Walimu wakuu 21 wavuliwa madaraka


Aidan Mhando, Mwanza

WALIMU wakuu 21 wa shule za msingi katika Halmashauri ya Ukerewe, mkoani hapa, wamevuliwa madaraka kwa tuhuma mbalimbali zikiwamo za kuisababishia Serikali hasara ya mamilioni ya fedha kwa kuhurusu usajili wa wanafunzi hewa.

Pia, walimu hao wamevuliwa madaraka kutokana na matumizi mabaya ya madaraka, ikiwamo kushindwa kusimamia miradi ya shule na kusababisha shule tano za visiwa hivyo kukosa vyoo.

Hatua hiyo ilichukuliwa na Mkurugenzi wa Halmashauri hiyo, Frank Bahati baada kubaini kuwa walimu hao wameshindwa kuwajibika na kukosa umakini katika kusimamia maendeleo ya shule zao, taaluma, miradi ya shule na ukiukaji maadili.

Akizungumza na waandishi wa habari wilayani humo hivi karibuni, Mkurugenzi huyo alisema uzembe wa walimu hao umesababisha shule tano kufungwa kwa kukosa vyoo.

“Baada ya walimu kushindwa kutekeleza agizo langu la kuwasilisha mpango mkakati wa kutatua  changamoto katika shule zao, nimeamua kuchukua hatua za kinidhamu,” alisema Bahati na kuongeza:

“Nawavua madaraka walimu hawa kutokana na uzembe. Niliwaagiza  kuwasilisha mpango mkakati wa kutatua baadhi ya changamoto, lakini wameshindwa kufanya hivyo. Shule zinakosa vyoo, ni uzembe wa hali ya juu. Miradi ya shule inashindwa kusimamiwa ipasavyo,” alisema Bahati.

Bahati alisema walibaini kuwepo wanafunzi hewa waliosajiliwa, matumizi mabaya ya madaraka, hali inayoonesha kwamba wameshindwa kazi, hivyo Serikali haiwezi kuvumilia uzembe.

Serikali imekuwa ikikemea na kuchukua hatua za kuondoa watumishi hewa jambo ambalo lilisababisha baadhi ya watumishi wa umma kupoteza kazi kwa suala hilo

Halmashauri ya Wilaya ya Ukerewe ina visiwa 38, shule za msingi za Serikali 123, walimu 1,600 na wanafunzi 102,114.
Share on Google Plus

About Unknown

    Blogger Comment
    Facebook Comment

0 comments:

Post a Comment

Laptop City

Tangazo