Wananchi wagomea taarifa ya mapato, matumizi


John Banda, DODOMA

WANANCHI wa kata ya Msalato katika Manispaa ya Dodoma jana wamegomea taarifa ya mapato na matumizi iliyosomwa na Ofisa Mtendaji, Herman Malindila na kusababisha vurugu kubwa kwenye mkutano wa hadhara uliofanyika katika eneo la Mnadani.

Katika mkutano huo uliofurika umati wa wakazi wa eneo hilo, wananchi walimtaka mwakilishi wa mkuu wa wilaya, Vicent Leo kuondoka na Ofisa Mtendaji huyo ili na wao washughulike na Diwani wa Kata, Alli Mohamed  na wenyeviti watatu wa mitaa.

Chanzo cha vurugu hizo zilitokana na wananchi kuzipinga taarifa ya diwani na Ofisa Mtendaji wake ambao kwa nyakati tofauti walisoma taarifa ambazo zilijaa udanganyifu, huku Mwenyekiti wa Mtaa wa Msalato Emanuel Mazengo wakipingwa hadharani kuhusu kutolewa kwa ardhi kwa mwekezaji.

Kata ya Msalato ambayo ni maarufu kwa kuwepo mnada ina vyanzo vingi vya mapato, lakini kwa zaidi ya mwaka mmoja sasa wananchi wamedai kuwa hawajasomewa taarifa ya mapato na matumizi.

Diwani Mohamed alikanusha madai ya kuuza ardhi wala kuitoa kwa mwekezaji licha ya mwekezaji huyo ambaye alijitambulisha kuwa ni mkazi wa eneo hilo kutamka hadharani kuwa alichukua ardhi hiyo kwa kupewa na viongozi akiwemo diwani.

“Ndugu zangu ninawahakikisheni kuwa mimi sihusiki na wala sijashirikishwa na jambo lolote, kesho nitakuwa ofisini hivyo naomba Mwenyekiti na mwekezaji aliyemtaja kwa jina la Paloline Erenest  waje ofisini tuzungumze vingine nitawapeleka polisi kwa mujibu wa sheria kwa kuwa mnaninzingizia ” alisema Mohamed.

Naye Mwenyekiti wa mtaa huo wa msalato A Emanuel Mazengo alikanusha kuuza ardhi hiyo lakini akasema alikuwa akijua kilichokuwa kinaendelea chini ya mwekezaji huyo ambaye alikuwa amesaidia pia pamoja na kuchonga barabara ndani ya mtaa wake.

Kwa upande wake Mtendaji Malindila alisoma mapato ya machinjio tu lakini alipoulizwa maswali mengi alikosa majibu hivyo akashindwa kusoma mapato mengine ikiwemo pango la minara ya simu, gulio na vyanzo vingine.

Mwakilishi wa Mkuu wa wilaya aliamuru mkutano huo kufungwa baada ya kelele nyingi ambazo zilisababishwa na mapungufu katika usomaji wa taarifa hasa ya mapato na matumizi iliyowasilishwa na Mtedaji.

Leo aliwataka wananchi kutokuchukua sheria mkononi ikiwemo ya kufunga ofisi kama walivyotaka kwani litakuwa ni kosa na badala yake wasubiri majibu kutoka kwa mkuu wa wilaya na uongozi wake juu ya jambo hilo.

Hata hivyo suala hilo kwa upande wa wananchi liliwalazimu  kupaza sauti wakimtaka mwakilishi huyo kuondoka na watumishi hao ili uongozi wa Manispaa upeleke timu ya kuwachunguza zaidi akiwemo mkaguzi wa hesabu za ndani kwani fedha nyingi walihisi zimeliwa.
Share on Google Plus

About Unknown

    Blogger Comment
    Facebook Comment

0 comments:

Post a Comment

Laptop City

Tangazo