Bosi Jamii Forums aanika ubaya wa Sheria



Suleiman Msuya

MKURUGENZI wa Jamii Media, Maxence Melo, amesema kinachokuta baadhi ya Watanzania akiwamo yeye kufunguliwa kesi kinaweza kutokea kwa waandishi wa habari siku yoyote kutokana na Sheria ya Mtandao ya Mwaka 2016 ilivyo.

Melo alisema hayo juzi wakati akichangia semina iliyoandaliwa na Shirika la Kimataifa la Internews kuhusu Sheria ya Takwimu ya Mwaka 2015 na Sheria ya Mtandao.

Alisema tangu awali walipinga sheria hiyo kuwasilishwa kwa hati ya dharura na kupitishwa bila wabunge kuwa na uelewa wa kilicho ndani yake, hali ambayo leo inaumiza watu wengi.

Mkurugenzi huyo ambaye anakabiliwa na kesi mbalimbali, alisema ni jukumu la kila mwanahabari kutambua kinachowakuta sasa, kuwa ni kutokana na sheria hiyo ambayo ina upungufu kadhaa.

“Kinachotokea leo ni matokeo ya vyombo vya habari kujitoa na kuona kuwa Sheria ya Mtandao ya 2016 haitawagusa, hivyo wakati sisi tunalalamika wanatuacha wenyewe ila nadhani kila kitu kinaonekana,” alisema.

Melo alisema ni Tanzania pekee ambako Jeshi la Polisi linapewa mamlaka ya kutaka kujua mtoa habari, hivyo ni dhahiri kuwa hakuna aliye salama.

Alisema mwaka 2017 unaweza kuwa mgumu kwa tasnia ya habari na kuwa dalili zilianza baada ya sheria hiyo kupitishwa.

Mkurugenzi huyo alisema sheria hiyo inagusa kila eneo ambalo linahusu mawasiliano ya simu, ujumbe mfupi na hivyo hata wanaotumia mtandao wa WhatsApp hawako salama.

Alibainisha kuwa watumiaji wa simu kwa ujumla ni waathirika wa sheria hii bila kujali matumizi ya mtandao au simu ya kawaida.

Akitoa mada katika semina hiyo, Mwanasheria wa Mtandao wa Watetezi wa Haki za Binadamu Tanzania (THRDC), Deogratius Bwire alisema sheria hiyo haifai hata kipengele kimoja huku akikitaja kipengele cha 16 kuwa chenye upungufu mwingi.

Alisema tangu sheria hiyo ipitishwe jumla ya kesi saba zimefunguliwa na kufikisha  mahakamani zaidi ya watu 50 na wengine kuhukumiwa.

Mwanasheria huyo alisema watu walioshitakiwa na kuhukumiwa sababu kubwa ni kuandika ujumbe kwenye kurasa zao na makundi ya WhatsApp, hivyo waandishi wanapaswa kuwa makini.

“Watu hao walikamatwa chini ya kifungu cha 16, kinachuzungumzia kuchapisha na kusambaza taarifa au takwimu au habari katika mfumo wa maneno au alama,” alisema.

Alisema baadhi ya kesi ni zinazohusu ndugu kujadili masuala ya siasa katika kundi lao la nyumbani.
Bwire aliwataja wengine walioshitakiwa kuwa ni Erico Nyerere, Israel Willium, Habakuk Emily na wafanyakazi ambao walitumika kama waangalizi wa TACCEO na Kituo cha Sheria na Haki za Binadamu (LHRC).

“Kifungu cha 32 kinalazimisha kusaidia Polisi kutoa taarifa za wachangiaji wa mtandao wake kama Jamii Forums, nadhani mnaona ugumu uliopo,” alifafanua.

Aidha, alisema kifungu cha 31 kinawapa polisi mamlaka ya kuingia bila ruhusa ya Mahakama na kuchukua kompyuta za ofisi husika.
Share on Google Plus

About Unknown

    Blogger Comment
    Facebook Comment

0 comments:

Post a Comment

Laptop City

Tangazo