Taasisi ya Kikwete kuchunguza nyoyo shuleni


Salha Mohamed

TAASISI ya Moyo ya Jakaya Kikwete (JKCI) inatarajia kwenda shuleni kufanya uchunguzi ili kubaini wenye matatizo ya moyo.

Hatua hiyo imekuja baada ya JKCI kubaini watoto kati ya miaka 10 hadi 18 ndiyo waathirika wa milango ya moyo huku ikifanya upasuaji wa kubadilisha milango ya moyo (valves) ambayo haipitishi damu vema.

Hayo yalibainishwa Dar es Salaam jana na Mkurugenzi Mtendaji wa JKCI, Dk Bashiri Nyangasa wakati akizungumza na waandishi wa habari kuhusu upasuaji uliohusisha uvunaji wa mishipa ya damu mguuni na kupandikiza katika mishipa ya moyo.

Upasuaji huo wa siku tano ulifanyika kwa wagonjwa sita ulishirikisha jopo la madaktari kutoka hospitali ya Apolo, Bangalore, India.

“Tuna mpango wa kuzungumza na shule na kaya kwa ajili ya kupata wagonjwa kwa ajili ya upasuaji, wagonjwa wengi ni kati ya miaka 10 hadi 18 ndiyo waathirika wakubwa wa kuharibika kwa milango ya moyo,” alisema.

Alisema: “Upasuaji huu ulifanyika bila kutumia mashine ya mapafu na moyo. Tumemfanyia mgonjwa upasuaji wa milango miwili ya moyo ambayo iliharibika sana”.

Alisema ubadilishaji wa milango hiyo iliyoharibika ulifanyika kwa kutanuliwa kishina cha mshipa mkubwa wa moyo kwa kutumia mfuko wa moyo.

Dk Nyangasa alisema kupitia upasuaji huo, Serikali iliokoa Sh milioni 174 kama ingepeleka wagonjwa India.

Mkurugenzi wa Tiba ya Afya ya Moyo JKCI, Dk Peter Kisenge alisema kwa kuanza mwaka wameanza na kambi ya Apolo ambapo wiki ijayo watakuwa na kambi ya madaktari wa Marekani.

“Wao watafanya tiba ya moyo bila upasuaji na kuweka kizibua njia kwa wagonjwa 15 kuanzia Januari 23 hadi 29. Februari 4 watakuja wa Saudi Arabia ambao watafanya matibabu bila kupasua moyo kwa wagonjwa 55,” alisema.

Akizungumza kwa niaba ya jopo la madaktari wa Apolo, Dk Sathyaki Nambala alisema ni mara ya nne kufanya upasuaji hospitalini hapo kulikokuwa na upungufu wa madaktari na vifaa.

“Tulipokuja mara ya mwisho kulikuwa na upungufu wa vifaa na madaktari lakini sasa vyote vipo, kikubwa ni kushirikiana na timu kufundishwa  upasuaji na kupata elimu zaidi,” alisema.

Alisema wanatarajia kuona madaktari hao wakijitegemea katika kufanya upasuaji mgumu zaidi huku akiitaka Serikali kupeleka madaktari nje ya nchi kujifunza ili kupunguza gharama za kupeleka wagonjwa nje ya nchi. 

Share on Google Plus

About Unknown

    Blogger Comment
    Facebook Comment

0 comments:

Post a Comment

Laptop City

Tangazo