TAZARA Zambia hali si shwari


Leonce Zimbandu

SIKU 60 zimepita baada ya Rais John Magufuli kukutana na Rais wa Zambia, Edgar Lungu kuzungumzia kuimarisha Mamlaka ya Reli Tanzania na Zambia (TAZARA), bundi ametua upande wa Zambia baada ya huduma ya usafiri wa treni kusitishwa kwa muda usiojulikana.

Huduma hiyo imesitishwa baada ya vyama viwili vya wafanyakazi nchini humo kuwatangazia wanachama wao kukusanyika kutafakari, huku wakidai marekebisho ya mishahara yao kulipwa kwa dola za Marekani.

Msemaji wa TAZARA, Conrad Simuchile alithibisha jana kusitishwa kwa huduma hiyo alipozungumza na gazeti hili makao makuu ya Tazara Dar es Salaam.

Alisema shughuli za usafiri wa treni ya abiria zitaathirika upande wa Zambia kutoka Ndola hadi Kapiri Mposhi lakini Tanzania treni za abiria na mizigo zinaendelea kutoa huduma kuanzia Dar es Salaam hadi Mbeya.

“Mazungumzo kati ya pande mbili yanaendelea kujadiliana na kutaka wafanyakazi warudi kazini huku majadiliano yakiendelea, kuepusha usumbufu kwa wateja,” alisema.

Alisema mazungumzo hayo yanafanyika kati ya Serikali, Chama cha Wafanyakazi wa TAZARA Zambia (WUTAZ) na Wafanyakazi na Umoja wa Wafanyakazi wa Zambia (CRAWUZ) kwa lengo la kupata ufumbuzi wa kudumu.

Aliongeza kuwa kitendo cha kusitisha usafiri kina lengo la kurudisha nyuma maendeleo ya Mamlaka hiyo, kwani tayari ilianza kurudisha imani kwa wateja baada ya kuyumba kwa utulivu wa uendeshaji kwa miaka mingi kupita.

Novemba 28, mwaka jana marais Magufuli na Lungu walikubaliana kuchukua hatua madhubuti ya kuboresha utendaji kazi wa Tazara na bomba la kusafirisha mafuta la Tanzania na Zambia (Tazama) ili miradi hiyo ilete manufaa kwa wananchi wa Tanzania na Zambia.
Share on Google Plus

About Unknown

    Blogger Comment
    Facebook Comment

0 comments:

Post a Comment

Laptop City

Tangazo