CUF yahadharisha CCM, Dola


Abraham Ntambara

WAKATI CUF leo ikiadhimisha miaka 16 ya kumbukizi ya mauaji na ukiukwaji wa haki za binadamu, imeihadharisha CCM na Rais John Magufuli kutofanyia mzaha matumizi makubwa ya nguvu za Dola kuendesha shughuli za kidemokrasia na uchaguzi nchini.

Taarifa iliyotumwa jana kwa vyombo vya habari na Naibu Mkurugenzi wa Haki za Binadamu na Sheria wa CUF,  Pavu Abdallah Juma, ilisema wanalaani mauaji ya raia wasio na hatia na vitendo vyote vya ukiukwaji wa haki za binadamu vilivyofanywa na Serikali ya CCM.

“Jeshi la Polisi limeshindwa kutekeleza wajibu wake kwa misingi ya haki, sheria na uadilifu,  badala yake  linatumika kama mkono wa kulazimisha ushindi wa CCM katika uchaguzi na kufanya kazi zake kisiasa zaidi, badala ya kutanguliza uzalendo na weledi,” alisema Juma kwenye taarifa hiyo.

Aidha, iliitaka Serikali kutambua kuwa wananchi wamechoka uonevu na ukiukwaji wa haki za binadamu na wamechoka kunyanyaswa na kushindwa kuheshimiwa kwa mfumo wa siasa za vyama vingi nchini, misingi ya demokrasia na uchaguzi huru na wa haki.

Iliionya Serikali ya CCM na vyombo vya Dola kutoirejesha nchi kwenye matukio ya Januari 26 na 27, 2001 ambayo yalisababisha umwagaji wa damu na mauaji ya raia wasio na hatia. 

Alisema CUF itaendeleza juhudi za kuhakikisha migogoro ya kisiasa inapata ufumbuzi kwa njia ya kidemokrasia na amani, na kuunganisha Wazanzibari na Watanzania kwa  kuwa kitu kimoja na kutanguliza maslahi mapana ya nchi.

Aidha, ilitoa shukrani kwa viongozi, wanachama, wapenzi na wananchi wakazi wa Zanzibar kwa  uvumilivu ambao unadhihirisha ukomavu wa hali ya juu wa kisiasa, licha ya hujuma, mauaji, uchokozi na usumbufu wa makusudi uliofanywa na Jeshi la Polisi na vyombo vya Dola na vikosi vya ulinzi.

Taarifa ilieleza kuwa CUF itaendelea kushirikiana na vyama vingine vya siasa, wadau wanaounga mkono kuheshimiwa kwa demokrasia na misingi ya utawala bora ili kuhakikisha Serikali ya CCM inaheshimu  demokrasia na Watanzania wanapata tume huru za uchaguzi na Katiba inayotokana na ridhaa yao.

Ilibainisha, kwamba madai hayo yanaungwa mkono na jumuiya ya kimataifa ambayo ilishiriki kwenye uangalizi wa uchaguzi mkuu wa Oktoba mwaka juzi,  ambapo katika ripoti ya waangalizi wa Jumuiya ya Ulaya walipendekeza hadi 2020 matatizo yaliyopon yawe yamefanyiwa kazi.

Mwaka 2001 wanachama na wafuasi CUF walijitokeza kwenye maandamano ya kupinga matokeo ya Uchaguzi Mkuu wa mwaka 2000 na kudai Katiba mpya na tume huru za uchaguzi.
Share on Google Plus

About Unknown

    Blogger Comment
    Facebook Comment

0 comments:

Post a Comment

Laptop City

Tangazo