Wabunge watakiwa kuelewa ushiriki uwekezaji


Mwandishi Wetu, Dodoma

WABUNGE wametakiwa kuielewa dhana ya ushiriki wa Watanzania kwenye uwekezaji ili kuwa mstari wa mbele kuelimisha wananchi kushiriki shughuli za kiuchumi na uwekezaji nchini.

Mwito huo umetolewa na Serikali kupitia Waziri wa Nchi Ofisi ya Waziri Mkuu, Sera, Bunge, Kazi, Vijana, Ajira na Walemavu, Jenista Mhagama aliyesema wabunge kama wawakilishi wa wananchi, wana nafasi kubwa ya kuwaelimisha kuhusu kuwawezesha Watanzania kuwa sehemu kubwa ya wamiliki wa uchumi.

“Mafunzo haya yanatolewa kwenu kusaidia kuleta mabadiliko chanya na jamii zitashirikishwa kikamilifu katika uwekezaji unaofanywa katika maeneo yao kupitia ninyi wabunge,” alisema Waziri Mhagama.

Akizungumza kwenye Semina Elekezi kwa Kamati za Bunge juu ya ushiriki wa wananchi katika uwekezaji iliyoandaliwa na Baraza la Taifa la Uwezeshaji Wananchi Kiuchumi (NEEC) mwishoni mwa wiki mjini hapa, Mhagama alisema wakati umefika kwa Watanzania kunufaika na uwekezaji.

“Ni muhimu wananchi katika sehemu ambapo viwanda au miradi inaanzishwa kushirikishwa hatua za awali za uwekezaji au utekelezaji wa miradi,” alisema Waziri  na kuongezea kuwa lengo la kufanya hivyo ni kuhakikisha kuna uwazi na wananchi wajione ni sehemu ya uamuzi.

Alisema mafunzo hayo kwa kamati za Bunge pia yametoa nafasi kwa wabunge kutambua majukumu ya NEEC ambalo ndilo lenye dhamana ya kuratibu shughuli zote za uwezeshaji nchini.

Mwenyekiti wa Bodi ya NEEC, Dk John Jingu alisema uhusiano wa karibu kati ya wawekezaji na wananchi wa eneo la mradi unatakiwa kuimarishwa ili wananchi wanufaike na uwekezaji wa miradi kwenye maeneo yao.

“Changamoto kubwa ni ujuzi wa wananchi katika uwekezaji na ushiriki wao,” alisema Dk Jingu na kuongeza kuwa Baraza limejipanga kuhakikisha wananchi wanapewa elimu ya namna bora ya kushiriki uwekezaji na kukuza uchumi wao.

Mbunge wa Muheza ambaye ni Mwenyekiti wa Kamati ya Ulinzi na Usalama, Balozi Adadi Rajabu alisema semina hiyo ilikuwa na umuhimu mkubwa kwa wabunge, kwani itawasaidia kuwaelimisha wananchi juu ya ushiriki wao kwenye miradi inayofanyika kwenye maeneo yao.

“Tuna kila sababu za kuelimisha wananchi wetu juu ya kuongeza thamani ya bidhaa ili kuendana na matakwa ya wawekezaji,” alisema Balozi Adadi na kutaka sheria zinalinde wazawa katika ushiriki wao kwenye uwekezaji.

Mbunge wa Muleba Kusini, Profesa Anna Tibaijuka alisema ni vema Baraza na wadau wengine watathmini mambo yaliyofanyika na yanayotarajia kufanyika ili watu wote wazungumze lugha moja juu ya ushiriki wa wananchi kwenye uwekezaji.

Katibu Mtendaji wa NEEC, Beng’i Issa alisema lengo kuu la semina hiyo kwa wabunge ni kuwafahamisha majukumu ya Baraza na mchango wao katika dhana ya ushiriki wa wananchi kwenye uwekezaji.

Jumla ya wajumbe 152 wa kamati za Bunge walihudhuria semina hiyo iliyodhaminiwa na Shirika la Maendeleo la Umoja wa Mataifa (UNDP).
Share on Google Plus

About Unknown

    Blogger Comment
    Facebook Comment

0 comments:

Post a Comment

Laptop City

Tangazo