Makundi CUF yagongana vichwa kuhusu ruzuku


Suleiman Msuya

Magdalena Sakaya
HATUMTAMBUI, tunamtambua. Hivyo ndivyo unavyoweza kusema kutokana na kauli za kutofautiana za makundi mawili ya viongozi wa CUF, kuhusu maazimio ya Bodi ya Wadhamini wa chama hicho.

Wakizungumza na JAMBOLEO jana kwa nyakati tofauti, viongozi hao walitofautiana kuhusu Bodi huku CUF ya Mwenyekiti Profesa Ibrahim Lipumba ikijinadi kuwa haitambui Bodi na ya Mwenyekiti wa Kamati ya Uongozi, Julius Mtatiro ikisema anaitambua.

Tofauti hizo zinakuja siku moja baada ya Bodi hiyo kufanya kikao juzi na kukubaliana kufunga akaunti zote za chama hadi mgogoro utakapomalizika kwa ilichodai ni fedha za chama kuibwa.

Naibu Katibu Mkuu Bara ambaye anatajwa kuwa timu ya Lipumba, Magdalena Sakaya, alisema kwa mujibu wa Katiba ya CUF, Bodi hiyo ilimaliza muda mwaka jana na kukiri kuwa haijachaguliwa nyingine kutokana na mgogoro uliopo.

Sakaya alisema anaamini Bodi hiyo kwa sasa haina mamlaka yoyote ya kuzuia au kufunga akaunti za chama.

“Bodi hiyo haina mamlaka kisheria na kwa mujibu wa Katiba ya CUF, kwani muda wake ulikwisha Januari mwaka jana, hivyo inachokifanya ni kujifurahisha, kwani sisi tunaendelea kujenga chama,” alisema.

Kuhusu utaratibu waliotumia kuchukua fedha za ruzuku, Sakaya alisema waliomba fedha hizo kwa yeye kuandika barua kwa Msajili ili chama kishiriki uchaguzi mdogo na shughuli zingine za kiofisi.

Naibu Katibu Mkuu huyo alisema ni dhahiri mgogoro ndani ya CUF unawaathiri hivyo kutaka pande zinazokinzana kuachana nao.

Aidha, Sakaya alihoji iwapo kuna upande ambao unahoji wao kutoa fedha hizo ni kwa nini hauelezi sababu za wao kutoa Sh milioni 86 na kuzitumia bila kuwashirikisha wao.

Mtatiro alikiri Bodi hiyo kumaliza muda wake kikatiba lakini bado inafanya kazi kwa sababu hakuna Bodi mpya.

Alisema ukomo wa Bodi hiyo utafikiwa Baraza Kuu la CUF litakaa na kuteua wajumbe wengine kitu ambacho hakijafanyika hadi sasa.

“Kama anasema Bodi iliyopo si halali ni ipi halali ambayo imeingiliwa na hii iliyopo, kimsingi wana mamlaka ya kufunga hizo akaunti, kwani likitokea tatizo wao ndio wanashitakiwa na wakiona tatizo wao ndio wanashitaki,” alisema.

Kuhusu Sh milioni 86 zilizotolewa chini yake, Mtatiro alisema zilitolewa kwa kufuata utaratibu hivyo kama kuna mtu anahoji, afuate taratibu kama wanavyofanya kuhoji Sh milioni 369 zilizotolewa na Lipumba.

Aidha, alisema CUF haijaathirika kutokana na Ofisi ya Msajili wa Vyama vya Siasa kuzuia ruzuku na kubainisha kuwa wanapata michango kwa wabunge, madiwani na wadau wengine ambao wanakipenda chama chao.

Mwenyekiti wa Bodi, Abdallah Katao alisema kwa sasa wako kwenye mchakato wa kufungua kesi na suala la uhalali wao liko chini ya baraza la uongozi.

Kwa upande wake Msajili wa Vyama vya Siasa, Jaji Francis Mutungi alisema hayuko tayari kuzungumzia mgogoro wa CUF na kuwa wakati ukifika atafanya hivyo.

Kwa takribani miezi minne sasa, CUF imekuwa kwenye hali ya sintofahamu ambapo kumeibuka na makundi mawili yanayosigana; moja la Lipumba na lingine likijinadi kuwa la wafia chama.
Share on Google Plus

About Unknown

    Blogger Comment
    Facebook Comment

0 comments:

Post a Comment

Laptop City

Tangazo