Seif: Serikali Z’bar inaninyanyasa


*Asema siku si nyingi atakuwa Rais

Fidelis Butahe

Maalim Seif Sharif Hamad
KATIBU Mkuu wa Chama cha Wananchi (CUF), Maalim Seif Sharif Hamad, amedai kuwa Serikali ya Mapinduzi ya Zanzibar (SMZ) inamnyanyasa, huku akisisitiza kuwa naye pia siku si nyingi atakuwa Rais.

Mbali na kauli hiyo aliyoitoa jana kupitia Kipindi cha Funguka kilichorushwa na Televisheni ya Azam, Seif alitaja mambo 12 yanayohusu mustakabali wake kisiasa na kufafanua mambo kadhaa yanayohusu mgogoro unaoendelea ndani ya CUF.

Katika kipindi hicho, Seif ambaye aligombea urais Zanzibar katika Uchaguzi Mkuu wa Oktoba 25 mwaka 2015 ambao ulifutwa na kurudiwa Machi 20, mwaka jana, aliulizwa takriban maswali 15 na mwongozaji wa kipindi hicho, Tido Mhando.

Maalim Seif alizungumzia kuhusu matibabu yake, baada ya kumaliza muda wake na kubainisha kuwa ameamua kujigharamia kutokana na sababu mbalimbali, ikiwamo kile alichoita uwezekano wa kunyanyaswa.

“Safari zangu zote za matibabu najilipia mwenyewe siombi serikalini. Siombi kwa sababu ukiwaambia wanakuwa na manyanyaso,” alieleza Seif na kuongeza;

“Nikasema nitajipeleka mwenyewe, matibabu yote ninayokwenda baada ya wadhifa wangu najilipia mwenyewe ingawa nina haki kikatiba ya kulipiwa.”

Seif alienda mbali na kutaja haki anazopata sasa kutoka serikalini akiwa kiongozi mstaafu kuwa ni kutumia gari la Serikali, mlinzi na kulipwa posho.

“Nilikuwa Makamu kwa Kwanza wa Rais, baada ya kustaafu kuna haki ambayo lazima nipate, wala hawafanyi hisani ni haki yangu,” alisema na kuzitaja haki hizo.

Akijibu swali lililomtaka aeleze kama bado anaota kuwa rais wa Zanzibar, Seif alijibu “tena si mbali,  natarajia muda mfupi ujao inshallah nitakuwa rais wa Zanzibar.”

Awali, akisisitiza kuhusu kuwania nafasi hiyo alisema, “ngoja tupate haki yetu (mahakamani) na mimi nikawa rais wa kuongoza Serikali ya Umoja wa Kitaifa, hapo ndio tutaona serikali ijayo itakuwaje.”

“Kwanza tuone tunafanikiwa au hatutafanikiwa ila baada ya hapo ninaweza kufanya maamuzi. Sasa ninajua tutafanikiwa. Kugombea 2020 ni jambo ambalo ni lazima,  tusubiri muda ufike tuone na hali ya kisiasa. CUF haijadhoofika.”

Seif amegombea urais Zanzibar mwaka 1995, 2000, 2005, 2010, huku mwaka 2015 ndoto zake zikiyeyuka baada uchaguzi kufutwa kutokana na sababu mbalimbali zilizotolewa na Mwenyekiti wa Tume ya Uchaguzi Zanzibar (ZEC), Jecha Salim Jecha.

Jecha aliitangaza Machi 20, mwaka jana kuwa siku ya marudio ya uchaguzi huo ambao ulisusiwa na CUF kwa sababu ni kinyume na sheria na Katiba jambo lililoipa mwanya CCM kuibuka na ushindi  wa zaidi ya asilimia 95.

Katika kipindi hicho cha saa moja, Maalim Seif alizungumzia mgogoro wa CUF ulioibuka baada ya mwenyekiti wa chama hicho, Profesa Ibrahim Lipumba kutambuliwa na Ofisi ya Msajili wa Vyama vya Siasa, kusisitiza kuwa msomi huyo alipojiuzulu taratibu zilifuatwa, hawezi kupewa nafasi nyingine.

Mambo mengine aliyoyazungumzia ni kesi zilizopo mahakamani, Waziri Mkuu wa zamani Edward Lowassa kujiunga Ukawa, Lipumba kutumiwa na dola, uchaguzi mdogo, kasoro uchaguzi wa ubunge jimbo la Dimani Zanzibar sambamba na Uchaguzi Mkuu uliopita.

Nyingine ni maridhiano Zanzibar, Serikali ya Umoja wa Kitaifa (SUK), ruzuku ya chama hicho pamoja na jinsi anavyozunguzwa katika kulipiwa fedha za matibabu licha ya kuwa alikuwa Makamu wa Kwanza wa Rais Zanzibar.

