Wenyeviti mitaani kuendelea kuhodhi mihuri


Peter Akaro

George Simbachawane
SERIKALI imefuta mwongozo uliotaka wenyeviti wa serikali za mitaa na vijiji kusitisha matumizi ya mihuri, badala yake jambo hilo sasa litajadiliwa kwa kushirikiana ili kufikia uamuzi utakaosaidia wananchi.

Akizungumza jana Dar es Salaam, Waziri wa Nchi, Ofisi ya Rais, Tawala za Mkoa na Serikali za Mitaa, George Simbachawane, alisema wenyeviti wamekuwa wakifanya kazi katika mazingira magumu ya kuhudumia wananchi, hivyo haoni sababu ya kulumbana muda huu.

“Ninasitisha mwongozo uliotolewa hadi tukakaposhirikishana kwa kuangalia namna bora ya kuhudumia wananchi.

“Hakukuwa na ajenda yoyote ila ni kuweka utaratibu mzuri ambao tulilenga kudhibiti wanaotumia mihuri kinyume na taratibu,” alisema.

Alisema mwongozo huo haukuwa na dhamira ya kuwapunguzia wenyeviti mamlaka na heshima zao, bali kuweka utendaji mzuri katika ngazi za chini za serikali.

“Mwongozo ulitolewa kwa sababu ya matumizi mabaya ya mihuri inayofanywa na baadhi ya wenyeviti, vijijini na hata mijini ambayo imechangia migogoro mingi ya ardhi nchini,” alisema.

Alitolea mfano sheria namba nne na namba tano za mwaka 1999 zinazoeleza mwisho wa Mwenyekiti wa Kijiji kutoa ardhi kwa mwekezaji au mgeni kuwa ni ekari 50 lakini wapo ambao wanatoa ardhi hadi ekari 100 na 1,000.

“Mahali ambapo Mwenyekiti amesaini, akagonga na muhuri hati ile inahesabika ina nguvu kisheria kama ilivyo hati inayotolewa na Wizara ya Ardhi, ingawa utoaji huo unakiuka sheria,” alisema.

Alisema mijini utawala wa ardhi unasimamiwa na sheria namba nane ya mwaka 2007 ambayo inasema eneo likishakuwa la mipango miji, sheria ya vijiji inaondoka, lakini hilo limekuwa likipuuzwa na ndiyo maana kumekuwa na migongano ya hati kwa kutumia mihuri

Alisema ipo sheria ambayo inasimamia vitendea kazi kwa wenyeviti wa serikali za mitaa na vijiji ambayo ni Tangazo la Serikali namba tatu la mwaka 1994.

Sheria hiyo inataja vitendea kazi vya Mwenyekiti kuwa ni Bendera yenye nembo ya halmashauri, usajili wa wakazi wote, daftari la muhutasari ya vikao vya mtaa, ila haitaji muhuri.

“Nguvu ya Mwenyekiti haiko kwenye muhuri na ndiyo maana hata Rais hana muhuri isipokuwa Katibu Mkuu Kiongozi, hivyo wenyeviti waelewe nguvu yao iko kwenye utendaji na uamuzi,” alisema.

Uamuzi huu wa Serikali umekuja siku moja baada ya wenyeviti wa serikali za mitaa jijini Dar es Salaam kutangaza azma ya kugomea shughuli zao za usimamizi wa amani na usalama kwenye maeneo yao na kuhudumia wananchi kutokana na mwongozo wa kunyang’anywa mihuri.
Share on Google Plus

About Unknown

    Blogger Comment
    Facebook Comment

0 comments:

Post a Comment

Laptop City

Tangazo