Mzee ruksa apinga kudai haki nje ya Mahakama


Abraham Ntambara

Ali Hassan Mwinyi
RAIS mstaafu wa Awamu ya Pili, Ali Hassan Mwinyi, amewataka wananchi wasioridhishwa na uamuzi wa kesi zao kukata rufaa katika mahakama za juu na kuachana na kudai haki katika vyombo vingine vya serikali nje ya Mahakama.

Rais Mwinyi alitoa kauli hiyo jana Dar es Salaam wakati wa uzinduzi wa wiki ya utoaji wa elimu ya mahakama kwa umma.

Alisema kuwa wananchi wengi hawana elimu ya sheria, hivyo kushindwa kujua hatua za kuchukua katika kudai haki baada ya mahakama kutoa hukumu ya kesi zao.

“Nakumbuka nikiwa Rais nilikuwa nikipokea malalamiko, ushauri wangu nautoa tena leo. Kama haukuridhishwa na uamuzi wa Mahakama, njia sahihi ni kukata rufaa katika Mahakama ya juu,” alisema Rais Mwinyi.

Aidha alisema kutokana na wananchi wengi kutokuwa na uelewa wa masuala ya sheria na taratibu za kimahakama, wamekuwa wakipoteza haki yao kwa kwenda kuidai nje ya chombo cha Mahakama.

Rais Mwinyi alisema ni ajabu kuona wananchi wakienda kudai haki ya kimahakama kwa mkuu wa mkoa ama wa wilaya, kitu ambacho siyo sahihi.

Alieleza pia kuwa ukosefu wa elimu ya kisheria, umekuwa ukichangia tabia ya watu kujichukulia sheria mkononi, hviyo ni vema katika wiki hii, wananchi wakapata elimu na kujua hatima yao katika kudai haki.

Kaimu Jaji Mkuu wa Tanzania, Profesa Ibrahim Juma aliwataka wananchi kufahamu kuwa Mahakama ni chombo ambacho kipo kwa ajili ya ustawi wao.

“Ibara ya Nane ya Katiba inasema, mwananchi ndiyo mwenye mamlaka ya mwisho na mihimili mitatu ya dola, Mahakama, Bunge, na utawala vipo kwa ajili ya ustawi wa mwananchi,” alisema Kaimu Jaji Mkuu Juma.

Aidha alisema kuwa sheria ni nyenzo muhimu ya kumwezesha mwanadamu kuishi katika jamii. Akawataka wananchi kutembelea vibanda mbalimbali katika wiki hii na kujifunza umuhimu wa utawala wa sheria.

Alisema katika mabanda hayo watapata kujua namna sheria zinavyofanya kazi na zote zikilenga kumsaidia mwananchi.

Kaimu Jaji Mkuu alisema mwananchi ni mtu muhimu katika sheria, hivyo sheria lazima ilenge katika kumnufaisha.

Alisema mwaka 2008 Kamisheni ya Umoja wa Mataifa ilisisitiza kuwa sheria zote za nchi lazima zijengwe katika kumwezesha masikini, mizani ya ubora wa sheria hupimwa kwa jishi inavyomsaidia mwananchi kutoka katika umasikini.

Share on Google Plus

About Unknown

    Blogger Comment
    Facebook Comment

0 comments:

Post a Comment

Laptop City

Tangazo