Mgogoro CUF

Akizungumzia mgogoro CUF alisema kundi linaloongozwa na Profesa Lipumba ndio linalozua tafrani katika chama hicho huku wakisaidiwa na Ofisi ya Msajili.

“Tulimsihi Lipumba asijiuzulu, lakini alishikilia msimamo wake. Hakufukuzwa alijiuzulu mwenyewe na baada ya miezi 10 anaandika barua kwamba anatengua uamuzi wake, jambo hili sijawahi kuliona duniani,” alisema.

Huku akieleza jinsi CUF kilivyoshindwa kukutana kwa wakati muafaka kupitia mkutano mkuu wake kujadili barua ya Lipumba kujiuzulu kwa sababu ya kukabiliwa na ukata, Maalim Seif alisema mkutano huo ulifanyika baadaye na uamuzi ukatolewa kwa kufuata Katiba ya chama hicho.

“Hatukubaliani na msajili ndio maana tumefungua kesi Mahakama kuu ili tupate tafsiri ya uamuzi huu. Msajili hawezi kutengua uamuzi wa kikao halali cha chama, hatukuridhika na uamuzi wake,” alisema.

Alisema iwapo CUF kitashindwa katika kesi hiyo watakubaliana na uamuzi huo licha ya kuwa watakuwa na nafasi ya kukata rufaa katika Mahakama ya rufaa.

Akijibu hoja zilizowahi kutolewa na Lipumba kuwa alijizulu baada ya kuchukizwa na kitendo cha Ukawa kukubali Lowassa  agombee urais alisema, “Lipumba hana msimamo. Yeye ndio aliyemleta Lowassa, akasema akija kwetu atatusaidia na tulikubaliana Lowassa atakuwa mgombea wetu hapo ndio akabadilika.”

“Hana nia njema alidhani akijiuzulu watu wengi watamfuata ila haikuwa hivyo. CUF bila Lipumba huku ikishirikiana na Ukawa imefanya vizuri zaidi, imeshinda majimbo 10 Tanzania Bara. Tulipata Halmashauri za wilaya nne na nyingine tano kwa kushirikiana na wenzetu wa Ukawa.”

Alisema katika katika uchaguzi mdogo uliofanyika wiki iliyopita Lipumba alisimamisha wagombea katika kata 11 na kushindwa huku wagombea wakipata kura kati ya 10 hadi 15.

Maridhiano

“CCM hawakubali matokeo ya Oktoba 2015 ambayo yalifutwa kinyume na sheria na taratibu, sisi hatukubali matokeo ya Machi 20 mwaka jana kwa sababu yalifanyika kinyume na Katiba. Hapo lazima tutafute njia ya kutoka na lazima tuzungumze na upande wa pili,” alisema.

Akizungumzia jinsi walivyokutana na Rais mstaafu Zanzibar, Aman Abeid Karume na kukubaliana kuunda Serikali ya Umoja wa Kitaifa (SUK), alisema lengo lilikuwa ni kuwafanya wananchi kuwa kitu kimoja na ndio ukawa msingi wa kufanyika kwa mabadiliko ya 10 ya Katiba ya Zanzibar.

“Inawezekana kwa sasa tukarejesha SUK kama kutakuwa na nia njema kwa kila upande ukubali Zanzibar kuna tatizo na haja ya viongozi kupata ufumbuzi wa matatizo ili kushirikiana pamoja. Miaka mitano iliyopita mambo yalikwenda vizuri ila kwa sasa ugomvi na uhasama umerudi. Hakuna dawa Zanzibar isipokuwa vyama kushirikiana,” alisema.

Ruzuku

Kuhusu Ofisi ya Msajili kutoa ruzuku kwa kundi la Profesa Lipumba alisema, “nilimuandikia barua kuhoji sababu za kutopewa ruzuku akanijibu kwamba kazuia ruzuku kwa sababu chama kina mgogoro cha ajabu akaruhusu upande wa Lipumba upate ruzuku.”

Alisema fedha hizo zimekwenda katika akaunti ambayo yeye haijui wala Bodi ya Wadhamini ya chama hicho na huku akihoji jinsi ukaguzi wa fedha hizo utakavyofanywa na Mdhibiti na Mkaguzi wa Hesabu za Serikali (CAG).

“Hata mimi Msajili ananitambua, iweje fedha ampe mwenyekiti asiyehusika na masuala ya fedha. fedha hizi zitakaguliwa vipi? Fedha za chama zilikuwa zinakwenda kwenye akaunti inayotambulika si akaunti mpya,” alisisitiza.

Alisema wamemuandikia barua Msajili, Gavana wa Benki Kuu ya Tanzania (BoT) na Taasisi ya Kuzuia na Kupambana na Rushwa (Takukuru), kwamba wanatarajia kufungua kesi kupinga jambo hilo.
Share on Google Plus

About Unknown

    Blogger Comment
    Facebook Comment

0 comments:

Post a Comment

Laptop City

Tangazo