Ukawa yashangaa


*Yajiuliza kilichojiri uchaguzi mdogo udiwani, ubunge
*Yataja sababu tano zilizoisababishia ‘kuangukia pua’

Waandishi Wetu

Danda Juju
WAKATI taarifa za ndani zikionesha kuwa kati ya kata 22 zilizofanya uchaguzi mdogo juzi, CCM imeshinda kata 21, vyama vinavyounda Umoja wa Katiba ya Wananchi (Ukawa), vimetaja sababu tano zilizochangia kuanguka kwenye uchaguzi huo.

Taarifa zilizolifikia gazeti hili jana zilieleza kuwa Chadema ndiyo iliyotetea kata hiyo, huku CUF ikipokwa moja na kuacha maswali mengi kuhusu nguvu iliyotumiwa na vyama hivyo kwenye kampeni, ambayo hailingani na matokeo. 

Wakizungumza kwa nyakati tofauti na JAMBO LEO jana Dar es Salaam, viongozi wa vyama hivyo walilalamikia hatua ya kuzuiwa kwa mikutano ya hadhara na maandamano, kuwa imechangia kuanguka kwao.

Sababu nyingine ilitajwa kuwa ni kila chama kuweka wagombea, vijana kutishwa kupiga kura na kuwaachia wazee tu, upande wa CUF unaomwunga mkono Profesa Ibrahim Lipumba kuweka wagombea na mgogoro wa ndani ya chama hicho katika pande zote za Muungano.

Mikutano

Katibu Mkuu wa NCCR-Mageuzi, Danda Juju, alisema hatua ya Serikali kuzuia mikutano ya hadhara na maandamano ya amani, ni moja ya sababu iliyochangia Ukawa kufanya vibaya katika uchaguzi mdogo wa marudio ya udiwani.

“Mimi binafsi haya matokeo hayajanishangaza niliyajua, kwa sababu tangu mwanzo nilishasema, kazi kubwa ya vyama vya siasa ni kufanya mikutano ya hadhara na maandamano ya amani yanayoonesha hisia lakini imepigwa marufuku,” alisema Juju.

Juju alisema kwa kitendo cha kunyamazishwa vyama vya upinzani kufanya mikutano ya hadhara na maandamano na ubabe wa Serikali kinakwenda kuua au kunyonga vyama vya upinzani.

Alieleza kwamba wakati wao wakizuiwa, CCM imeendelea kufanya mikutano ya hadhara kupitia wakuu wa mikoa, wilaya, Rais na watendaji wa ngazi ya kata, ikitumia fursa hiyo kukutana na wananchi na kuendelea kujiimarisha.

Wakati Juju analalamikia hatua hiyo ya Serikali, mjumbe wa Kamati Kuu ya Chadema, Edward Lowassa amekuwa akibeza hatua hiyo na kusema vikao vyao vya ndani na wanachama vimewaimarisha zaidi kuliko mikutano ya hadhara.

Kutoachiana

Akizungumzia kuhusu kutoachiana wagombea kwenye baadhi ya kata kama utaratibu wao, Juju alisema kitendo hicho kimeonesha udhaifu ndani ya Ukawa ambao wanatakiwa kuuchukua kama changamoto na kuifanyia kazi ili kujiimarisha.

Mkurugenzi wa Uchaguzi wa CUFShaweji Mketo alisema kushindwa kwao kwenye uchaguzi huu kumesababishwa kwa kiasi kikubwa na mienendo ya Serikali kutisha vijana, hivyo kushindwa kujitokeza kupiga kura.

Shaweji alitaja sababu nyingine kuwa vijana kutojitokeza kwenye uchaguzi, kwa sababu ya kukata tamaa na kutokana na hali hiyo, wamekuwa wakirubuniwa na kutoa vitambulisho vyao kwa kupewa ‘bahasha’ na CCM ili wasijitokeze.

