Serikali yasubiri Jiji kuhusu fedha za Uda


Hussein Ndubikile

George Simbachawene
WAZIRI wa Nchi Ofisi ya Rais, Tawala za Mikoa na Serikali za Mitaa, George Simbachawene, amesema Serikali inasubiri taarifa za uamuzi wa Halmashauri ya Jiji la Dar es Salaam juu ya fedha za mauzo ya Shirika la Usafiri la Dar es Salaam (UDA) ndipo iamue.

Hatua hiyo imekuja baada ya Rais John Magufuli kutoa agizo la siku tano kwa Jiji hilo kuzipangia matumizi Sh bilioni 5.8 zilizopatikana baada ya shirika hilo kuuzwa na ikishindwa litoe taarifa kwa Serikali izipangie kwa kuzipeleka.

Hata hivyo, siku tano zimemalizika na hakuna kiongozi wa Jiji aliyetoa taarifa za wapi fedha hizo zitaelekezwa na sababu zipi zinakwamisha utekelezaji wa agizo hilo.

Akizungumza na gazeti hili kwa simu jana, Waziri alisema baada ya siku hizo kwisha wanasubiri taarifa rasmi kutoka Jiji kwa lilichoamua ndipo Serikali iamue wapi fedha hizo zielekezwe.

“Nasubiri kupata taarifa rasmi kutoka Jiji la Dar es Salaam juu ya walichoamua, ili Serikali ichukue uamuzi,” alisema.

Uongozi wa Jiji uliopita uliuza shirika hilo kwa kampuni ya Simon Group kwa kiasi hicho cha fedha, matokeo yake kuliibuka mzozo mkubwa bungeni kwa madai kuwa kiwango hicho hakilingani na thamani halisi ya mali za UDA.

Mbali na mzozo huo, kulitokea hali ya kutoelewana na kutoleana lugha za matusi kati ya wabunge wa Dar es Salaam na aliyekuwa Meya wa Jiji hilo, Didas Masaburi.
Share on Google Plus

About Unknown

    Blogger Comment
    Facebook Comment

0 comments:

Post a Comment

Laptop City

Tangazo