Sababu 23 zatajwa Mtwara kuanguka kielimu


Waandishi Wetu

Dk Charles Msonde
SIKU moja baada ya Baraza la Mitihani la Taifa (Necta), kutangaza matokeo ya kidato cha pili huku shule tisa kati ya 10 zilizofanya vibaya zikiwa za Mtwara, wadau wa elimu, ukiwamo Umoja wa Wabunge wa Mkoa huo wametaja sababu 23 za anguko la shule hizo.

Wakati sababu hizo zikianikwa, taarifa kutoka Mtwara zilizolifikia gazeti hili zilieleza kuwa wakuu wa shule zilizofanya vibaya wamepewa waraka wa kuwazuia kuzungumza chochote kuhusu matokeo hayo.

Matokeo hayo yaliyotangazwa na Katibu Mkuu wa Necta, Dk Charles Msonde, yanazitaja shule hizo kuwa ni Chingungwe, Malocho, Naputa, Chanikanguo, Mtiniko, Michinga, Msimbati, Salama na Lukokoda.

Katibu wa wabunge wa mkoa huo ambaye pia ni Mbunge wa Nanyamba, Abdallah Chikota alizitaja baadhi ya sababu hizo, kuwa ni usimamizi mbovu wa sekta ya elimu ambapo alifafanua kuwa maofisa elimu wameshindwa kufanya kazi zao ipasavyo kwa kukosa vitendea kazi.

Alitaja sababu zingine kuwa ni kutotatuliwa kwa kero za walimu kwa muda mrefu, hali ambayo inachangia wakate tamaa na elimu kukosa kipaumbele kama ilivyokuwa katika uuzaji wa korosho.

“Sababu nyingine ni kukosekana kwa mazingira mazuri ya kufundishia na kujifunzia, kukosekana kwa maabara, jamii kukosa mwamko katika kuwekeza kwenye elimu na wazazi kutokamilisha majukumu yao,” alisema.

Chikota alisema sababu zingine ni umbali wa shule za mkoa huo ambapo pia hakuna hosteli, jambo ambalo linachangia wanafunzi kukataa tamaa, wanafunzi kukosa mtu ambaye wanajifunza kwake kama kivutio na watoto kutopenda shule.

Alisema ni jukumu la Serikali kuuangalia mkoa huo kwa jicho la huruma, huku akisisitiza kuwa kufeli kwa wanafunzi hao kusihusishwe na uvunaji korosho.

Katibu Mkuu wa Shirikisho la Wamiliki na Mameneja wa Shule na Vyuo visivyo vya Serikali (Tamongsco), Benjamin Nkoya alisema sababu nyingine ni mkoa huo kutumika kama sehemu ya adhabu kwa walimu wanaoonekana kukosa uhusiano mzuri na wanasiasa na wanaopigia kelele uboreshaji elimu.

Alitaja sababu zingine ni mila na desturi, njaa, uhaba wa walimu, na walimu waliokuwa na vyeti bandia waliofukuzwa inaweza kuwa sababu pia.

"Inawezekana mkoa huo ulikuwa na walimu wenye vyeti bandia ambao kufukuzwa kwao kumesababisha hata kile kidogo walichokuwa wanatoa kwa wanafunzi kukosekana," alisema.

Alisema pia Serikali imetilia mkazo kufuatilia shule binafsi na kusahau shule zake jambo ambalo linapaswa kuachwa kutokana na kukosa tija.

”Utakuta shule ina wanafunzi zaidi ya 200 katika darasa moja, haina maabara huku inatoa wanafunzi wa Sayansi lakini hayo yote katika uhakiki huo hayaandikwi kama inavyofanyika katika shule binafsi,” alisema.

Alisema sababu nyingine ni walimu kupanga migomo kwenye shule za Serikali, kukosa vitabu na taarifa za ukaguzi.

Katibu Mkuu wa Chama cha Walimu Tanzania (CWT), Ezekiah Oluoch alisema idadi ya walimu katika shule za Serikali ni tofauti na shule binafsi.

"Shule nyingi za Serikali mazingira si rafiki, kwa mfano hadi sasa shule za msingi zina uhaba wa walimu 100,000 huku wahitimu zaidi ya 30,000 hawajaajiriwa, na asilimia 75 ya shule hizo ziko vijijini ambazo pia hukumbana na changamoto mbalimbali," alisema.

Aidha, Mtwara alisema kuwa mila na desturi, uhaba wa walimu ndizo zimekuwa zikichangia wanafunzi kufeli, hivyo alitumia nafasi hiyo kupongeza wanafunzi waliofanya vizuri katika mkoa huo na kubainisha kuwa wamejitahidi sana.

Aliitaka Serikali kuboresha mazingira na maslahi ya walimu ili waweze kufundisha vizuri na kuanzisha programu ya chakula shuleni.

Mbunge wa Kigamboni, Dk Faustine Ndungulile alisema mfumo wa elimu na mitaala vinaweza kuwa sababu za matokeo mabaya ya mitihani nchini.

Ndungulile alisema ni wakati wa wadau kukutana na kujadili changamoto zinazoikumba mikoa ambayo inafanya vibaya katika mitihani ya elimu ya msingi na sekondari nchini, ili kupata mafanikio.

“Mbaya zaidi wanafunzi wanafeli masomo ya Sayansi na Hisabati ni hatari kwa Taifa ambalo linataka kuwa la viwanda,” alisema.

Wakati wadau wakiwa na mitazamo hiyo inasemekana katika Manispaa ya Mtwara, walimu wa shule wamepewa waraka kuwataka kutozungumzia hali hiyo.

Walimu hao walisema kweli hali ni mbaya na changamoto ni kubwa, lakini hawana ruhusa ya kuzungumzia jambo hilo kinyume na hapo, hadi mwandishi wa habari afuate taratibu za kupata kibali kwa Mkurugenzi wa Manispaa hiyo.

“Hatuna nafasi ya kulisemea hili sisi walimu lakini kielimu hali Mtwara bado jitihada kubwa zinahitajika ili kuisaidia, mimi naomba tu ufuate taratibu husika,” alisema kwa masharti ya kutotajwa jina gazetini

Diwani wa Majengo, Ziha Khalidi akiwa mzazi alisema jambo hilo si la kawaida kwa mkoa huo, ambapo alitaka kuwekwa mazingira mazuri ya walimu yakiwamo madarasa ya kufundishia, nyumba za walimu, kuwezeshwa kifedha na masuala mengnine ambayo yatamfanya mwalimu kuwa na moyo wa kufundisha.

Ofisa Elimu wa Mkoa, Fatuma Kilimia alipopigiwa simu na gazeti hili kutaka azungumzie hali hiyo alishindwa kuizungumzia.

Mkurugenzi wa Manispaa simu yake iliita bila majibu huku Mkuu wa Mkoa, Halima Dendegu akisema yuko kwenye kikao na kuahidi kumpigia simu mwandishi, lakini hakufanya hivyo jana.

Imeandikwa na Suleiman Msuya, Emerciana Athanas na Sijawa Omary


Share on Google Plus

About Unknown

    Blogger Comment
    Facebook Comment

0 comments:

Post a Comment

Laptop City

Tangazo