmashauri wanatakiwa kujiepusha na rushwa na ubadhirifu wa mali za umma na uzembe kazini na watakaobainika kufanya vitendo hivyo  wachukuliwe hatua kali za kisheria na kinidhamu.

“Someni taarifa ya CAG (Mkaguzi na Mdhibiti Mkuu wa Hesabu za Serikali) na kutoa majibu ya kina ya namna mtakavyodhibiti mianya ya rushwa na ubadhirifu kama ilivyoainishwa kwenye ripoti hizo,” alisema.

Hata hivyo, alitaka kila Halmashauri iandae mpango wa utekelezaji wa Ilani ya CCM kwenye maeneo makubwa ya kipaumbele, kama vile ujenzi wa miundombinu ya shule, maboresho kwenye sekta ya afya (ujenzi wa hospitali, zahanati na vituo vya afya).

“Endeleeni kuwa na uhusiano mzuri miongoni mwenu, fanyeni kazi kwa kuzingatia sheria, kanuni na taratibu.  Kila mmoja kwa nafasi aliyonayo atimize wajibu wake na kuzingatia mipaka ya nafasi yake. Punguzeni migogoro, matusi, dharau, bezo na vitisho. Mshirikiane, na jamii ione mko wamoja,” alisema.
Share on Google Plus

About Unknown

    Blogger Comment
    Facebook Comment

0 comments:

Post a Comment

Laptop City

Tangazo