Alisema kutokana na hali hiyo, wanaojitokeza kupiga kura ni wachache ambao ni wanawake na wazee kwa kuwa wakati mwingine vijana wanaona hata wakijitokeza, vyama vya upinzani haviwezi kushinda.

Akizungumzia suala la kutoachiana baadhi ya kata, alidai Mwenyekiti wa CUF, Profesa Lipumba na timu yake, ndio walivuruga utaratibu kwani wao walisema hawatashirikiana na Ukawa na hivyo kuweka wagombea katika kata zote.

Kutokana na hali hiyo, Shaweji alisema walijikuta vyama vingine vya Ukawa vikiweka wagombea kwenye kata hizo wakiwa na lengo la kuivuruga CUF ya Lipumba isishinde.

“Kwa mfano kata ya Kijichi, CUF ilionekana kuwa na nguvu tangu uchaguzi uliopita, lakini vyama vingine viliweka wagombea ili kuivurugia CUF isishinde,” alisema Mketo.

Naibu Katibu Mkuu wa Chadema, Salum Mwalimu alisema matarajio yao yalikuwa ni kushinda kwa kishindo, lakini matokeo yamekuwa kinyume.

“Unapoingia kwenye uchaguzi, unaamini unakwenda kushinda na si kushindwa, kwa hiyo matarajio yetu yalikuwa nji kushinda tena vizuri sana,” alisema Mwalimu.

Aliongeza kuwa hawezi kusema sababu zilizochangia kushindwa kwao kwa kuwa bado hawajapata mrejesho wa hali ilivyokuwa kutoka kata mbalimbali, ili kufanya tathmini.  

Mgogoro CUF

Wakati huo huo, Jumuiya ya Vijana ya CUF (Juvicuf), imesema mgogoro unaondelea ndani ya  chama hicho umesababisha kufanya vibaya kwenye uchaguzi huo.

Kutokana na hali hiyo, Juvicuf imewataka vijana wote wa chama hicho kurudi nyuma na kutafakari hatima ya chama chao na wasipofanya hivyo, upo uwezekano wa uchaguzi wa mwaka 2020 ‘kuwawashia taa nyekundu’.

Mwenyekiti wa Juvicuf ambaye pia ni Mbunge wa Mchinga, Hamidu Bobal alisema hayo jana alipozungumza na waandishi wa habari Dar es Salaam.

Bobal alisema hakuna sababu ya wanachama wa CUF kutafuta mchawi kutokana na matokeo hayo, kwani ushahidi upo wa kutosha kuwa mgogoro uliopo unakimaliza chama.

Alisema mgogoro wa CUF ulikuwa ni kati ya Profesa Lipumba na chama, ila kwa sasa umeongeza maadui ambao ni vyombo vya Dola na CCM, jambo linalozidi kuharibu chama.

Mwenyekiti huyo alisema pamoja na mikakati ambayo inaongozwa na makundi hayo, bado wana CUF hasa vijana wana wajibu wa kutafakari na kuchukua uamuzi kuhusu chama chao na wao pia.

“Mimi na wenzangu katika jumuiya tumekaa na kutafakari kwa dhati na kubaini kuwa mgogoro  ndani ya chama chetu hivi sasa umepata mashabiki wengi ambao hawakitakii mema, chama kinapambana na Dola, CCM na sisi kwa sisi,” alisema.

Alisema kwa wingi huo wa maadui chama kupata matokeo hayo si jambo la kushangaza, hali inayowaumiza vijana, hivyo ni vema kutafuta njia ya kukinusuru.

“Tunatoa mwito na kufungua milango kwa vijana wa CUF, kutafuta njia ya kukinusuru chama badala ya kukubali kutumika kukiangamiza kwa lengo la kumfurahisha mtu mmoja,” alisema.

 *Imeandikwa na Suleiman Msuya na Abrahama Ntambara.










Share on Google Plus

About Unknown

    Blogger Comment
    Facebook Comment

0 comments:

Post a Comment

Laptop City

Tangazo