Wenyeviti mitaa Dar wabwaga manyanga


Dalila Sharif

WENYEVITI 400 na wajumbe 130 wa serikali za mitaa mkoa wa Dar es Salaam wamejivua madaraka kwa kutoshiriki kutoa huduma kwenye mitaa yao, ikiwa ni baada ya Serikali kuwaagiza kurejesha mihuri yake waliyokuwa wakiitumia katika kazi zao.

Mbali na kutangaza kujivua madaraka, wenyeviti hao wamedai kuwa watalifikisha shauri hilo mahakamani ili kupata tafsiri ya kisheria juu ya utendaji kazi wao.

Tamko hilo lilitolewa jana Dar es Salaam na katibu wa wenyeviti hao, Mariam Machicha kwenye mkutano uliofanyika katika ukumbi wa TCC Chang’ombe.

Mariam alisema kwa mujibu wa tamko la Serikali Novemba 30 mwaka jana barua kutoka Ofisi ya Rais,Tawala za Mikoa na Serikali za Mitaa ikisainiwa na Katibu Mkuu Musa Iyombe, kuhusu mwongozo wa matumizi ya mihuri kwa wenyeviti wa mitaa na vijiji:

“Mtu yeyote atakayechaguliwa kuwa Mwenyekiti wa Mtaa au Kijiji, atatakiwa awe na   bendera yenye nembo ya Halmashauri, rejesta ya wakazi wote wa mtaa na daftari la mihutasari ya vikao vya mtaa,” alisema Mariam.

Aliongeza kuwa kutokana na tamko hilo wenyeviti wa mkoa wa Dar es Salaam, walikubaliana kurudisha mihuri ya Halmashauri kwenye manispaa walizochukulia na kutoa tamko lao kwamba:

“Wenyeviti wote hawatashiriki vikao vya kamati za maendeleo ya kata na hawatafika ofisi za serikali za mitaa kutoa huduma za kijamii kwa wananchi wa maeneo yao.

“Kutokana na hili wenyeviti tunakubali kwamba kitendo hiki cha kutotumia mihuri kitasababisha athari kubwa katika mfumo wa uongozi na utoaji huduma kwa umma.”

Mariam alisema wenyeviti hao watashindwa kutoa huduma kwa wananchi kwa wakati wote na kuanzia sasa hawatasimamia ulinzi na usalama wa wananchi kwenye mitaa yao.

“Kwa hali hiyo, hususan kwa watumizi ya vyombo vya moto kama silaha, hatutasaini na wananchi watatangatanga na kupata usumbufu wa kupata huduma kwenye ofisi za kata kwa sababu watendaji wengi hawajui matatizo ya wananchi,” alisema Mariam.

Kiongozi wa wenyeviti wa mkoa wa Dar es Salaam, Juma Mgendwa aliwataka wenyeviti hao kurudisha mihuri kwenye manispaa zao na walioichonga wenyewe waache kuitumia.

Mkuu wa Wilaya ya Temeke, Felix Lyaniva aliwataka wenyeviti hao kutii agizo la Serikali na kuendelea na majukumu yao kwa kushirikiana na watendaji wa mitaa  kutoa huduma kwa jamii.

“Ni vema kuwa na busara na kutekeleza tamko hilo, kwa kuwa wapo baadhi walioanza kurudisha mihuri hiyo, hivyo ni vema hatua hii ikafanyika  kwa amani,” alisema Lyaniva.
Share on Google Plus

About Unknown

    Blogger Comment
    Facebook Comment

0 comments:

Post a Comment

Laptop City

Tangazo